Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi ya pekee kukushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya Waziri wa Kilimo. Awali ya yote nimpongeze kwa kazi kubwa na nzuri ambayo yeye mwenyewe Mheshimiwa Bashe na Naibu wake Mheshimiwa Mavunde wanaifanya, hongereni sana.

Mheshimiwa Spika, Baada ya kutoa pongezi, kwa kuwa muda ni mfupi naomba niende moja kwa moja kutoa mchango wangu kwenye hotuba yako hasa kwenye mazao ya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeipitia hotuba ya Waziri wa Kilimo. Nimeenda kwenye jedwali kwenye mazao ya biashara. Yapo mazao saba yanayotuingizia fedha nyingi za kigeni nayo ni tumbaku, kahawa, chai, korosho, pamba, pareto na mkonge.

Katika mazao haya saba kwa msimu huu wa kilimo wa 2022/2023 zao ambalo limeingiza fedha nyingi za kigeni ni zao la kahawa, limetuingizia fedha USD 204,670,147 likifuatiwa na tumbaku ambayo imetuingizia USD 154,084,169 likifuatiwa na pamba ambayo imetuingizia USD 147,135,803 na zao ambalo ni la mwisho na limetuingizia kiwango kidogo ni pareto ambalo limetuingizia USD milioni 5,484,927. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo nchi ambazo uchumi wake umekua kutokana na mchango wa kahawa. Brazil ndio nchi ulimwenguni ambayo kabisa ni mkulima na mzalishaji mkubwa na imetajirika kwa sababu ya zao la kahawa. Katika Afrika tunazo nchi, ipo Uganda imetutangulia mbele, lakini ipo Ethiopia. Ukienda kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2020 – 2025 inasema hivi; “Ifikapo mwaka 2025 zao hili la kahawa kwa mwaka tuwe tuna uwezo wa kuzalisha tani 161,000,” lakini mpaka sasa hivi ndiyo tumefikia tani 80,000 na ndizo hizi zimetuletea hizi fedha za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe ushauri mkubwa kabisa kwa kulinganisha na majirani zetu. Ukiangalia tukijilinganisha na Nchi jirani ya Uganda ambayo sisi katika nchi yetu kahawa inalimwa katika mikoa 16 ukitafuta arable land, ardhi inayofaa kwa zao hili ni zaidi ya mara tatu ya ardhi ambayo inalimwa kahawa Uganda, lakini wao wenyewe kwa mwaka huu, kwa msimu huu wameingiza USD milioni 800, kiwango hicho ni kikubwa tukijilinganisha.

Mheshimiwa Spika, zipo jitihada ambazo bado kama nchi tunatakiwa tufanyie kazi. Ni zao pekee hili la kahawa ambalo linaweza likawa na mchango mkubwa kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Bado kuna nafasi kubwa ya juhudi ambazo zinatakiwa zifanyike, nchi inatakiwa iwekeze, pamoja na kwamba, imekwishaandikwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ukiangalia kwenye uzalishaji kwa miaka hii miwili, mitatu, tukianzia na msimu ule wa 2019 na 20 tulizalisha tani 73,000, mwaka uliofuatia tani 70,000, msimu uliofuatia 66,000 tulishuka, lakini sasa tumepanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inatakiwa ichukue hatua madhubuti kwanza ili tuweze kuwa na malengo makubwa. Tuwe na malengo makubwa ya kuhakikisha kiwango cha uzalishaji wa kahawa ambayo ndio zao namba moja ambalo limetuingizia fedha za kigeni ni lazima Serikali iwekeze. Sehemu za kuwekeza kwanza ni lazima uwe na uwezo wa kuzalisha mbegu bora katika mikoa yote ambayo inalima kahawa kwa kuitumia TACRI. Uganda kwa mwaka huu wenyewe wanaenda kuzalisha miche bora milioni 171, Ethiopia wanaenda kuzalisha miche bora ya kahawa milioni 362, sisi milioni 20, kiwango hicho ni kidogo, hakiwezi kuleta mapinduzi ya kilimo cha kahawa na kikachangia kwenye uchumi wetu. Kwa hiyo, zinahitajika jitihada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima tuwe na malengo makubwa tutoke kwenye milioni 20 twende hata kwenye milioni 200 halafu tuigawe hiyo miche, tupanue mashamba, tuwawezeshe wananchi ambao tayari wanajishughulisha na kilimo hiki cha kahawa, tuwawezeshe vijana kufungua mashamba mapya na tuwape mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine ya pili, naomba nichangie tena kwenye zao la chikichi. Kwanza nampongeza Waziri na sisi watu wa Kigoma tunamshukuru sana kwa sababu, kwenye bajeti hii tumeona chikichi kwa mara ya kwanza imeenda kupata ruzuku, inaenda kuwa mkombozi. Itaenda kuokoa bilioni 470 ambazo Serikali inatumia kwa ajili ya kununua mafuta ya kupikia na kuyaleta humu nchini. Yafuatayo yanatakiwa yafanyike ili kuhakikisha uzalishaji wa chikichi unaongezeka.

Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa Kandege ambavyo amekwishazungumza ukitoka Kigoma, Katavi mpaka Rukwa ule ukanda wote ni wa hali ya hewa ambao unaweza ukakuza zao la chikichi, ule mpango wa Waziri sasa wa BBT wa zile block farms ndio wakati wake sasa. Serikali ije kuyafungua mashamba hayo, iwatayarishe vijana na iwape mashamba hayo wayasimamie, itachukua muda mfupi tu tutaweza kujitegemea kwa mafuta na tutakuwa tumeokoa fedha hizi za kigeni ambazo tunazitumia katika kuingiza mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zao la tatu ni tangawizi, nalo linalimwa katika Jimbo langu la Buhigwe. Tunavyo vijiji zaidi ya kumi ambavyo sasa hivi vinashughulika na kilimo cha tangawizi. Tangawizi ni mojawapo ya viungo muhimu sana, kwa hiyo, tunaomba katika bajeti hii Waziri ajitahidi na aoneshe namna gani Serikali inaweza kuboresha miundombinu ili kuongeza kipato cha wakulima wa tangawizi na hasa kwa kuwaletea viwanda vya kuchakata zao la tangawizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)