Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Kilimo. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akiifanya katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niwapongeze Wizara kupitia Waziri wa Kilimo na timu yake yote kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya kwa manufaa ya nchi yetu. Niwapongeze pia Wizara kwa ruzuku mbalimbali katika mazao ya kilimo ambayo wameendelea kuitoa. Lakini pia niwapongeze kwa kurudisha export levy katika msimu wa mwaka jana; export levy ambayo ni msaada sana kwa wakulima, hasa wa korosho ambako ndiko zao lenye export levy.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo nimeenda kuangalia miongoni mwa malengo ya Wizara ni pamoja na kupunguza umasikini kwa asilimia 50 kwa wakulima ifikapo 2030. Ni wazo zuri, ni mpango mzuri. Lakini napata shida kidogo; ni namna gani tutafikia kupunguza umaskini kwa wakulima hawa kwa trend ambayo tunaenda nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kurudisha export levy kwenye zao la korosho tulifarijika sana, na tunaendelea kushukuru; faraja yetu ilikuwa ni kwamba, kumbe sasa zile tozo mbalimbali ambazo zinapunguza kiasi cha fedha ambazo mkulima wa korosho anapoenda kuuza zao lake zinaenda kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tunashukuru kwamba tunapata pembejeo kwa ile asilima 50 ambayo inaenda kwenye tasnia ya korosho; lakini ile 50% ambayo inaenda kwenye mfuko mkuu wa Serikali tuombe sasa. Ili mkulima asibebeshwe mzigo mkubwa au apate bei ambayo italeta manufaa kwake na kupunguza umaskini, kama ambavyo tumetarajia kuupunguza, basi tunaomba zile tozo kwa mfano za CBT, TARI, task force zichukuliwe na Serikali ili mkulima anapoenda kuuza korosho yake basi aweze kupata angalau kitu kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mikorosho gharama ambazo mkulima anazitumia kuanzia kuandaa mashamba, palizi na shughuli zote mpaka aje kuvuna gharama zake ni kubwa mno. Gharama zile zinamfanya mkulima azidi kudidimia siku hadi siku. Kwa mfano kuna mwaka ambao korosho bei ilipanda kidogo kwenye soko, ikafikia kwa kilo shilingi 3,000 hadi 4,000. Ukienda yale maeneo ambayo yanalima korosho hali ilikuwa nzuri tulichangamka, watu walijenga nyumba bora na walikuwa wanapeleka watoto shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi imekuwa ni kinyume, wakulima wa korosho wamedidimia kwa sababu gharama za uzalishaji zimekuwa kubwa sana, hali ambayo inazidi kudidimiza. Ndiyo maana nachelea kwamba, je kweli tutaweza kupunguza hiyo asilima 50 ya umaskini kwa hali ambayo tunaiona sasa hivi? Lazima mkakati wa dhati uwepo wa kuhakikisha kwamba zao hili linaenda kumuinua mkulima. Bila mkakati wa dhati itakuwa ni hadithi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ili kuthaminisha korosho hizo sasa hivi akina mama wengi wanabangua korosho zao ili wauze zikiwa katika hali ya thamani kubwa zaidi, lakini wanakosa namna ya kupata masoko. Korosho wanazo, wanamuuzia nani wanashindwa. Niombe, Serikali itakapokuja kuhitimisha ituambie mkakati wa kuwasaidia wakulima ambao wanabangua korosho zao ukoje ili wapate masoko. Wanashindwa branding, korosho zinabakia ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona Serikali imetuambia kwamba, hadi kufikia Aprili 2023 imepeleka Marekani tani 74.19 zilizobanguliwa zenye thamani ya shilingi milioni 455.7, ni jambo zuri la kushukuru. Lakini sasa tuone ni namna gani Wizara itabeba, badala ya wabanguaji wakubwa peke yake tuwafikie wale wabanguaji wadogo ambao na wenyewe wanatamani siku moja korosho zao walizobangua wanaziuza na wana uhakika wa soko. Lakini pia wanauza hata huko nje. Wizara tukifanya hivyo tutakuwa tunawasaidia sana wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, tunashukuru kwamba Serikali ilitupatia pembejeo za ruzuku kwenye msimu uliopita na kule nyuma pia. Lakini msimu wa mwaka jana, baada ya kuona changamoto zilizojitokeza kwenye msimu wa mwaka 2020/2021 mwaka jana Wizara ilitoa mwongozo wa namna ya ugawaji wa pembejeo zile za ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwongozo ule ulileta shida kidogo katika utekelezaji wake. Nishauri Wizara, kwamba tunapoandaa miongozo hii tujaribu kushuka kulechini tukaone hali halisi. Mengi yanatendeka kwa kukaa mezani, hatujui uhalisia ulivyo kule chini kwa wazalishaji wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwongozo ule badala ya kumnufaisha mkulima halisi wa korosho ambaye tulimtegemea ulienda kuwanufaisha wale ambao walikuwa wananunua kangomba. Wananunua ndio wao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ashante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachania kwa maandishi naunga mkono hoja. Ahsante (Makofi)