Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nitoe mchango wangu kwenye bajeti hii muhimu sana. Nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema ambaye anatujalia uzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nitumie nafasi hii kumpongeza kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania kwa namna alivyotoa jicho la uhakika kwenye sekta ya kilimo. Kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri na watendaji wote wa Serikalini wakiongozwa na katibu Mkuu. Kiukweli Mheshimiwa Bashe, sisi vijana tunajifunza kwako na kwenu, na tuna imani kubwa na ninyi, na tunaridhika na kazi nzuri mnayoifanya. Kwa sababu hiyo nitakuwa na mambo madogo tu mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni la umwagiliaji. Kipekee sisi wananchi wa Korogwe tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri. Tumeimba muda mrefu habari ya Bonde la Mkomazi. Tumekuwa na hadithi nyingi, wewe ni shahidi tangu ukiwa Naibu Waziri na mwenzako Mheshimiwa Mgumba, lakini mwaka jana 2022 uliniahidi ukasema, mdogo wangu tunatenga fedha, tunarudia upembuzi yakinifu na usanifu, na mwaka unaofuata tutakwenda kwenye ujenzi. Hakika mkataba umesainiwa na nimeona kwenye bajeti ukurasa wa 25 umenihakikishia kwamba kwenye bajeti hii ujenzi wa skimu hiyo unakwenda kuanza kwenye mwaka wa fedha unaokuja. Nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninawashukuru Mawaziri hawa kwa usikivu wao. Nimekaa nao kawenye vikao akaniambia nimwandikie, nikamwandikia. Kwenye bajeti, nimeyaona mabonde yale ya Magoma. Ukarabati wa skimu ile ya Chekerei, skimu ya Magila na eneo lile la Mayuni kule Mapangoni nimeona, nawashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili la umwagiliaji sina cha kuchangia, zaidi nawashukuru sana. Tunaomba tu kazi hizi ziende kwa speed ili tuweze kuwanufaisha wakulima wetu na wananchi wa Korogwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni eneo la kilimo cha zao la mkonge. Sisi watu wa Mkoa wa Tanga ndio tunaongoza kwa uzalishaji wa Mkonge kwenye nchi hii. Unaposema Mkoa wa Tanga unaongoza kwenye uzalishaji, anayeongoza ni Wilaya ya Korogwe hasa Korogwe Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa namna walivyorudisha matumaini ya wananchi wa Korogwe na Mkoa wa Tanga na Tanzania kwa ujumla kwenye zao la mkonge. Tulijengewa dhana kwamba mkonge ni zao la wakulima wakubwa wenye fedha nyingi, wenye maeneo makubwa ya kulima, lakini imani mliyoijenga kwa wananchi wa Mkoa wa Tanga, imani mliyoijenga kwa wananchi wa Korogwe na wakulima wa mkonge, imewarudisha watu wa Tanga na watu wa Korogwe kwenye kilimo cha mkonge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mwaka 2020 nchi yetu tumezalisha Mkonge tani 37,022, lakini katika hizo wakulima wadogo walizalisha tani 26,000. Mwaka 2021 tumealisha tani 39,484, wakulima wadogo wamezalisha tani 24,000. Mwaka 2022 uliopita, tumezalisha tani 48,351, wakulima wadogo wamezalisha tani 22,000. Kwa miaka hii mitatu iliyopita, jumla kama nchi tumezalisha tani 124,858.39, na katika hizo wakulima wadogo mchango wao ni tani 73,420 sawa na asilimia 58.8. Kwa takwimu hizi huwezi kubeza mchango wa wakulima wadogo kwenye uzalishaji wa zao la mkono. Kwenye hotuba yako umesema na kwa mujibu wa takwimu za Bodi ya Mkonge wakulima wenye mkonge mdogo ambao haujapita miaka miwili wakulima wadogo sasa hivi wenye mkonge mdogo hawajaanza kuvuna, wana hekta 3,545. