Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi. Awali ya yote nishukuru na kuipongeza sana Serikali kwa jitihada kubwa sana ya kuleta fedha za maendeleo ambazo zimekuja kwenye eneo la Wilaya ya Tanganyika. Naishukuru sana Serikali kupitia Mheshimiwa Rais kwa kuleta fedha nyingi za maendeleo. Tumejengewa Hospitali ya Wilaya ya Tanganyika, tunavyo vituo vya afya visivyopungua saba, na vipo vingine viwili vinajengwa. Hayo ni mafanikio makubwa sana kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika. Tunaipongeza Serikali, na tunawapongeza Mheshimiwa Waziri, na Naibu Waziri. Wote walishafika kwenye maeneo ya Wilaya hiyo ya Tanganyika na kwenye hospitali ya wilaya na baadhi ya vituo vya afya. Tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie sana uhaba wa watumishi. Hospitali ya Wilaya ya Tanganyika ni miongoni mwa Wilaya ambayo imejengewa hospitali nzuri ya kisasa, lakini kwa bahati mbaya hospitali hii haina watumishi kabisa. Ina watumishi wachache na huduma ambazo zinatolewa kwa sasa ni kama vile hadhi ya zahanati. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba Mheshimiwa Waziri atuletee watumishi ambao watakuja kufanya kazi ili hadhi ya majengo yaliyojengwa, na Mheshimiwa Waziri ni shahidi, amefika kwenye eneo lile. Mheshimiwa Rais alimsifia kwa kujenga hospitali nzuri na ya kisasa, na mandhari yenyewe ilikuwa ya kuvutia sana. Sasa zile sifa ambazo ulipewa Mheshimiwa Waziri, kazifanyie kazi ulete watumishi. Vile vile Naibu Waziri amefika hapo, ameleta fedha za vitendea kazi na aliwaahidi wananchi kwenye eneo lile ili kufanya maboresho makubwa kwenye Hospitali ya Wilaya. Naomba sana, Mheshimiwa Waziri nendeni mkalete wafanyakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Wilaya ya Tanganyika ina watumishi 20 tu. Kwa hiyo mkija kuangalia hadhi ya hospitali iliyojengwa ni tofauti na vitendea kazi kwa maana ya rasilimali watu. Namwomba Mheshimiwa Waziri, pelekeni watumishi kwenye vituo vya afya ambavyo vimejengwa. Tunavyo vituo vya afya vya Karema, Mheshimiwa Waziri umefika pale. Tunavyo vituo vya afya vya Kasekese, Kituo cha afya cha Mwese, Kituo cha Afya cha Mishamo, tunavyo Vituo vya Afya Nyagala, hivyo vyote havina watumishi. Naomba sana kwenye eneo hili mlifanyie kazi na mtusaidie ili wananchi waangalie huduma iliyoletwa na Serikali iendane na mazingira halisia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Hospitali ya Wilaya tumeletewa x-ray ya kisasa kabisa, nzuri, lakini kwa bahati mbaya hata kutuletea wataalam wa mionzi imeshindikana. Kwa hiyo, huduma hiyo haipo. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri alikuja, aliona hali halisi, lakini vifaa tiba vilivyoletwa, kuna upungufu, wale wataalam wa Tume ya Mionzi wameshindwa kufika kwenye eneo hilo. Naomba Wizara ishughulikie ili wananchi waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliahidiwa na Mheshimiwa Naibu Waziri vifaa tiba, alileta vyenye thamani ya shilingi milioni 270, zikabaki kama shilingi milioni 230 ili hospitali ile iweze kufanya kazi, mpaka sasa bado vifaa hivyo havijakamilika. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba mtuletee hivyo vifaa tiba, sambamba na watumishi ili wataalam wetu waweze kutoa huduma. Tunao watumishi wachache ambao wanajitahidi sana kufanya kazi nzuri ya kuwatumikia wananchi. Kwa bahati mbaya idadi ya wanaohitaji huduma ni kubwa. