Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, naipongeza Wizara kwa kuleta bajeti ambayo inamatumaini kwa Watanzania, lakini yapo maeneo ambayo nataka niishauri Serikali. Nianze kwenye eneo la miradi ya umwagiliaji. Ili nchi iweze kwenda mbele, ni lazima tuwekeze kwenye miradi ya umwagiliaji. Jimboni kwangu mimi ipo miradi ya umwagiliaji ambayo mpaka sasa bado haijakamilika. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri aangalie ule mradi wa umwagiliaji wa skimu ya Karema uweze kukamilika, kwani kila bajeti inayokuja huwa tunaambiwa kwamba inakwenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri aliangalie hili, ahadi zilizotolewa na Mawaziri ni nyingi kwenye mradi ule wa skimu ya Karema, sambamba na ile skimu nyingine ya Kabage ambayo ilianzishwa na Serikali. Kwa hiyo, tunaomba mkakamilishe ile miradi. Yapo maeneo mengine nchini kama tutawekeza kwenye miradi ya umwagiliaji, nchi itakuwa na usalama wa chakula, tutakuwa na uhakika wa uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo napenda kuchangia ni suala la mbolea ya ruzuku ya Serikali. Kwenye eneo hili, Serikali ilitoa fedha na tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuongeza fedha za ruzuku ambazo zimeenda kuwasaidia wananchi, lakini zipo kasoro kubwa sana ambazo zilijitokeza. Mwaka huu kuna baadhi ya wakulima ambao wamekula hasara kwa sababu mbolea zilizopelekwa zile ambazo tulikuwa tunakusudia kwamba zingeenda kuwafanyia kazi wananchi hazikuwa na ubora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali, mbolea zile ambazo zilikuwa na mashaka, tunaomba sana mziangalie, msije mkafanya makosa makubwa kama yaliyojitokeza, kupeleka mbolea mbazo hazina ubora uliokusudiwa. Hili ni jambo la kufanyiwa kazi na wataalam wafanye kazi ambayo inaweza kupambanua mbolea ambazo zinaweza zikawa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kilimo cha tumbaku. Nampongeza Mheshimiwa Waziri, kwanza kwa ushawishi wa kuleta makampuni ya ununuzi wa tumbaku. Amefanya jambo jema, wananchi wengi sasa wanaanza kupata manufaa makubwa. Hata hivyo, kuna kasoro ambayo tunamwomba Mheshimiwa Waziri akalifanyie kazi. Mbolea za ruzuku zililoletwa hazijawagusa wakulima wa zao la tumbaku. Hawa wanatumia mbolea za CAN, UREA, SA na hizo ni miongoni mwa mbolea ambazo zilitolewa ruzuku na Serikali, lakini hawajanufaika na kitu chochote. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi. Ahakikishe mbolea hizi zimewafikia, tena kwenye msimu huu huu ambao wamelima, ziwanufaishe na wao. Ni muhimu sana kwenye eneo hili mlifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili uweze kufanya maboresho makubwa kwenye zao la tumbaku, ni vyema Mheshimiwa Waziri mkaweka fedha ambazo zitakuwa zinafanya maboresho ya kuongeza idadi ya ma-classifier wanaoteua zao la tumbaku kupitia Bodi ya Tumbaku. Eneo hili linachelewesha masoko sana. Leo hii Mkoa wa Katavi una classifier watatu tu. Mahitaji ni zaidi ya classifier sita ambao wana kazi ya uteuzi wa tumbaku. Sasa nazungumzia mkoa mmoja tu, lakini hata ambao natoka, Mkoa wa Tabora, una uhitaji mkubwa, Mkoa wa Shinyanga una uhitaji mkubwa, Mkoa wa Ruvuma na pengine mikoa yote inayolima zao la tumbaku.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri aelekeze mawazo ya kuboresha Bodi ya Tumbaku kwa eneo ambalo wanateua wateuzi ambao ni wa Serikali. Hili tunaomba Mheshimiwa Waziri akalifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri tuweke mkakati wa mazao yale ya kibiashara. Mazao ya kibiashara ndiyo yanayoleta fedha za kigeni hapa nchini, lakini kwa ujumla bado Serikali haijawekeza kwa kiwango kikubwa sana. Mazao haya ni kama yako yatima, yanajiendesha yenyewe bila nguvu ya Serikali. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aje na mkakati wa kufanya maboresho ili mazao haya ya kimakakati yaweze kutoa tija kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante. (Makofi)