Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Halima Ali Mohammed

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kwa mara ya kwanza kabisa kusimama katika Bunge lako hili Tukufu. Namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na utukufu kwa kunijalia afya njema. Nakishukuru Chama changu, Chama cha Wananchi (CUF) kwa kuniamini, nami nitajitahidi kuwatendea haki wananchi wote kwa kuwawakilisha vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu afya. Suala la afya ni suala ambalo halina mjadala. Ni suala ambalo ni muhimu kwa maisha ya binadamu! Bila ya Afya, hakuna maendeleo. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, amezungumzia kuhusu idadi ya vituo vya huduma ya afya na vilevile akaelezea azma ya Serikali ya kuweza kuendeleza vituo vya afya katika ngazi ya kata, ngazi ya kijiji na ngazi ya halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli kuna manung’uniko makubwa sana katika huduma ya afya; kuna matatizo lukuki katika huduma za afya katika zahanati zetu. Sasa hivi zahanati zetu ni kama madarasa matupu pamoja na mizani ya kupimia watoto. Kuna changamoto chungu nzima! Zahanati zetu hazina nyumba za madaktari, hakuna vifaa tiba, hakuna dawa, hata wafanyakazi hawatoshelezi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapoboresha huduma za afya, basi umewasaidia wanawake na umewasaidia wananchi wote. Naishauri Serikali iboreshe miundombinu katika huduma za afya, lakini vilevile Serikali iongeze bajeti katika Wizara ya Afya na kuwe na ukaguzi wa zahanati zetu, vituo vya afya na hospitali zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, naomba nizungumzie kuhusu suala zima la fungu la UKIMWI. UKIMWI bado upo katika nchi yetu lakini vilevile ni tatizo na ni janga kubwa sana katika nchi yetu. UKIMWI unamaliza nguvukazi ya nchi yetu na ukitilia maanani zaidi wanaoathirika ni akina mama kwa sababu ndio wanaopata maambukizi kwa sababu ya maumbile yao na kama katika familia kuna wagonjwa, basi wanawake ndio wanaohusika katika kuhudumia wagonjwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa ruhusa yako nitoe takwimu za maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI kwa baadhi ya Mikoa iliyopo Tanzania Bara. Kwa mfano, Mkoa wa Njombe una asilimia 18.8, Mkoa wa Iringa una asilimia 9.1, Mkoa wa Mbeya una 9%, Mkoa wa Rukwa una asilimia 7.2 na Mkoa wa Shinyanga una asilimia 7.4. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonyesha kwamba ni asilimia 40 ya wananchi wetu bado hawana taarifa kuhusu ugonjwa wa UKIMWI. Ni jambo la kusikitisha sana katika bajeti yetu hii yote hakuna fungu ambalo limetengwa kwa ajili ya wagonjwa wa UKIMWI. Tunategemea wafadhili ambao hawana uhakika! Tunategemea wafadhili ambao wana interests zao! Kwa hiyo, naishauri Serikali itenge fungu la mapato ya ndani kwa ajili ya ugonjwa huu wa UKIMWI, ugonjwa ambao ni hatari na ni tishio katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka nizungumzie kuhusiana na suala la 10% ya mapato ya Halmashauri zetu kutengewa makundi haya mawili ya wanawake na vijana. Hili ni agizo na wala siyo hiari Halmashauri kama wakipenda watenge na wasipopenda wasitenge. Hili ni agizo, lazima litekelezwe lakini kwa bahati mbaya agizo hili halitekelezwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali itengeneze sheria ambayo itatia nguvu ili Halmashauri ambazo hazikutekeleza, basi ziweze kuwajibishwa. Vilevile nataka nisisitize kwamba katika fungu hili la 10% za wanawake, hizi ni pesa za walipa kodi wa nchi hii, kwa hiyo basi, ni budi fedha hizi zigawiwe bila itikadi za vyama. Wananchi wote ni sawa, kwa hiyo, wana haki sawa mbele ya sheria katika nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu miradi ya TASAF III. Mradi huu Serikali ilikuwa ina nia safi tu ya kusaidia kaya ambazo ni masikini, angalau basi na wao waweze kupata fedha kidogo ya kuweza kununulia angalau sare za shule za watoto wao pamoja na kudiriki kuwapeleka watoto hawa wachanga clinic. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu unatumika kinyume na utaratibu. Kuna baadhi ya viongozi wanatumia fedha hizi kwa ajili ya kuboresha au kujijenga kisiasa. Hili ni kosa mbele ya sheria, lakini vilevile kuna tatizo kule kwetu upande wa Zanzibar. Upande wa Zanzibar Masheha wanatumika vibaya katika mifuko hii ya TASAF; wamepewa uwezo wa kuingiza majina wanayoyataka na yale wasiyoyataka wanayafuta. Wanakiuka, maana yake Masheha kule kwetu wana uwezo zaidi kuliko CMC ambao ndio wahusika wa huu mfuko. Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, naomba hilo ulichukulie kwa uzito wake uweze kulifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nilikuwa napendekeza kwamba posho ile ya shilingi 10,000/= ambayo wanalipwa wale vijana ambao wanasimamia ugawaji wa hizi fedha ambao ni CMC, haitoshelezi. Kwa hiyo, waangaliwe kwa jicho la huruma ili waweze kuongezewa kidogo, kwa sababu dhamana waliyonayo ni kubwa ya kusimamia fedha zile kuanzia Benki mpaka kuzigawa na wanapokosea mahesabu, basi wanafunguliwa kesi. Kwahiyo, ni vyema basi na wao wakaangaliwa kwa jicho la huruma ili wasiweze kufanya yale mambo ya kufanya wizi katika mfuko huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ahsante sana.