Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, utangulizi; nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa nafasi hii uliyonipa nami niweze kuchangia hotuba hii muhimu ya Makadirio ya Mapato na Matumzi ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Awali ya yote naomba nipongeze hatua zinazochukuliwa na Serikali kuendelea kuongeza bajeti ya kilimo na suala la kilimo cha umwagiliaji kupewa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, nipongeze kwa uamuzi wa Serikali wa kujenga Bwawa na Skimu za Umwagiliaji katika Kijiji cha Mwakasumbi na Mwaukoli katika Jimbo la Kisesa. Suala hili nimekuwa nikilipigia kelele humu Bungeni kwa muda mrefu sana na ninaomba maeneo mengine yaliyobaki ya Mwandu Itinje, Mwasengela, Sakasaka, Tidabuligi na Mwabusalu nako maeneo hayo wananchi wanazisubiri kwa hamu kubwa skimu na mabwawa kwa kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kushindwa kukusanya maduhuli ya Serikali ambapo imeweza kukusanya kiasi cha shilingi milioni 679.57 sawa na asilimia 0.5 ya lengo la shilingi bilioni 126.1 zilizokadiriwa mwaka 2022/2023 hata mwaka wa fedha 2021/2022 mchezo ulikuwa ule ule Tume ilishindwa kukusanya mapato. Kitendo cha Wizara kutochukua hatua stahiki kwa uongozi wa Tume hii maana yake imebariki uzembe na ubadhirifu unaoendelea, hali hii inanipa mashaka makubwa juu ya uwezo wa Tume kusimamia majukumu na miradi mikubwa ya umwagiliaji ambayo tunaitengea mabilioni ya fedha kila mwaka. Hatua stahiki zichukuliwe ikiwemo kuwajibika kwa uongozi na Menejimenti ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa bajeti ya maendeleo; hapa kuna mkanganyiko mkubwa, fedha za maendeleo zilizoidhinishwa katika mwaka wa fedha 2022/2023 ni shilingi bilioni 569.97; hadi kufikia Aprili, 2023 fedha zilizokuwa zimetolewa ni shilingi bilioni 470.75 sawa na asilimia 82.6 ya bajeti nzima ya maendeleo. Fedha hizo zimetolewa na zimetumika kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji na uhifadhi, kuimarisha utafiti na uzalishaji wa mbegu bora, kuanzisha mashamba makubwa ya pamoja na kugharamia ruzuku ya mbolea.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya maendeleo ya shilingi bilioni 569.97 fedha kwa ajili ya kuimarisha kilimo cha umwagiliaji ni shilingi bilioni 361.5 sawa na asilimia 63.4 ya bajeti nzima ya maendeleo. Kiasi kilichokuwa kimelipwa hadi Aprili, 2023 kwa ajili ya miundombinu ya umwagiliaji ni shilingi bilioni 85.15 sawa na asilimia 23.5 tu ya bajeti ya umwagiliaji. Fedha zilizopokelewa na kutumika zilifikiaje kiasi cha shilingi bilioni 470.75 wakati fedha zilizotolewa kwa ajili ya miundombinu ya umwagiliaji ni shilingi bilioni 85.15 tu kati ya shilingi bilioni 361.5?

Mheshimiwa Spika, hata tafsiri yake ni kwamba fedha kwa ajili ya miradi ya umwagiliaji imeshabadilishiwa matumizi na hapa kwa hesabu zangu ni takribani shilingi bilioni 200 hazijulikani zilipo na matumizi yake hayafahamiki. Waziri hana mamlaka kisheria kubadilisha matumizi ya vifungu na bajeti iliyoidhinishwa na Bunge. Waziri atueleze fedha ziko wapi na zimebadilishiwa matumizi kwa ridhaa ya nani?

Mheshimiwa Spika, kuhusu Tume ya Taifa ya Ushirika; Serikali iliahidi kwa muda mrefu kuanzisha Benki ya Maendeleo ya Ushirika lakini utekelezaji wake umekuwa wa kusuasua, mwaka jana Waziri wa Kilimo aliahidi hapa Bungeni kuwa benki hii ingekuwa imeanza katika mwaka huu wa fedha unaomalizika. Taarifa iliyowasilishwa inaonesha mtaji umefikia shilingi bilioni 5.2 tu kati ya mtaji wa shilingi bilioni 15 unaohitajika ili kukidhi vigezo vya kuanzisha benki kama vilivyowekwa na BOT na hatujaelezwa benki hiyo itaanzishwa lini.

