Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii ili nami niweze kuchangia hii Wizara ya Kilimo katika makadirio yake ya mwaka 2023/2024. Niwapongeze sana Wizara kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea huu mradi wa upembuzi yakinifu katika Kijiji cha Mwakasumbi pamoja na Mwalukoli katika Jimbo la Kisesa, kazi nzuri sana lakini na namna bajeti inavyoongezwa ya kilimo ni jambo ambalo wakulima tunafurahia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba leo wafugaji ambao wamekwazwa na madhila yale ya wahifadhi wote leo wako hapa ambao Mheshimiwa Spika aliomba vielelezo hivyo viletwe wamekuja wenyewe na vielelezo. Kwa hiyo leo jioni tunakabidhi vielelezo hivyo vilivyoombwa na Mheshimiwa Spika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa bajeti. Katika utekelezaji wa bajeti hapa, bajeti ya maendeleo ya Wizara ya Kilimo katika mwaka huu wa fedha ni shilingi bilioni 569.97. Fedha zilizotolewa mpaka sasa hivi na Serikali ni shilingi bilioni 470.75. lakini katika fedha hizo, shilingi bilioni 361.5 ni za umwagiliaji ambazo mpaka sasa hivi zilizotolewa ni shilingi bilioni 85 tu sawa na asilimia 23. Sasa unaipataje asilimia 40, unaipataje shilingi bilioni 470 wakati fedha za umwagiliaji shilingi bilioni 361 ambazo ni sawa na asilimia 63 ya fedha za maendeleo zimetolewa asilimia 23 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba fedha kwa ajili ya kuendeleza miundombinu ya umwagiliaji mpaka sasa hivi imeshabadilishiwa matumizi. Zaidi ya shilingi bilioni 200 na kama imebadilishiwa matumizi, fedha za maendeleo, fedha zilizotengwa kwa ajili ya shughuli za umwagiliaji zimebadilishiwa maendeleo, zimepelekwa wapi? Kwa idhini ya nani? Waziri ana uwezo wa kubadilisha fedha za maendeleo zilizoidhinishwa na hili Bunge akazipeleka kwenye shughuli zingine. Tuambiwe kwa umakini juu ya hizi takwimu zilivyokaa na Waziri atakapokuja hapa ili tuweze kujua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni suala la utoaji wa mbolea ya ruzuku. Ukiangalia taarifa ilivyowasilishwa kwamba mpaka sasa hivi tayari mbolea tani 449,795 zimekwishatolewa na wanufaikaji 801,000 lakini ukienda kwenye ile jedwali alilosema jedwali la nane lina takwimu nyingine. Mbolea iliyopokelewa na kusambazwa mpaka sasa hivi ni tani 342,729 badala ya hiyo 400. Kwa hiyo kuna mkanganyiko mkubwa sana wa takwimu. Sasa hizi takwimu ni za kupika? Sasa kama zina uhalisia kwa nini zinatofautiana ukurasa hadi ukurasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, kama tuliandikisha wakulima 3,050,000, wakulima walioenda kunufaika na mbolea ni 801,000 peke yake, hawa wakulima wengine 2,200,000 walipata wapi mbolea? Kama tulijua kwamba mfumo huu wa utoaji wa mbolea ya ruzuku hatuwezi kuwafikia wakulima wote kwa pamoja, kwa nini tulileta mfumo ambao unapelekea mbolea kuipata mpaka upitie mfumo wa ruzuku ya mbolea? Hawa wananchi wengine wamelimaje kama hawakufikiwa? Kama tulikuwa na lengo la kusajili wakulima milioni saba na leo tumesajili milioni tatu, hawa wakulima wengine wanaendeshaje kilimo chao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto nyingi sana katika zoezi hili la utoaji wa mbolea ya ruzuku. Moja, mfumo wa mtandao wa mbolea za ruzuku uliokuwa ukitumika una changamoto nyingi. Moja, unaruhusu double scanning mpaka multiple scanning. Pili, mtambo huu hauwezi kuruhusu sub-agent. Mfumo unachelewa ku-left na hivyo mkulima anaweza aka-draw zaidi ya mara moja. Sasa kama una mfumo umeandaliwa wa namna hii, unaweza kwenda kufanya mpaka double