Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, naungana na Watanzania wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali za ustawi wa kijamii, amani, upendo, mshikamano wakati wote tangu kuanzishwa kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, naungana na wananchi wote wa jimbo langu la Mbulu Mjini kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, viongozi na watendaji wote Serikalini kwa jinsi walivyotatua changamoto mbalimbali na utekelezaji wa Ilani ya CCM 2022-2025, tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu awajalie mafanikio na baraka.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika kwa jinsi unavyoliongoza Bunge letu toka ulivyopokea majukumu yako, nawe Mwenyezi Mungu akujalie baraka na mafanikio pamoja na wananchi wa jimbo la Mbeya Mjini.

Mheshimiwa Spika, kwa moyo wa dhati nampongeza Mheshimiwa Jumaa Aweso – Waziri wetu; Mheshimiwa Maryprisca Mahundi - Naibu Waziri; Katibu Mkuu Engineer Nadhifa Kemikimba; Naibu Katibu Mkuu na watendaji wetu wote wa Wizara kwa ngazi zote. Kwa kweli jitihada zinaonekana japo kuna changamoto.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu; kwanza, Serikali iongeze jitihada za kutafuta fedha za kujenga miundombinu ya visima vyote vilivyotayari kuchimbwa katika maeneo mbalimbali kwani tayari tumemaliza uchimbaji wa visima saba katika jimbo langu la Mbulu Mjini yapata mwaka sasa, lakini hatujaweza kujenga matanki na kuweka mtandao wa mabomba kwenye vijiji, hali hii inawafanya wananchi kusubiri huduma ya maji kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, Serikali itazame upya suala la mchakato wa uteuzi wa bodi mpya ya maji kwenye mamlaka za maji za RUWASA Wilaya na Miji kwani maeneo mengi bodi humaliza muda wake, lakini ngazi hizo hazichukui hatua za mchakato wa uteuzi wa bodi mpya haraka.

Mheshimiwa Spika, Serikali iwe na ratiba ya ukaguzi wa tathimini ya kiufanisi wa utendaji, mapato na matumizi pamoja kuangalia mwongozo wa uendeshaji wa mamlaka za maji kama unakidhi haja na kutoa fursa ya maoni kama upande wa wapokea huduma wanaridhika.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie suala la upotevu wa maji kwenye mitandao ya mabomba kwa kulinganisha uzalishaji wa maji kutoka vyanzo mpaka ankara za malipo kwa watumiaji, kwenye suala la madeni mpango wa kuunganisha mfumo wa kulipa bill ya maji kwa kununua kwanza ili kufanikisha upunguzaji wa madeni.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa maeneo mengi ya mji yanapokea wimbi kubwa la wananchi wengi wanahamia, Serikali iangalie upatikanaji wa vyanzo vikubwa vya maji badala ya kuchimba visima vingi kwenye eneo moja ilhali upatikanaji wa maji hauendani na wingi wa watu.

Mheshimiwa Spika, Serikali ijitahidi kutoa fedha zote zinazoombwa kwenye bajeti ya Wizara hii kwani kuna maeneo mengi miradi mingi imekwama kwa ajili ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, Serikali itafute fedha za ujenzi wa majengo ya Ofisi za Mamlaka ya Maji RUWASA kwa ngazi ya Wilaya na mijini ili kupunguza gharama za uendeshaji isiyolingana na mapato halisi ya mamlaka mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.