Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuendelea kuipanua na kuendeleza sekta hii ya kilimo ambayo ina mchango mkubwa wa pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri pia pamoja na timu yake yote kwa uthubutu waliouonesha pamoja na kuendeleza maono haya mazuri ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, Watanzania milioni 61 wote wanakula chakula kila siku, na kati ya hawa zaidi ya milioni 40 wanajihusisha na shughuli za kilimo kwenye maisha yao ya kila siku. Hivyo basi tunaona kabisa sekta hii ilivyo na mchango mkubwa kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala moja la mazao ya bustani (horticulture) ambayo inajumlisha mbogamboga, matunda, maua na viungo.

Mheshimiwa Spika, mazao haya ya bustani yanachangia sana kwenye kuingizia nchi yetu fedha za kigeni kwa kiasi kikubwa, lakini bado Wizara hayajayapa mkazo wa kutosha. Ukiangalia ukurasa wa 104 ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri utaona mwenendo wa uzalishaji wa mazao ya bustani kutoka mwaka 2018 hadi 2022. Ukiacha mazao mengine, zao la maua limekua limetelekezwa muda mrefu kama halina mwenyewe licha ya kwamba maua ni zao ambalo lina soko la uhakika duniani na lina mchango mkubwa kuingiza fedha za kigeni.

Mheshimiwa Spika, mwenendo huu wa maua hauridhishi na hivyo naiomba sana Wizara iweze kutueleza wakati wanahitimisha mikakati iliyonayo kwenye kuendeleza zao la maua hapa nchini na hususan kwa mkoa wangu wa Arusha.

Mheshimiwa Spika, leo hii kwenye nchi jirani ya Kenya zao hili la maua linachangia zaidi ya dola milioni 900, ajira 100,000 na inagusa maisha ya zaidi ya watu 2,000,000. Lakini pia ukiachia zao la chai, maua ni ya pili kwenye kuchangia pato la Taifa katika nchi ya Kenya. Hivyo basi tunaona jinsi majirani zetu wanavyo ipa kipaumbele hii sekta.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Arusha ni miongoni mwa mikoa iliyokuwa inastawisha sana mazao haya ya bustani na ilikuwa inachangia pato la Taifa na fedha za kigeni kwa kiasi kikubwa, lakini tokea mashamba yalioyokuwepo ya mbogamboa, maua na matunda kufilisika na kutaifishwa mazao haya yameshindwa kuingizia taifa letu fedha hizi.Namuomba pia mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha atuambie mikakati ya kufufua mashamba haya kwa ajili ya mustakabali mpana wa Mkoa wa Arusha na nchi yetu kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.