Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa maoni yangu na mchango wangu kwenye bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. Niungane na Wabunge wenzangu wote waliotangulia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada kubwa anazozifanya na kuuona umuhimu sana wa Wizara hii ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wengi humu ambao tunatokea maeneo ya majimbo ambayo yana wananchi wengi wakulima tusipozungumzia sekta hii ya kilimo tutakuwa tumewasaliti wakulima.

Mheshimiwa Spika, niungane na Wabunge wengine waliompongeza sana Mheshimiwa Bashe na Naibu wake Mheshimiwa Anthony Mavunde, Kaka yangu na wasaidizi wao wote kule Wizara. Kwa kweli wanajitahidi wanafanya kazi vizuri na wana maono nazuri. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikisoma malengo ya Wizara, Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake ameandika ni kuongeza tija na uzalishaji katika Sekta ya Kilimo. Ili kuongeza tija, maana yake nini? Maana yake tunaangalia mkulima sasa kwa ekari, akipanda ekari moja atapata mavuno kiasi gani. Hili jambo ni muhimu sana tukaliangalie ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata matokeo ya kile ambacho wanakifanya.

Mheshimiwa Spika, tutafikiaje hapo sasa? Ili tuweze kufikia kwenye tija ni muhimu sana kuboresha huduma za ugani kule kwenye vijiji. Sasa hapa maana yake tunaenda pamoja na kuangalia idadi ya watumishi walioko pale. Kule Ludewa nashukuru sana Wizara hii tumeongezewa watumishi, tulikuwa na watumishi 41, tumeongezewa Maafisa Umwagiliaji watatu na maafisa wengine watatu. Kati ya hao graduates ni tisa. Kwa hiyo niishukuru sana Serikali kwa kutuongezea watumishi kwenye Sekta ya Kilimo watumishi sita na kwenye Sekta ya Mifugo watumishi 10.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sasa hivi maana yake tija tunayoitaka anayozungumza Mheshimiwa Waziri itakuwa ni rahisi kuweza kuipata. Maana yake wale watumishi sasa wataenda kuwaelimisha wakulima. Sasa ili wapate tija lazima tunaangalia hata muda ambao wanapanda, je wakulima hawa wanapanda kwa wakati? Kwa hiyo tunatarajia watumishi hawa ambao wameletwa waweze kwenda kuhakikisha kwamba wakulima wetu wanapanda kwa wakati, lakini vile vile wanatumia mbegu bora.

Mheshimiwa Spika, sasa hapa kwenye eneo la mbegu, ningependa sana kuishauri Serikali, mbegu bado kwa mkulima wa kijijini, bado ni ghali sana. Kwa hiyo Serikali ingefaa iweze kuwekeza fedha kwa kushirikiana na vyuo vikuu vya kilimo na taasisi mbalimbali za utafiti, ili waweze kuandaa mbegu ambazo mkulima atazipata kwa gharama nafuu kuliko hali ilivyo hivi sasa. Kwa sababu wakati tunakua tuliona wazazi wetu, mbegu kama alipanda mwaka jana, mwaka huu anachagua anarudia tena. Hii ilikuwa inawapunguzia gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi zile mbegu za asili tumezipoteza. Kuna Mbunge mmoja alisisitiza hapa kwamba kuna umuhimu wa kuja kuhangaika pia kuhakikisha kwamba hizi mbegu tunaweza tukaziandaa na kuzihifadhi. Kwa hiyo, eneo la mbegu bado ni ghali, kwa hiyo Serikali iwekeze, ishirikiane na vyuo vikuu vya kilimo na taasisi za utafiti kuhakikisha kwamba mbegu inashuka bei na ikiwezekana tuweke ruzuku pia kwenye mbegu na yale madawa ya kuua wadudu na yenyewe tuweke ruzuku ili yapatikane kwa bei nafuu sana.

Mheshimiwa Spika, niishukuru sana Serikali kwa kuweka ruzuku kwenye mbolea. Kule Ludewa tulipata shida kidogo kutokana na changamoto ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezieleza, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake. Kuna mtaalam mmoja anaitwa Mablanketi, nafikiri aliniunganisha Naibu Waziri mpaka tuligombana, lakini baadaye alifanya kazi nzuri tukaweza kupata lori zaidi ya 15 zenye mifugo 600 kila moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kutokana na ruzuku ile ya mbolea leo lazima niwe muungwana niweze kuishukuru sana Serikali. Nami niombe tu zile changamoto za kukosekana kwa maghala, mawakala kule wilaya za pembezoni yaweze kutatuliwa mapema.

Mheshimiwa Spika, vile vile nipongeze sana Serikali kwa kuifufua ile TFC na kuipa fedha iweze kuagiza mbolea. Nimesoma kwamba awamu ijayo mbolea itakuja mapema na hii kwa kweli sisi kule Mkoa wa Njombe alizungumza ndugu yangu Mwanyika. Tunalima mara kwa mara viazi vinalimwa misimu miwili au mitatu, lakini kuna kilimo cha bustani vitunguu, nyanya, mboga mboga. Kwa hiyo muda wowote mbolea zinahitajika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitaomba hawa watu wa TFC waweze kuleta mbolea mapema iweze kupatikana muda wote. Vile vile kuna wazee ambao hawana uwezo wa kumudu kununua mbolea ya mfuko 70,000. Wao wakipata hela kidogo wanakwenda ananunua kwenye kilo. Naomba pia hilo liweze kuzingatiwa kwa sababu hali za wananchi wetu hazifanani, tusiwalazimishe wote kununua mbolea kilo 50 na kuendelea.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu sana, Ludewa tumepata mahindi mengi, tumelima hekta 51,000, tunaomba masoko yaweze kuandaliwa kwa sababu tutakuwa na mavuno mengi. Tani laki tano hazitoshi, naomba Serikali ionge fedha.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo machache, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)