Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Aleksia Asia Kamguna

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi. Awali ya yote, hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupatia uhai. Nampongeza Mheshimiwa Samia kwa kazi anazozifanya yeye na wasaidizi wake pamoja na Mawaziri na Watanzania wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, nimesimama kwa ajili ya kuchangia kwenye hii bajeti ya kilimo kama inavyojieleza yenyewe, katika ukurasa wa 11 aya ya 26, amesema kwamba, upande wa mazao mwaka 2020 mazao yalipatikana kwa asilimia tano, mwaka 2021 ilikuwa asilimia 3.6 na mwaka 2020 tena katika upande wa kipato ilikuwa ni asilimia 15.4 na mwaka 2021 ilikuwa ni asilimia 14.6.

Mheshimiwa Spika, katika Tanzania idadi yetu ni milioni 61.74, lakini walio wengi ni wakulima ambao ni asilimia 65. Wakulima hawa ukiwaangalia sana kwa haraka haraka ni watu ambao kidogo ni wenye shida nyingi na changamoto nyingi. Wao wamesema kwamba katika ukurasa huo, aya ya 26, wanasema kilimo kilipungua na mapato pia lilipungua kwa sababu ya Uviko-19 pamoja na vita vya Ukraine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naenda mbali zaidi, siyo vita tu na Uviko-19, mmeacha kitu kikubwa tu; migogoro ya wakulima na wafugaji. Migogoro ya wakulima na wafugaji pamoja na tembo, hao ndio wamefanya wakulima warudi nyuma. Kwa sababu Uviko vijijini walikuwa hawavioni, wakulima wadogo wadogo walikuwa wakiendelea na kazi, lakini wakilima kule vijijini watu wa mifugo wanaingia wanakula; tembo wanaingia wanashambulia yale mazao; lakini wanaposhambulia, tembo ana mtetezi wake ambaye ni Wizara ya Maliasili na Utalii, anakwambia wewe mazao yako yameliwa kwa sababu umelima kwenye shoroba. Mtu wa mifugo, Wizara yake inamtetea pia, inasema kwamba, mtu wa mifugo kazi yake, amewaandalia chakula, kutengeneza manyasi, ambayo ameyapanda. Sasa yale manyasi hayatakua ndani ya miezi mitatu au miezi sita. Sidhani kama mtu ana ng’ombe 100 atalisha kwenye robo heka, itamuchukua muda. Je, huyu mkulima katika kipindi hiki atakuwa Halimi, ataishije? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkulima anaonekana kama hana mtetezi, ni mkiwa. Kama tembo anatetewa na maliasili, kama mfugaji anatetewa na Wizara ya Mifugo: Je, huyu mkulima anatetewa na nani? Katika hotuba yake sijaona sehemu yoyote ameainisha kwamba mkulima tumsaidie katika hatua hii na hii, katika hali hii. Jamani, hicho kilimo kitaendaje? Umetenga hela nyingi sana kwa ajili ya skimu za wakulima, lakini zile skimu zitaenda kufanya kazi gani kama mtu analima, halafu mazao yake yanaliwa na tembo, mazao yake yanaliwa ni mifugo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza Wizara ya Kilimo kama inavyosema, imwangalie mkulima, mnamteteaje mkulima huyu ambaye ni yatima? Hatuwezi tukapanga bei wakati kile kilichovunwa hakipo. Sasa tunaomba Wizara ya Kilimo imtetee mkulima ambaye ni yatima. Kwa mfano, hususan Mkoa wa Morogoro, mnajua kabisa ule ni Mkoa wa kimkakati, kama Wizara ya Kilimo mngesimama, tungeweza kulisha Tanzania nzima, lakini kwa kuwa tumebaki yatima, Morogoro itakuwa ni masikini kuliko ilivyokuwa hapo awali, kwa sababu haina mtetezi.

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara hii iangalie, kama wao wameweka nyasi, hao watu wa mifugo, na maliasili wanasema tunalima kwenye shoruba: Je, ninyi mnatuteteaje wakulima? Naomba mnapomalizia hapa unijibu kwamba, ninyi mmejipangaje katika kumtetea huyu mkulima ambaye ni yatima? Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili nazungumzia kuhusiana na usalama wa chakula. Katika Tanzania, zamani kulikuwa na National Milling, watu wanachukua vyakula wanaweka dawa kwenye magunia na kwenye mifuko, lakini walikuwa wanakoboa National Milling, kumbe vile vyakula vina dawa ndani yake. Sasa hivi unakuta kila kona vimezagaa viwanda vya kukoboa mahindi: Je, usalama wa huyo Mtanzania uko wapi? Kwa mfano, kule Dar es Salaam Manzese, unakuta unaenda, kuna viwanda, lakini kuna maji kwenye kikopo. Sasa yale maji yatasafisha yale mahindi jamani? Matokeo yake unakuta kwamba, watu tunakula sumu na wanapata magonjwa mengi kama ya kansa kwa sababu hatudhibiti hivyo vyakula. Tunaomba Wizara ya Kilimo msimamie, ili tuweze kupunguza haya magonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna kilimo hiki cha mbogamboga, tunapulizia dawa. Hizi dawa katika kupulizia, hamjawaelimisha wale wakulima wadogo wadogo. Wakipulizia dawa baada ya siku mbili mtu anaziuza zile mboga; akishaziuza, walaji wanakula, hatujui mle ndani kuna nini? Matokeo yake magonjwa tena yanaongezeka. Kwa hiyo, naomba Wizara ya Kilimo mliangalie hilo, kwamba wakulima ni watoto yatima.

Mheshimiwa Spika, mkitaka tuendelee, kwanza mkae ninyi Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mifugo ili mjue kwamba mtatatuaje tatizo la wakulima na wafugaji kwa Tanzania nzima hususan Mkoa wa Morogoro? Pia mkae muone kwamba mtatatuaje hilo tatizo la sumu ambazo nafikiri Watanzania wengi tunakula sumu, baada ya kuwa tunakula sumu, tunatumia hela nyingi sana katika kujitibia, basi mtafute namna ya kusimamia hiyo miradi yetu ambayo tunawawezesha wakulima wadogo wadogo, tusiwaache, lakini tuwasimamie hatimaye nao waweze kujikwamua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hayo, machache, naunga mkono hoja. Nashukuru. (Makofi)