Mheshimiwa Spika, aidha, ukaguzi uliofanywa na COASCO katika Vyama vya Ushirika 6,005 matokeo ya ukaguzi huo yameonesha kuwa hati safi ni 5.65% huku hati zenye mashaka, mbaya na kushindwa kutoa maoni zikiwa 94.35% na mwaka jana hali ilikuwa vilevile na kwa maana hiyo hakuna mabadiliko yoyote yaliyofanyika na hii ni ishara ya kuota mizizi kwa ubadhirifu wa mali za umma na udhaifu wa mifumo ya udhibiti ya ndani hata Tume ya Maendeleo ya Ushirika ilipofanya ukaguzi ilibaini vyama vingi vya ushirika vinakabiliwa na madeni makubwa.

Mheshimiwa Spika, nimshauri mwaka jana na leo namshauri tena, Waziri aachane na mpango wa kuanzisha Benki ya Maendeleo ya Ushirika na badala yake aimarishe mifumo ya usimamizi ya vyama hivi na kuondoa mianya ya upotevu wa fedha za wanachama na fedha za umma na kadhalika. Pia ili kuwezesha kupata mikopo kwa wingi na kwa urahisi lianzishwe dirisha la Vyama vya Ushirika katika Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB).

Mheshimiwa Spika, kuhusu utoaji wa mbolea ya ruzuku; huu utaratibu wa utoaji wa mbolea za ruzuku ulianzishwa na Serikali katika msimu wa kilimo wa 2022/2023 kwa lengo la kuongeza upatikanaji na kuwapunguzia gharama wakulima baada ya mtikisiko wa kiuchumi uliosababishwa na Covid-19 na vita ya Ukraine na Urusi. Utaratibu huu ulitarajiwa kuondoa kasoro na dosari zilizokuwepo lakini badala yake hali imekuwa mbaya zaidi, mbolea kuadimika na kusababisha wakulima kukosa mbolea, wakulima kuuziwa mbolea fake ambayo imeenda kuua mazao na kuharibu afya ya udongo, mbolea kuchelewa kufika kwa wakulima, utoroshaji wa mbolea nje ya nchi, kuuziwa michanga badala ya mbolea, wananchi kusafiri umbali mrefu kufuata mbolea, kupoteza muda na wengine kupoteza maisha wakiwa kwenye foleni wakihangaika kutafuta mbolea.

Mheshimiwa Spika, utoaji wa mbolea ya ruzuku umekuwa na changamoto nyingi kama ifuatavyo: -

(i) Takwimu zilizotolewa na Waziri zina mkanganyiko mkubwa ambapo anasema hadi kufikia Aprili, 2023 mbolea za ruzuku zilizokuwa zimepokelewa na kusambazwa kwa wakulima ni tani 449,795 na wakulima walionufaika ni 801,776 lakini kiambatisho Na. 8 kinaonesha kuwa mbolea ya ruzuku iliyosambazwa ni tani 342,729 na wakulima walionufaika ni 782,553. Nini chanzo cha mkanganyiko huo wa takwimu au hizi takwimu ni za kupika? Waziri afafanue.

(ii) Wakulima waliosajiliwa ni 3,050,621 lakini wakulima walionufaika na mbolea ya ruzuku ni 801,776, nini kilichosababisha wakulima zaidi ya milioni 2.2 waliosajiliwa na kuahidiwa kupewa mbolea ya ruzuku wakose mbolea wakati nchini tuna ziada ya mbolea ya ruzuku tani 369,647?

(iii) Serikali ilifahamu kuwa haitawafikia na kuwasajili wakulima wote kwa mara moja, kwa nini ilianzisha mfumo wa utoaji wa mbolea ambao unalazimisha kupata lazima upitie mfumo wa mbolea ya ruzuku?

(iv) Mfumo wa kimtandao wa mbolea za ruzuku, hapa najiuliza kwa nini Wizara ya Kilimo ilianza kutumia mfumo huu ukiwa na changamoto nyingi kiasi hiki, na siamini kuwa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) inaweza kutoa kibali (clearance) kuruhusu mfumo huu kutumika nchini. Mfano mfumo huu unaruhusu: -

(a) Mfumo hauna usalama wala ukomo (Security and Limit). Imewezekana kufanyika mikwaruzo ya kivunge cha mwitikio wa haraka (QR code scanning) zaidi ya mara moja (double scanning) or multiple scanning) kwa mauzo ya mfuko mmoja wa mbolea ambayo ingeweza kufanywa na waagizaji, mawakala, muundaji wa mfumo au haramia yeyote wa mfumo na kupelekea mauzo hewa ya mbolea kwa wakulima na madai hewa ya fedha kwa Serikali. Hapa ushahidi upo TFRA ilifutia leseni za mawakala 721 kwa makosa ya double scanning tarehe 17 Aprili, 2023.

