Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyetuwezesha kufika siku ya leo na kwa baraka zake tele tuko hapa siku ya leo. Pia kipekee kabisa nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa miongozo yao na maelekezo yao katika kutekeleza majukumu ndani ya Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kipekee kabisa naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri Hussein Mohamed Bashe, Waziri wa Kilimo pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Kilimo kwa ushirikiano mkubwa ambao wamekuwa wakinipatia katika kutekeleza majukumu katika Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa mbele ya Bunge hili naomba niseme namshukuru sana Mheshimiwa Waziri amekuwa kaka, amekuwa rafiki, amekuwa kiongozi, lakini amekuwa Mwalimu mzuri. Nimejifunza kilimo kupitia yeye na mimi kila siku asubuhi nikiamka saa 12 lazima nisikilize kwenye YouTube jambo lolote la Hussein Bashe kwenye kilimo imenifanya nimekielewa vizuri kilimo hivi sasa. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na hoja ya kwanza, hoja ya BBT kwamba ni kwa nini hatujaenda Mikoa yote? Tulitoa utaratibu mzuri kabisa ambapo tuliandika barua kwa Mamlaka za Mikoa za kuwataka kutenga maeneo maalum kwa ajili ya program hii kubwa ya vijana na wakina mama. Ipo mikoa ambayo ilifanya kwa uharaka na iliandaa maeneo na ikawa rahisi katika sehemu ya kwanza ya utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kutoa rai kwa Mikoa mingine yote ambayo maeneo yapo kwa ajili ya kilimo kwenda kutekeleza program hii ya BBT, Wizara tuko tayari kuja kuyaangalia maeneo hayo, tutatuma wataalam wetu na tuko tayari kuanzisha program hizi katika maeneo hayo. Lengo letu kubwa ni kuhakikisha tumeifikia nchi nzima kutokana na ikolojia ya kila eneo na hiyo ndiyo maksudi mazima ya program hii.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Shinyanga kwa mfano, ukiangalia hapa katika vitabu vyetu haimo lakini Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga namshukuru sana pamoja na Mheshimiwa Mbunge Katambi hapo walishirikiana kwa pamoja na Wabunge wa Mkoa wa Shinyanga, tulizungumza na Mwekezaji pale Jambo ambaye yeye anazalisha juice na ana mahitaji makubwa sana ya maembe, Mkoa wa Shinyanga wanaweza kulima maembe. Ninavyozungumza hivi sasa wameshaandaa eneo na tumeshamuelekeza mtaalam wetu kwenda kupima afya ya udongo, tutakwenda kufanya BBT katika Mkoa wa Shinyanga na off taker tayari yuko pale ni Jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Geita wameonesha utayari. Mkoa wa Geita kwenye kilimo cha mananasi na wenyewe wako tayari kwa ushirikiano wa Mkuu wa Mkoa na kwenyewe pia kule tutakwenda, bahati nzuri mananasi ya Geita Jambo ameshayapima na ana uwezo wa kuyatumia kutengeneza juice, kwa hiyo soko la uhakika lipo na pale tutakwenda kuweka mradi mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesikiliza hoja za Waheshimiwa Wabunge, wamechangia vizuri sana na kutoa ushauri mzuri sana, liko jambo nataka niliweke vizuri ili lieleweke vizuri. Hapa kuna hoja mbili, kuna hoja ya program ya BBT na kuna hoja ya mashamba makubwa ya pamoja (block farms) haya ni mambo mawili tofauti. Ni sawasawa na kwamba kila Wakili ni Mwanasheria lakini siyo kila Mwanasheria ni Wakili. Maana yake ni hivi katika haya mashamba. Mashamba makubwa ya pamoja siyo lazima yote kuwemo kuna BBT. BBT ni program ya uwezeshaji wa vijana na wakina mama ambao siyo lazima iwekwe katika mashamba makubwa yote ya Pamoja, lakini BBT ni mkusanyiko wa eneo kubwa kwa hiyo ni shamba moja au mashamba ya pamoja lakini siyo lazima ya kwamba kila kwenye block farm kuna BBT, na hapa ndiyo dhana ile ambayo nataka niiseme kwamba watu wanafikiri tumewasahau wakulima wengine na tumewalenga vijana peke yao na wakulima wengine tumewaacha kabisa, hapana.

Mheshimiwa Spika, katika mashamba haya makubwa watakwenda kulima wakina mama, wakina baba, wenye umri ambao siyo umri wa vijana na vijana pia watakuwemo. Kwa hiyo, hoja ya kwamba tumewaacha kabisa hapana. Kwa hiyo nataka niliweke sawa sawa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni suala la umwagiliaji. Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi imetuelekeza kwamba ikifika mwaka 2025 tuwe tuna eneo linalomwagiliwa la hekta milioni 1.2, Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Wabunge mwaka jana mkatoa hoja na ushauri kwamba nchi yetu imejaliwa mabonde, maeneo mazuri, kwa nini hatuongezi eneo la umwagiliaji?

