Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Hussein Bashe, Naibu Waziri Mheshimiwa Anthony Mavunde, Katibu Mkuu Ndugu Gerald Mweli, Naibu Katibu Mkuu Dkt. Hussein Mohamed, wataalam wa Wizara, wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizara pamoja na wadau wa maendeleo kwa mchango mkubwa sana kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utahusu fursa za kilimo cha umwagiliaji katika jimbo la Moshi Vijijini, hali ya Vyama vya Ushirika na Kiwanda cha Kukoboa Mpunga kilichopo Kijiji cha Chekereni, Kata ya Mabogini jimbo la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Spika, mkoa wa Kilimanjaro una fursa kubwa sana za kilimo cha umwagiliaji. Hii ni kutokana na ukweli kwamba Kilimanjaro kuna mito mingi inayoanzia mlimani na kuishia bahari ya Hindi bila kutumika kikamilifu kwenye kilimo.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali ijenge skimu mpya na kukarabati zile skimu za asili ili haya maji yatumike kuzalisha mazao badala ya kuishia baharini.

Mheshimiwa Spika, katika jimbo langu la Moshi Vijijini ninaishauri Serikali ifanye yafuatayo; kwanza Serikali iwekeze kikamilifu kwenye kuboresha na kujenga upya skimu za asili. Kule Kilimanjaro kulikuwa na mradi wa Rehabilitation of Traditional Irrigation Schemes. Tangu mradi huu ufungwe, miundombinu ya skimu hizi imekuwa kwenye hali mbaya. Kwa ujumla miundombinu hii imechoka na maji hayawafikii tena wakulima wa kahawa, ndizi, mbogamboga na matunda kama maparachichi. Skimu hizi za asili zikiboreshwa (Kata za Kibosho, Kirima, Kibosho Kati, Kibosho Mashariki, Kibosho Magharibi, Kindi, Okaoni, Uru Shimbwe, Uru Mashariki, Uru Kaskazini, Uru Kusini, Kimochi, Oldmoshi Mashariki, Old Moshi Magharibi na Mbokomu) zitasaidia sana kuongeza tija kwa wakulima wangu wa Jimbo la Moshi Vijijini.

Pili, Serikali ijenge skimu mpya za umwagiliaji katika maeneo ya tambarare ambayo hukumbwa na mafuriko makubwa kila mwaka. Maji ya mafuriko yaelekezwe shambani kuzalisha chakula (mpunga na mazao mengine). Maeneo ya kuzingatia ni: -

a) Wizara ijenge skimu mpya Kata ya Arusha Chini katika Mto Ronga itakayohusisha vijiji vya Mikocheni na Chemchem ambako kuna takribani 2000 ha.

b) Wizara ijenge skimu mpya ya ziada Kata ya Mabogini ambapo kuna 1350 ha.

Mheshimiwa Spika, skimu hizi mpya zikijengwa, zitaongeza 3350 ha kwenye kilimo cha umwagiliaji na kuongeza uzalishaji wa chakula na kuchangia kikamilifu katika uchumi wa wananchi na Taifa.

Mheshimiwa Spika, mchango mwingine ni kuhusu mashamba ya ushirika na vyama vya SACCOS zilizopo kwenye maeneo mbalimbali ya Jimbo la Moshi Vijijini. Uongozi wa mashamba na baadhi ya SACCOS ni changamoto kubwa sana. Viongozi wengi wa ushirika hawana taaluma za kuongoza ushirika.

Mheshimiwa Spika, katika baadhi ya vyama jimboni kwangu kuna matumizi mabaya ya madaraka na rasilimali za mashamba mengi ya ushirika. Katika mikutano yangu ya hadhara, wakulima wametoa malalamiko kuwa wanaibiwa na viongozi wa ushirika.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa fedha za kutosha zimetengwa kwenye idara ya ushirika, ninaishauri Serikali ifanye ukaguzi maalum katika mashamba na SACCOS zote na watakaobainika wamefuja mali za ushirika, wachukuliwe hatua za kisheria na vyombo husika. Hii ni pamoja na kurekebisha sheria na sera za ushirika Tanzania ili tuwabane wabadhirifu wa mali za ushirika.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa mwisho ni kuhusu Kiwanda cha Kukoboa Mpunga cha Kilimanjaro Paddy Hulling Co. Ltd.

Mheshimiwa Spika, kiwanda hiki kimesimamisha shughuli zake na kabla ya kufungwa, kiwanda hiki kilikuwa moja ya kiwanda kilichokuwa kimepata mafanikio makubwa sana. Kiwanda hiki kipo Chekereni – Moshi katika Kata ya Mabogini.

Mheshimiwa Spika, kiwanda hiki kiko kwenye eneo ambalo huzalisha mpunga mara mbili hadi tatu kwa mwaka. Kiwanda hiki hakifanyi kazi tangu Septemba, 2014. Kiwanda cha Kukoboa Mpunga kilikodishwa na Chama Kikuu cha Ushirika cha Kahawa (KNCU) na baada ya kushindwa kukiendesha, mkoa ulimshauri Msajili wa Hazina kukirudisha Serikalini ili atafutwe mwekezaji mwingine anayeweza kukiendesha. Tayari Msajili wa Hazina amerejesha kiwanda hiki Serikali tangu tarehe 18 Oktoba, 2018 lakini bado hajapatikana mwekezaji, na shughuli zimelala. Kutokuwepo kwa kiwanda hiki kumeondoa fursa ya wakulima kupata bei nzuri ya mpunga na ajira kiwandani kwa wana Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Spika, kiwanda hiki kinaweza kuwa ni chanzo cha kuongeza thamani na kusafirisha mchele wetu nje na kuwapatia wakulima kipato na taifa kwa ujumla. Naiomba Wizara isaidie kumpata mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.