(b) Mfumo huu hauwezi kung’amua kama mbolea imetumika kwenye shamba husika (traceability). Hivyo mtu anaweza kuja kuchukua tu mbolea kwa namba ya mkulima halafu akaenda kuiuza nchi jirani kwa magendo ambao wanampa bei kubwa zaidi kuliko bei ya ruzuku. Hali hii imepelekea utoroshaji mkubwa wa mbolea nje ya nchi. Kesi za utoroshaji wa mbolea nje ya nchi zimekuwa zikiripotiwa mara kwa mara. Hata Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alipofanya ziara Nyanda za Juu Kusini alikuta kesi za utoroshaji wa mbolea za ruzuku zimefurika kwenye Mahakama za Mikoa iliyo mipakani kama Songwe.

(c) Mfumo ulianzishwa bila kuzingatia kwamba huko mashambani mitandao ya simu inasumbua na inabidi wakulima wasafiri umbali mrefu kuitafuta mbolea sehemu zenye mitandao ya simu hali ambayo imekuwa ikiwaingiza hasara kubwa wakulima ya pesa za nauli, kulala guest house na gharama ya chakula.

(d) Mzabuni wa aliyeunda mfumo hatujaelezwa uwezo wake namna alivyopatikana, au alipatikana kwa kupewa mkataba bila kushindanishwa na wengine kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi ya Umma (Public Procurement Act).

(e) Mfumo huu unachelewa ku-left na hivyo unamwezesha mkulima ku-draw zaidi ya kiwango alichonacho mfano anaweza kuchukua mbolea zaidi ya kituo kimoja na hivyo kupelekea hasara kwa mawakala.

(f) QR Codes zinaingiliana na kampuni nyingine mfano QR Codes za Kampuni X na Kampuni Y zinaingiliana na hivyo kusababisha mawakala kushindwa kutofautisha na hivyo kusababisha hasara na kudaiwa upande mwingine.

(g) Mfumo na matumizi ya Agrodealer Too/ hauruhusu kufanya Branch au Sub–Agent na hivyo kulazimisha wakulima kuja mjini sehemu moja kufuata mbolea na hautambui gharama nje ya eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kitendo cha Wizara ya Kilimo kuanzisha na kutumia mfumo bila kupata kibali (clearance) cha Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), ni kwenda kinyume cha sheria ya Serikali Mtandao (Electronic Government Act of 2019) na wahusika wanapaswa wawe wanatumikia kifungo hadi sasa. Mfumo huu umeleta hasara kubwa kwa wakulima, mawakala na Serikali ikiwemo. Madai hewa ya fedha za ruzuku za mbolea, mazao kudumaa na kukosa mavuno na madeni makubwa ya mawakala na waagizaji wa mbolea makampuni, kutumia fedha zaidi ya kiasi kilichoidhinishwa na Bunge cha shilingi bilioni 150. Nani atafidia hasara hii, huu ni uhujumu uchumi, ni lazima tupate maelezo ya kutosha ili Bunge lichukue nafasi yake.

(v) Kufuta leseni za mawakala wa usambazi wa mbolea 721, Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea (TFRA) iliwafutia leseni mawakala 721 wa usambazaji wa mbolea ya ruzuku kupitia matangazo ya magazeti ya Mwananchi na The Guardian ya tarehe 17 Aprili, 2023 ambapo pia maamuzi hayo yalipata kibali cha Waziri wa Kilimo alipoongea na waandishi wa habari nje ya Ukumbi wa Bunge Dodoma kupitia Kituo cha Televisheni cha Azam (UTV). Tarehe 19 Aprili, 2023 TFRA iliwaandikia barua mawakala hao wajieleze kwa nini wasifutiwe leseni ya biashara ya mbolea kwa kosa la kuvunja sheria kwa kufanya udanganyifu wa ku-scan QR Codes zaidi ya mara moja (multiple scanning). Jambo hili linaleta mkanganyiko mkubwa sana.

(a) Serikali kwa nini iandae mfumo unaoruhusu kufanya udanganyifu yaani double scanning or multiple scanning?