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita ni Serikali sikivu, Mheshimiwa Rais alisikia hoja ya Wabunge juu ya maeneo makubwa ya kimkakati ya kufanya kilimo cha umwagiliaji na Tarehe 20 mwezi Machi, 2023 mbele ya Mheshimiwa Rais, tumesaini mikataba ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina katika mabonde 22 ya kimkakati ambayo tafsiri yake ni nini? Tafsiri yake ni kwamba tunakwenda kuimwagilia nchi nzima. Mabonde haya ya kimkakati inaanzia katika Bonde la Ziwa Victoria, zaidi ya hekta 20,000. Tunakwenda Bonde la Bugwema, Bonde la Suguti, tunakwenda Bonde la Mto Manonga Wembele, tunakwenda Bonde la Ruhuhu, Bonde la Tumbandiosi, Bonde la Makondeko, Bonde la Lukuledi, Bonde la Mto Songwe, Ifakara Idete, Kilombero, Mkomazi, Rufiji Basin, inakwenda mpaka Kasinde, Ngomai. Mabonde haya yote yanakwenda kutengeneza hekta 306,631 za umwagiliaji, ni nchi nzima tunakwenda kuigusa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hiyo tuliona kutokana na mabadiliko ya tabianchi lazima tuhakikishe tunafanya kilimo cha umwagiliaji. Kilimo cha umwagiliaji maana yake nini? Lazima uwe una skimu zinazokusaidia kufanya kilimo mwaka mzima zaidi ya mara moja. Ili uweze kufanya hivyo lazima uwe na chanzo cha uhakika cha maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha huu 2022/2023 ambao unaishia, tumekwenda na Wakandarasi wako site tunachimba mabwawa 14 ya awali ambayo yatatupa mita za ujazo ya maji 131,535,000 ambazo ukizibadilisha ni sawa na maji lita bilioni 131. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyafanya hayo, kwenye bajeti hii ya mwaka huu ambayo Wabunge mtaipitisha hapa, tunakwenda kuchimba mabwawa mapya 100 ambayo yatakuwa yana mita za ujazo milioni 906 sawa na lita za maji bilioni 900. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuishii hapo, tunakwenda kuchimba visima 150 katika Halmashauri 184. Wako wakulima ambao kwao wanahitaji visima tu kuweza kuongeza uzalishaji, tutafanya Wizara ya Kilimo. Tumejifunza kwa Wabunge wametuambia hapa ya kwamba yako baadhi ya maeneo hatuhitaji visima, hatuhitaji mifereji mikubwa. Tutapeleka pia na pampu katika maeneo ambayo ni karibu na vyanzo vya maji ili wakulima wetu waweze kumwagilia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ilizungumzwa hoja hapa kwanini hatuweki nguvu nyingi kwenye mazao ambayo yatatuletea pia fedha za kigeni? Sasa nafikiri tu kuna baadhi ya Waheshimiwa hasa aliyeongea hoja hii Mheshimiwa Halima Mdee nafikiri hakuangalia vizuri humu ndani. Nitampa mfano wa mazao mawili tu, mchele na parachichi ambayo aliisema yeye. Kwenye mpunga, maeneo ambayo tunayategemea sana ni Mkoa wa Mbeya, Wilaya ya Mbarali. Pale Wilaya ya Mbarali tumefanya uwekezaji mkubwa wa miradi ya umwagiliaji. Mheshimiwa Mtega yuko hapa ni shahidi.

Mheshimiwa Spika, pale tuna mradi wa Bonokuva Gigolo, tuna mradi wa Herman Chosi, tuna mradi wa Ipolo Isenyela, tuna mradi wa Matebete, ambayo ni miradi ya fedha nyingi na hii yote itakwenda kusaidia upatikanaji wa mpunga wa uhakika kwa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili kwenye parachichi ambayo aliisema. Kwenye parachichi tunafanyaje? Tumetafuta masoko ya uhakika ya parachichi. Tarehe 25 Novemba, 2021, Mamlaka ya Afya ya Mimea ya India walituruhusu kuingiza parachichi. Tunapeleka parachichi India, tutapeleka parachichi Hispania, tutapeleka parachichi China, Marekani tunamalizia hoja ya phytosanitary ili tupeleke kule nako parachichi. Serikali inafanyaje katika kuliandaa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zao hili linahitaji pia requirement ya kimataifa, mojawapo ni usafi wa mazao. Ukienda Arusha, Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu tumepata ithibati ya kimataifa ya usafi wa mazao ambayo itasaidia kupeleka mazao yetu nje ya nchi, pale pia tumefunga mtambo mkubwa tunauita micro plasma atomic emission spectroscopy ambao unasaidia kupima usafi wa mazao na zamani mkulima wa Tanzania alikuwa analipa zaidi ya dola 10,000 kwa ajili ya kipimo hicho leo analipa dola 300 kwa ajili ya kupata hati ya usafi wa mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo nataka niseme hapa haraka haraka ni kwenye mkonge. Wabunge mmesema hapa kuhusu mkonge, Wabunge wa Mkoa wa Tanga mmesema vizuri sana, tumesikia hoja zenu. Hoja kubwa ya mkonge ambayo inapelekea mkonge wetu kupata changamoto kubwa ni mkonge mwingi unaoza kwa sababu ya kukosa makorona. Wabunge wa Mkoa wa Tanga mwaka huu mtayaona makorona katika Mkoa wenu wa Tanga kuanza kuchakata mkonge. Tumeshaagiza na procurement process inaendelea, korona zile zitakuja na Wabunge wetu wa Mkoa wa Tanga mtatembea kifuambele, wakulima wenu watapata sehemu ya kwenda kuchakata mkonge wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunataka mkulima wa mkonge wa Tanga aache kuuza UG, aache kuuza SSUG, aache kuuza UF. Tunataka mkulima wa mkonge wa Tanga auze SL na 3S. Hii ndiyo mkonge wa daraja la juu kabisa ambao utampatia fedha nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)