Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nichangie hoja ya Wizara ya kilimo ambayo iko mezani kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza Mawaziri, Bashe na Mheshimiwa Mavunde, kwa kazi nzuri ambayo wanyoifanya. Ni Mawaziri wachapakazi, wabunifu na ni wasikivu na wanafikika kwa urahisi. Kipekee nimpongeze na nimshukuru Mheshimiwa Rais, kwa maono yake na jinsi anavyopeleka fedha nyingi kwa sekta hii ya Kilimo na amepelekea sasa hivi bajeti yetu kuongezeka mpaka hiyo bilioni 970. Tunakupongeza sana Mheshimiwa Rais na ni matarajio ya wakulima sasa kwamba sekta hii sasa italeta manufaa ambayo sisi Wabunge kila mwaka tulikuwa tunalilia kwamba bajeti ya sekta ya kilimo iongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nitajikita kwenye uchangiaji ukurasa wa 169. Ukurasa wa 169 wa bajeti umezungumzia suala la kuongeza thamani. Nitazungumzia uongezaji wa thamani wa zao la Korosho, na kwenye korosho wenzangu waliotangulia kuchangia wamezungumzia changamoto. Kwenye Korosho kuna changamoto nyingi na zimekwisha tajwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye korosho kuna changamoto ya kupungua kwa uzalishaji, tumeona kwa kipindi cha miaka mitatu sasa hivi uzalishaji unapungua mwaka hadi mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye korosho kuna bei ndogo kwa mkulima ambayo haina tija, ambayo sasa hivi kwa muda wa miaka miwili kwenye minada yetu mkulima hapati bei ambayo inatija kwake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye korosho tumeshuhudia utitiri wa makato na tozo ambayo hatimaye inapunguza bei kwa mkulima. Pia, kwenye korosho ni zao pekee ambalo lina export levy. Hili nazungumzia kwa sababu export levy baadae inapunguza bei kwa mkulima, sio kwamba inalipwa tu na mfanyabiashara lakini anayeumia baadae ni mkulima anapokwenda sokoni kwamba bei yake inapunguzwa .

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Wizara kwa kuja na mwarobaini, inasema kwamba zimetengwa fedha bilioni 10 ili Bodi ya Korosho ipelekwe kwenye private sector kwa ajili ya kujenga kiwanda cha kubangua korosho. Huu ni mpango mzuri na suluhisho la kuuza korosho ghafi. Kwa sababu tukiendelea kuuza korosho ghafi wakuilima wetu hawafaidiki lakini tukiuza korosho karanga tutapata bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikupongeze Mheshimiwa Bashe, kwa wazo lako sasa la kuingia kwenye ubanguaji. Lakini tamko hili Mheshimiwa Bashe, nikushauri kwamba hii ni vita ya kibiashara. Kwa sababu kuna nchi duniani hawapendi Tanzania wauze Korosho karanga, wanataka kila mwaka wauze korosho ghafi kwa sababu ni ajira kwa wananchi wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanachukua korosho yetu na kupeleka nchini kwao na wanatengeneza ajira. Kwa hiyo, hili tamko ambalo umelitoa na kwenye mkutano wetu wa wadau wa korosho ulisema msimu wa 2025/2026 utakuwa ni mwisho wa kupeleka korosho ghafi, ina maana korosho yote itabangulia hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakuomba sasa tuwe na maadalizi ya kutosha. Tusipokuwa na maandalizi ya kutosha tutavurugwa, kwa sababu kama nilivyosema kuna nchi ambazo hawako tayari kuwekeza Tanzania kwa ajili ya kubangua korosho. Wanataka kila mwaka tupeleke korosho ghafi kwa sababu inatoa ajira kwao. Kwa hiyo, wao kwa gharama yoyote hawako tayari kuona Tanzania sasa inaanza ubanguaji. Kwa hiyo, tufanye vetting wakati wa kuwapata watu hao watakaoingia kwenye private sector wawe na nia ya kuwekeza na kubangua Tanzania. Kwa sababu tuna uzoefu wa viwanda 12 vya zamani, tulifungua viwanda 12 lakini baada ya muda mfupi vikafungwa. Haya vile viwanda vilibinafsishwa mpaka leo viwanda vile havifanyi kazi ni magodauni tu. Kwa hiyo, lazima tuwafanyie vetting ambao tutakuwa nao katika uwekezaji, la sivyo kutakuwa na changamoto kama ilivyokuwa zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile, hawa wawekezaji lazima tuwape motisha. Tupunguze kodi ya mitambo wakati wanapoingia ili kupunguza gharama ya uwekezaji. Tukifanya hivi tutapata wawekezaji ambao ni serious, watakuwa na mtaji mkubwa na wataingia kwenye ubanguaji serious.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Mheshimiwa Waziri, nikushauri kwamba wakati hao wawekezaji wanaendelea na shughuli zao za uwekezaji basi tuwe na forum za kuasikiliza ili pale wanapopata changamoto waweze kusikilizwa. Kwa mfano; sasa hivi kuna changmoto ya upatikanaji wa kosrosho kwa wabanguaji wa ndani, tuna mfumo wa soko la awali ambao unalalamikiwa, ni vizuri Waziri ukakaa na hao wenye viwamda ukatafuta mfumo ambao hautashusha bei kwenye minada, mfumo ambao hautapunguza bei kwa mkulima ili na wao wapate korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye suala la umwailiaji. Nimeona hapa umesema kwamba umeingia mikataba 22 kwa ajili ya kuanza umwagiliaji katika mabonde mbalimbali, hili ni wazo zuri. Kipekee kuna Bonde la Ruvuma Basin, ambalo linaanza Songea, Namtumbo, Tunduru, Masasi, Mtwara. Bonde hili bado hatujalitumia ipasavyo, lina kilometer square 60,000. Kwa hiyo, naomba yule mkandarasi ambae amepewa kazi ya kufanya usanifu aanze songea mpaka Kilambo – Mtwara Vijijini. Tukifanya hivyo tutatoka na Mradi ambao utasaidia Ruvuma Basin. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani? Mto Ruvuma una changamoto na ukiangalia jiografia ya Mto Ruvuma kwamba mto uko kwa chini na maeneo ya umwagiliaji yapo kwa juu. Ni lazima tuje na designing ya kujenga mabwawa mengi ili yatumike wakati wa umwagiliaji. Kwa hiyo, usanifu lazima ufanywe kutoka Songea kama nilivyosema hadi Wilaya ya Mtwara ili maeneo yote haya yafaidike na mradi huu. Tukitumia vizuri bonde hili tutaweza kunufaisha uzalishaji wa mazao ya mpunga lakini na mbogamboga na kuweza kuwasaidia wananchi wetu ambao sasa hivi wana utegemezi wa zao moja moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Songea wanategemea mahindi lakini Mtwara watu wengi wanategemea korosho. Lakini tukifanya upembuzi yakinifu na bonde hili likatumika ipasavyo basi tutawanufaisha watu wetu. Kuna maeneo ya Lipeleng’enye na kule Chikwedu kwa Mzee wangu Mkuchika, kuna changamoto ya mafuriko, lazima tujenge ukuta wa kutosha ili kuhakikisha sasa maji ya Mto Ruvuma hayawezi kuathiri mashamba ya hao wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye maazimio ya mkutano wetu wa wadau tulikubalina kwamba tuunde tume ya ufuatiliaji kwenye korosho nafikiri tutafanya kazi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naunga mkono hoja.