(b) Kwa nini TFRA iwafutie leseni mawakala 721 na kuwatangaza nchi nzima kuwa sio waadilifu halafu iwaandikie barua ya kuwataka wajieleze; kwa nini wasifutiwe leseni huku ikiwa tayari imeshawahukumu?

(c) Kwa nini TFRA imekiuka Sheria ya Mbolea ya mwaka 2009 ambayo inataka kutoa notisi ya siku 30 na kupata maelezo ya mawakala hao kabla ya kuwaondoa? Hapa kuna nia ovu iliyokusudiwa na Wizara dhidi ya hawa mawakala.

(d) TFRA ilijuaje kama double scanning imefanywa na mawakala wakati mfumo ulioandaliwa hauna usalama (security) kiasi kwamba multiple scanning inaweza kufanywa na waagizaji, muundaji wa mfumo au haramia mwingine yeyote wa mifumo ya mitandao.

(e) TFRA hakufahamu changamoto hizo, multiple scanning anasubiri imebaki miezi miwili kuisha msimu wa kilimo ndio anaanza kuchukua hatua?

Mheshimiwa Spika, nani atawafuta machozi mawakala 721 ambao wamevunjiwa heshima kwenye umma na mitaji yao kuwekwa rehani? Uvunjifu wa sheria ukiruhusiwa uendelee namna hii utaleta matatizo makubwa kwenye Taifa, watu wote waliohusika kufanya dhuluma hii wawajibishwe na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

(vi) Kutokufanyika uhakiki wa bei kabla ya kuanza kutoa mbolea ya ruzuku, Wizara ya Kilimo iliandaa mfumo wa kuanza kutoa mbolea za ruzuku bila kufanya uhakiki wa bei katika viwanda vinavyozalisha mbolea na matokeo yake pamoja na kushuka sana kwa bei za mbolea katika soko la dunia bado wakulima wanaumizwa kwa bei kubwa huku Serikali ikidaiwa pesa nyingi na makampuni yanayoingiza mbolea nchini ambazo zingeepukika kama ufuatiliaji wa bei za mbolea viwandani ungeendelea kufanyika mara kwa mara kama ilivyokuwa wakati wa BPS. Mfano, TFRA ilitangaza bei elekezi ya mbolea ya Urea kwa mfuko wa kilo 50 mwezi Agosti, 2022 kwa wastani wa shilingi 124,734, mwezi Novemba, 2022 wastani wa shilingi 116,687 na mwezi Machi, 2023 wastani shilingi 72,911. Mbolea katika soko la dunia ilikuwa inashuka bei kila mwezi kwa nini TFRA haikutangaza bei elekezi?

Kwa nini bei imeporomoka ghafla baada ya msimu wa kilimo kukaribia kufika mwisho na mahitaji ya mbolea kupungua? Lakini pia bei haina tabia ya kushuka ghafla inashuka kwa slope ni price elasticity or price volatility.

Mheshimiwa Spika, bei elekezi iliyotolewa na TFRA ilitokana na matamko ya wafanyabiashara na hakuna uhakiki wa kiuchunguzi (due diligence) uliofanywa na Serikali kupitia TFRA kama sheria inavyoelekeza. Pamoja na bei ya soko la dunia kuendelea kushuka, lakini ziliendelea kutumika bei zilezile za juu mpaka msimu wa matumizi makubwa ya mbolea ulipomalizika Machi, 2023 ndipo TFRA ikatangza bei ndogo zaidi (wastani wa shilingi 76,421 na hivyo kufanya wastani wa ruzuku ambayo Serikali ilitakiwa kuwalipa mawakala kuwa shilingi 6,421 kwa mfuko wa kilo 50). Hiki kitendo cha kuacha kufuatilia bei za soko la dunia kama sheria inavyoelekeza kumeifanya Serikali kulipa na kudaiwa na makampuni madai na malipo hewa.

(vii) Kiasi cha fedha kilicholipwa hadi sasa kugharamia mbolea ya ruzuku hakijatajwa mahali popote na Waziri wala madai ya waagizaji wa mbolea, kwa nini Waziri anatumia nguvu kubwa sana kuficha taarifa hizo.

Mheshimiwa Spika, ushauri; CAG afanye ukaguzi maalum kuhusu utekelezaji wa utoaji wa mbolea ya ruzuku kwa haraka kabla ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2023/2024 ili kubaini mapungufu yaliyopo na Bunge kuchukua nafasi yake.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.