Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana niweze kupata nafasi hii ya kuchangia kwenye Wizara hii ya kilimo, Wizara muhimu sana kwa ustawi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt, Samia Suluhu Hassan na wasaidizi wake wote katika Wizara hii ya kilimo kwa sababu tangu ameingia madarakani ameonesha utashi wa moja kwa moja wa kumkomboa mkulima, kumuondoa mkulima wa kitanzania kutoka katika kuwa mtu ambae tunamtoa sadaka pale ambapo tunapata changamoto bila kujali tunamuumiza kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niende moja kwa moja kwenye ninachotaka kuzungumzia. Nitazungumzia huu mradi wa BBT au jenga kesho iliyo bora ambayo kimsingi inaangalia zaidi ushiriki wa vijana na wanawake katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Mbunge mwakilishi wa Vijana na nimeingia katika Bunge hili kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi na ahadi namba sita ya mwanachama yeyote wa Chama cha Mapinduzi, ni kujielimisha kwa kadri ya uwezo wangu na kutumia elimu yangu kwa maslahi ya wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya Mheshimiwa Bashe, kuja na jambo hili la Mradi huu wa BBT nilichukua jukumu la kujielimisha na kugundua jambo hili si jipya. Watu wengi waneweza kuona ndoto za Mheshimiwa Bashe na wasaidizi wake ni kama Ndoto za Alinacha au Hekaya za Abunuwas lakini sisi sio wa kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo hayo yalianza kufanyika katika Nchi ya Malaysia mwaka 1956, chini ya mradi ulioitwa FELDA au Federal Land Development Authority. Mradi huu kadri tunavyoongea leo unachangia asilimia 18 ya GDP ya nchi hii. Leo hii tunapozungumza ni moja ya mradi ambao unamiliki sekta kubwa sana ya uzalishaji katika nchi hiyo, ni mradi ambao umeifanya Malaysia iwepo katika nchi ambazo zinaongoza kwa uzalishaji wa palm oil duniani. Lakini ni mradi ambao umekwisha ondoka katika kupewa grants za Serikali na leo hii tunazungumza unapewa mikopo na Benki ya Dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Bashe, kwa sababu pamoja na uwepo wa wimbi kubwa la watu wasio na imani na mradi huu hajarudi nyuma. Nimpongeze kwa sababu amechukua initiative ya kutuamini vijana na wanawake wa Kitanzania kwamba tukishikwa mkono na kuwezeshwa na Serikali, tunaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme nasikitishwa sana kwa sababu kama sisi Wabunge ambao ni wawakilishi na kwenye majimbo yetu tuna vijana, sensa iliyofanyika mwaka 2022, inaonesha zaidi ya asilimia 34 walioko katika nchi hii ni vijana lakini sisi Wabunge hatuwaamini vijana, nani atuamini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili si jipya na katika haya nina machache ya kushauri na ninaamini tukienda pamoja Mheshimiwa Bashe, Mheshimiwa Rais, pamoja na wasaidizi wao tunakwenda kufanikiwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la recruitment, namna ambavyo vijana hawa wamepatikana. Yalitolewa matanzangazo na vijana waliomba kupitia mitandao na takwimu zinaonesha zaidi ya vijana 20,000 waliomba. Lakini wengi wa hawa walioomba wanatokea katika Jiji la Dar es salaam kuliko majiji mengine au mikoa mingine ya nchi hii. Hii inaonesha kwamba ilikuwa kama survival for the fittest. Watu wa Dar es salaam wana mtandao kwa karibu zaidi ndio maana wameweza kuomba wengi zaidi na kuchaguliwa kwa wingi zaidi. Kwa hiyo, nimuache Mheshimiwa Bashe na wasaoidizi wake, kipindi kijacho wanapokuja kuchukua vijana hawa wahakikishe wanawachukua vijana kwa