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema nini? Uzalishaji huu moyo huo wa wakulima wadogo ili uende vizuri naomba tuzingatie mambo mawili. Jambo la kwanza; mkonge kama mkonge majani hayani maana, maana ya mkonge ni nyuzi baada ya kusindika. Wakulima wadogo wanachangamoto kubwa sana ya mashine za kusindika mkonge kule Korogwe na AMCOS zile tano kuna mashine za kuchakata mkonge za Sasalana nilisema mwaka jana tunashukuru wamejirekebisha wanakwenda vizuri. Lakini wakulima wana uhitaji wa mashine ukiangalia uzalishaji huu, ukiangalia idadi ya eneo la mashamba mapya waliyokuwa nayo wakulima wetu na kazi wanayoifanya sasa baada ya miaka miwili kutakuwa na crisis kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana Mheshimiwa Waziri, alihaidi kwenye Bunge hili kwamba wanakwenda kununua mashine mbili kubwa za kuchakata mkonge wa wakulima kila tukiulizia tunaambiwa manunuzi bado ningetamani baadae ukija utuambie kwenye eneo hili Mheshimiwa Waziri mmefikia wapi? Lakini Mheshimiwa Waziri, wakulima wadogo kupitia AMCOS zao walitaka kuchukua mikopo kwenye taasisi za kifedha lakini mpaka leo taratibu zimekuwa ngumu wanakwama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana tumesema hapa Mheshimiwa Waziri kwani hii Benki ya Kilimo ni kwa ajili ya kina nani? Kwanini Benki ya Kilimo iisiingie kusaidia AMCOS zetu hizi? Benki ya kilimo isibaki na wakulima wakubwa tu tuwasaidie AMCOS, tutumie benki ambazo ziko tayari, tuwe na madirisha. AMCOS zikopeshwe wakulima wapate mashine ili waende wakasindike mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine bodi imegawa mashamba na nimesoma vizuri kwenye hotuba yako mmesema mmeishagawa hekta zaidi ya 3,829. Ombi langu na watu wa Korogwe tunaomba kwenye kugawa mashamba pamoja ya kwamba ardhi hii ni ya nchi nzima wapeni kipaumbele watu wa Korogwe kwenye yale maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ni kwenye mkonge. Mwaka jana tumesafirisha nje tani 32,627 sawa na asilimia 67.5 lakini kwa miaka mitatu iliyopita nyuzi za mkonge zinakwenda nje ni zaidi ya asilimia 71 ya uzalishaji wa mkonge wote. Kupeleka nyuzi za mkonge nje ni kuuza ajira za watu wetu, kupeleka nyuzi za mkonge zote hizi asilimia 71 nje ni kupunguza kodi tunapata kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali Mheshimiwa Waziri tunao watalamu wa uchumi, tunao watu wanafanya economic intelligence hivi tunashindwa kwenye kujifunza tunakopeleka mkonge? Wanazalisha nini? kwa ajili ya soko lipi? Tukafanya mikakati ya kuwavutia wawekezaji kuja kufunga mashine na viwanda Tanzania vya kuchakata mkonge, tusafirishe matunda ya mwisho siyo kusafirisha nyuzi. Tukisafirisha nyuzi tunapoteza ajira za watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimwia Waziri, mwaka jana kwenye hotuba ukurasa wa 165 na 166 ulisema vizuri sana kuhusu kuielekeza Bodi ya Mkonge kuongeza nguvu ya kuvutia matumizi ya magunia na nyuzi za mkonge naku– discourage bidhaa zile nyingine zinazoharibu soko la mkonge. Bahati mbaya mwaka huu kwenye hotuba yako sikuiona na bahati mbaya sana kwenye nchi yetu kuna viwanda nane vinavyoshulika na mazao ya mkonge kwa maana ya nyuzi za mkonge. Lakini leo tunapozungumza viwanda hivi nane vinavyofanya kazi vizuri ni viwanda vitatu tu kati ya viwanda vile nane na idadi ya uzalishaji wake ninayo hapa. Mheshimiwa Waziri siyo jambo zuri viwanda vinaendelea kufa, vinaendelea kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulijifunza kwenye COVID, ikitokea tuna majanga tujifunze kwenye vita ya Urusi, ikitokea kuna majanga masoko ya nje hayafanyi vizuri hatma yetu ni nini? Hatma ya wakulima wetu ni nini? Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili moja ya jambo linalo–discourage uzalishaji wa vifaa vya mkonge kwenye nchi yetu ni sheria tulizokuwanazo na usimamizi wa sheria tuliyonayo. Sheria ya Forodha ya Afrika Mashariki ina ruhusu msamaha wa kodi kwa nyuzi za plastiki…

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: …ni vizuri watu wa uvivi inawasaidia lakini tukazikague ili zitumike kwa matumizi yaliyokusudiwa na zisiende zaidi ya hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)