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba Serikali iangalie tatizo lililopo kwenye Wilaya ya Tanganyika na ukiangalia ni mazingira ambayo ni Wilaya iliyoko pembezoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ilijenga kwa nguvu za wananchi hospitali teule eneo la Ikola kule Tarafa ya Karema na ilijengwa mahususi kwa sababu katika ukanda wa ziwa kuna mlipuko wa magonjwa ya dharura ambayo huwa yanajitokeza, na ukiangalia tumepakana na nchi jirani ya DRC ambapo kuna milipuko ya mara kwa mara ya magonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa bahati mbaya pamoja na jitihada ambazo zilizofanywa na Serikali kupitia halmashauri ya wilaya, bado hatuna hata mtumishi mmoja na kuifanya hospitali ile iliyojengwa kuwa kama eneo ambalo ni mazalia ya popo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Mheshimiwa Waziri utakapopata fursa ya kuja Mkoa wa Katavi, tembelea kwenye eneo hilo uangalie jitihada ambazo zimefanywa na nguvu za wananchi namkaona jinsi walivyojipanga. Tusiangalie tu pale ambapo magonjwa yanapokuja kwenye mlipuko ndio tunakuja kuangalia jitihada za kutatua wakati wenzetu walishafanya jitihada za awali. Niombe na niishauri Serikali wafanye jitihada za dharura kuja kuwasaidia wananchi wa Wilaya ya Tanganyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo ahadi za viongozi ambazo zimetolewa kwenye Wilaya ya Tanganyika. Mheshimiwa Waziri, alifika kwenye eneo la Kata ya Katuma alituahidi kumalizia Kituo cha Afya cha Katuma. Niombe Mheshimiwa Waziri, ahadi yako uikamilishe na wananchi walishatumia nguvu zao na wametumia fedha za mfuko wa hewa ya ukaa kama chanzo cha awali cha kujenga kituo chao cha afya. Kwa hiyo, kilichobaki sasa tunasubiri fedha zile ambazo ziliahidiwa na Serikali ziweze kwenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na ahadi nyingine zilizotolewa na ukiangalia mazingira ya Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ilivyo ni ambulance ambazo ziliahidiwa mbele ya Makamu wa Rais. Tunaomba ahadi ile iweze kutolewa. Ukiangalia jiografia ilivyo tumetembea na Mheshimiwa Waziri anaijua vizuri Wilaya ya Tanganyika jinsi ilivyo. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba ambulance kama tatu hivi kwa ajili ya vituo vya afya cha Kalema, Kituo cha Afya cha Mishamo, Kituo cha Afya cha Mwese. Sambamba na ambulance ambazo zitahitajika kwenye hospitali ya wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie eneo la Bima ya Afya, Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika, wamepata fedha za hewa ya ukaa ambazo waliziingiza kwenye vijiji nane ili wapate huduma ya bima ya afya. Kwa bahati mbaya na masikitiko makubwa sana, pamoja na kuweka fedha nyingi na Mheshimiwa Waziri ndiye aliyekuja kuzindua kwenye eneo hilo, bado huduma ile iliyokusudiwa haipo kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nikuombe ufuatilie jambo hili uone ni kitu gani ambacho nakizungumzia kwa sababu ninaelewa ninachokisema wewe unakifahamu tulishiriki wote lile zoezi. Huduma haipo, wananchi wamelipa fedha na huduma ya afya haipo kabisa kiasi kwamba sisi wawakilishi tunaonekana kama tumeshirikiana na Serikali kuwaibia wananchi kwa sababu hawapati hiyo huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana, naamini haya yote ambayo tumeyazungumzia kama Wabunge, Serikali ikiyachukua ikayafanyia kazi itawasaidia sana wananchi wa eneo la Wilaya ya Tanganyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie hospitali ya Mkoa, hospitali yetu ya mkoa…

NAIBU SPIKA: Ahsante na ndio mwisho wako huo.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana. Ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)