namna ambayo itatoa fursa sawa kwa vijana wote wa nchi hii kuweza kuomba na kupata fursa hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee mimi niombe, mashamba haya yanapoanzishwa basi wajitahidi kuhakikisha kwamba yanaanzishwa katika kanda zote za nchi hii na hawa vijana wanapokuwa posted wawe posted katika Kanda zao. Tukiwapeleka mbali kama tunavyofanya sasa hivi ina risk vijana kuweza kutelekeza mashamba yale na kurudi nyumbani pale mambo yanapokuwa magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana tuhakikishe kwamba tunakuwa na mashamba haya katika kanda mbalimbali lakini hata kule tusipoweza kuanzisha mashamba haya, basi tuanzishe vitalu nyumba ili tutoe fursa sawa kwa vijana kushiriki katika kilimo kutoka kila sehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto moja wapo kubwa zaidi katika mradi huu ni suala la ardhi. Wenzetu wa Malaysia waliweza kwa sababu inamiilikiwa na Crown. Kwa hiyo, wenyewe ilikuwa ni rahisi sana kwa Mfalme na wasaididzi wake kutoa ardhi na kuwapa watu. Kwetu sisi jambo hili ni tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, naomba sana pale ambapo wizara inakuja kutujibu, ituambie namna bora ambayo inafikiria itaweza kutumia ardhi ndogo tuliyonayo kuwasaidia vijana wengi ambao wanazidi kuongezeka siku kwa siku. Takwimu za Sensa zinaonesha pamoja na kwamba asilimia 34 ni vijana lakini asilimia 44 ni wale walio chini ya miaka 18 na hawa tunawategemea ni vijana wa kesho. Wizara ije utuambie ni namna gani inafikira kutumia ardhi ndogo tuliyonayo ambayo haiongezeki, kuwasaidia hawa tulio nao na hawa ambao wanakuja ku-graduate na kuwa vjana wa kesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu unaonekana utakwisha mwaka 2030, ninaiomba sana Wizara, iangalie namna ya kutengeneza uendelevu wa huu mradi. Kama kule ambako tumejifunza wao wameanza tangu mwaka 1956, mpaka leo tunavyozungumza mradi huu upo na unaendelea na umejenga mabilionea wengi sana kutoka Malaysia. Naomba pia Serikali iangalie namna gani ya kuendelea kutengeneza uwezekano wa Mradi huu kuendelea hata baada ya mwaka 2030 ili vijana wa Kitanzania waendelee kunufaika, vijana wa Kitanzania waendelee kuvutiwa na kilimo, waendelee kuweza kusaidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilikuwa naomba kwa vile bajeti inayotumika au iliyotengwa katika mradi huu ni kubwa lakini bajeti kubwa zaidi imeenda kutengeneza foundation. Nilikuwa naishauri Wizara iangalie namna ya kupeleka mradi huu kwanza kwa mwanzo katika mikoa ambayo ina vyanzo vya maji vya uhakika ili tuweze kupunguza gharama za mwanzo za mradi na fedha nyingi zaidi iende kutumika kwa vijana moja kwa moja kuliko kutengeneza miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia Mheshimiwa Bashe, aangalie namna ambayo ata-link mradi huu na vijana wanaotoka vyuo na vyuo vikuu na a–link na vijana wanaotoka JKT ili kuweza kutumia mashamba haya kuweza kuwasaidia vijana hawa ambao tayari Serikali imekwishatumia fedha nyingi kuwaelimisha, tayari Serikali imekwishakutumia fedha nyingi kuwapa mafunzo hawa JKT na wao waje walisaidie Taifa lao waweze kuwa na kesho iliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee niombe, changamoto kubwa ya mkulima wa kitanzania ni suala la soko, niombe sana katika mradi huu Mheshimiwa anapokuwa anaangalia namna ya kutengeneza basi ahakikishe vile vyote vinavyozalishwa vinaweza kupata soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nakuomba sana… naunga mkono hoja.