scanning waharamia wengine wa kimtandao wanaweza kuiba fedha yoyote ile wanayoitaka kwenye huu mfumo, Wizara inaandaje mfumo na kuuleta kwa wananchi wenye changamoto za namna hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo ambao unaweza ukaiba fedha za nchi tukaenda kulipa mbolea hewa, unawezaje kuingia mfumo huo? Sitaki kuamini kwamba Serikali Mtandao kwa maana ya e-GA kwamba hawana uwezo wa kuwasimamia Wizara ya Kilimo, lakini nataka kuamini kwamba Wizara ya Kilimo walianzisha mfumo huu wa utoaji wa mbolea ya ruzuku bila kuwashirikisha e-GA na yawezekana kabisa hawana clearance ya e-GA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuendesha mfumo bila kupata clearance ya e-GA ni kosa kisheria na matatizo yake yanaenda kuzalisha matatizo makubwa ya uhujumu uchumi. Sasa Wizara inaweza namna gani kwanza huyu vendor alipatikanaje? Huyu vendor aliyetengeneza huu mfumo alipatikanaje? Alipitia zile procedure zinazotakiwa? Au alipatikana kwa kuteuliwa tu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili huu mfumo uliwezaje kuingia kwenye operation bila kupata clearance ya e-GA na tukawa na mfumo ambao una matatizo namna hii? Umepeleka matatizo makubwa kwa wakulima wetu. Wakulima wetu huko wanaambiwa mbolea ipo, tunaambiwa mbolea ipo lakini mbolea hawakupata wakulima wetu. Wakulima wameteseka kupata mbolea, wengine wamefia kwenye foleni. Mbolea zingine zimeibiwa, wameenda hawa mawakala 721 wamekuja kuambiwa kwamba tunawafutia leseni kwa sababu eti kwamba wamefanya double scanning. Sasa double scanning unawezaje kuifanya katika mfumo proper? Unawezaje kufanya double scanning kwenye mfumo proper halafu unamwambia nimekufutia leseni, halafu unamwambia jieleze kwa nini nisikufutie leseni wakati umeshamfutia tayari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria inakwambia toa notisi ndiyo umfukuze, huu mkanganyiko wa kuvunja sheria za nchi unaruhusiwaje kufanyika kwenye Taifa letu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bei elekezi. Wizara ilianza na bei elekezi ambayo haikufanyiwa uhakiki, hawakuhakiki bei elekezi inayotolewa kwa ununuzi wa mbolea na kusambaza mbolea, matokeo yake tumeenda kuwauzia wakulima kwa bei kubwa ambayo haina sababu yoyote kwa matamko tu ya wafanyabiashara. Wizara haikufanya uhakiki wa bei ya mbolea katika viwanda na katika masoko. TFRA haikufanya uhakiki huo matokeo yake leo mbolea eti ilipofika Machi baada ya kugundua kwamba sasa mahitaji ya mbolea yameisha nchini, yamepungua sana nchini, ilipofika Machi, TFRA inatoa bei elekezi ya shilingi 72,911 kwa mfuko wa urea wa kilo 50 kutoka shilingi 116,650 baada ya kuona mahitaji sasa hayapo. Wanashusha bei na price haiwezi ikashuka kama jiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, price volatility na price elasticity haiwezi kuruhusu mshuko wa namna hiyo, maana yake ni kwamba hapakuwa na usimamizi mzuri kwenye bei, matokeo yake pamoja na kutoa bei ya ruzuku, lakini ukweli ni kwamba tumeenda kutoa ruzuku kwenye bei fake. Sasa ukitoa ruzuku kwenye bei fake huwezi kupata value for money. Tumewachangia wananchi kulipia, tumetumia billions of money za fedha za Watanzania kwa bei ambazo hazina uhakiki, kwa bei ambazo hazina ukweli, matokeo yake tumepoteza fedha nyingi na hatuambiwi, bei mpaka sasa hivi wakandarasi wanatudai shilingi ngapi, mpaka sasa hivi tumetumia shilingi ngapi kwa ajili ya ruzuku ya mbolea na kwa nini tunafichwa vitabu vyoote havizungumzi gharama ya mbolea, mpaka sasa hivi ni shilingi ngapi Tanzania tumelipa? (Makofi)