Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii niweze kuchangia katika Wizara hii ya Afya. Awali ya yote niungane na wenangu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, kumpongeza sana Naibu wake, lakini kuipongeza wizara kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, wanafanya kazi kweli kweli. Hakuna asiyejua ndani ya nyumba hii kwamba watu hawa ukiwaambia neno wanakukimbilia, ukiwapa changamoto wanaisikiliza na kuitatua lakini ukiwaita kwenye jimbo lako wanakuja. Leo niwaombe, najua hamjafika Jimbo la Mbinga vijijini, kwa hiyo, niwaombe sana kupitia nafasi hii, tukimaliza hotuba hii au baada ya Bunge hili basi mpate nafasi mfike Mbinga vijijini. Karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze sana na nitoe shukrani kwa Serikali hii ya Awamu ya Sita, imefanya kazi kubwa katika jimbo langu. Nitoe shukrani kwa shilingi milioni 400 kwa ukarabati wa Kituo cha Afya Mapera. Sio hivyo tu, hivi karibuni wametoa milioni 350 vifaa tiba, kituo hiki cha afya sasa hivi kiko full full. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepewa ahadi kupitia mradi wa Global Fund kwamba naenda kupata ambulance. Kwa hiyo, kwa kweli tunashukuru sana. Tukijumlisha na ile ya COVID maana yake tunakwenda kuwa na ambulance hizi mbili. Ahsanteni sana Serikali hii ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maombi, tumejenga sasa hivi na kukamilisha vituo vya afya, Muungano, Matili na Mkumbi lakini pia kuna kituo cha Afya Magagula kwa Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Jenista Mhagama, niombe sana tupeleke maeneo haya vifaa tiba lakini na madaktari wakafanye upasuaji katika maeneo haya. Kwa sababu Jimbo la Mheshimiwa Jenista Mhagama na la kwangu yako Jirani. Kwa hiyo, hata wananchi wanaingilia na wanalima kule upande wa Msonga na Magagula yenyewe. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri, kama ulivyofanya hapa juu fanya pia na pale kupeleka hivi vifaa tiba ili wananchi hawa wapate huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la pili, utoaji wa huduma na huduma hizi za kibingwa. Kama nilivyosema hapo awali, nchi yetu sasa hivi kila mahala kuna majengo mazuri ya kutolea huduma hizi za afya. Tuna zahanati, tuna vituo vya afya, tuna hospitali za wilaya na tuna hospitali za rufaa kwa maana za mikoa na hizi za kanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, huwa ninaumizwa sana na ninasikitika sana pale wananchi wetu wanaposema siendi hospitali hii naenda hospitali fulani. Hapa niwe specific, kwa kule kwetu sisi sasa hivi habari ya mjini ni Ikonda iko Makete. Sasa mwananchi anakuja hana hela anaomba nauli ya kwenda Makate. Unamwelekeza kwa nini usiende hapa hospitali ya wilaya hii? Hakuelewi. Kwa nini usiende usiende pale mkoani kuna hospitali pale General? Hakuelewi anakwambia huduma nzuri zinatoa? Makete. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa kwa kweli niwapongeze kwanza madaktari wetu wanafanya kazi nzuri katika mazingira haya tuliyokuwa nayo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, nikuombe hebu tutafute majibu na utujibu hapa ni majibu gani yatakayowafanya wananchi waliopo huko wakaacha vituo vya afya na hospitali zilizopo maeneo haya waende sasa kwa mfano nilivyosema Ikonda? Sisemi kwa nia mbaya kwamba naichukia Ikonda, hapana naomba mnielewe sana. Hoja yangu tumejenga, tuna vituo vya afya vizuri na majengo mazuri na tuna madaktari maeneo haya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, niombe utupe maelezo mazuri namna gani wananchi wetu hawa wataviamini hivi vituo na kupata huduma? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, ni utoaji wa fedha za dawa. Upo ucheleweshaji mkubwa sana wa utoaji wa fedha hizi za dawa na hasa pale kituo kinaposajiliwa. Inachukua muda mrefu sana kituo kikisajiliwa kuingia kwenye mfumo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitolee mfano katika halmashauri yangu, kuna vituo vimesajiliwa muda mrefu vimechukua miezi mitano mpaka sita kuingia kwenye mfumo. kwa hiyo, niombe Waziri tubadilishe huu utaratibu, kwa sababu sasa hivi Serikali inasomana kwa nini ichukue muda mrefu? Tumesajili labda zahanati, tumesajili kituo cha afya, tumesajili hospitali lakini inachukua miezi mitano mpaka sita kituo hiki kuingia kwenye mfumo. Hawa watu wanafanyaje kazi? Sasa wanaanza kuwa omba omba, wanakwenda kituo fulani wanaomba, wanaenda kituo fulani wanaomba dawa. Hii inaleta shida hata kwenye kile kituo wanachoomba dawa. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, tutafute namna ya kurahisisha mambo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia fedha hizi za basket fund, hapa naomba tuwe na utaratibu mzuri. fedha hizi nadhani zinatoka Wizara ya Afya zinakwenda TAMISEMI halafu ndio zinakwenda eneo la kutolea huduma, lakini zinachukua pia muda mrefu sana. Sasa tatizo hapa sijui wapi wanapochelewesha kati ya Wizara ya Afya au TAMISEMI? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitolee mfano, fedha za mwezi wa saba katika halimashauri yangu, yaani quoter ya kwanza na ya pili zimekuja kutoka Desemba mwishoni. Sasa maana yake kazi yake zinakwenda kufanyiwa Januari. Hapa kutakuwa na ucheleweshaji wa mambo mengi yaliyopangwa kwenye ule mpango. Hata hivyo, tunasababisha hoja kwa hawa watu wa halmashauri. Kwa sababu, kwa nini hawakutekeleza huu mradi kwa wakati husika? Kwa hiyo, niombe sana kama ni Wizara ya Afya na mimi siamini, lakini pia siamini pia kule kwa Mama yangu Kairuki kama ndiko wanakochelewesha. Sasa niombe mkae mzungumze ni wapi hizi fedha zinacheleweshwa? Lakini tuzitoe kwa wakati zikafanye ile miradi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kama nilivyosema pale awali, tumejenga vituo vya afya na vituo hivi vya kutolea hudma za afya ni vingi sana. Iko shida mpaka sasa sealing inayotumika ni ile ile ya miaka mitano. Maana yake ni nini? Kama eneo limejengwa sasa hivi vituo vya afya vitano au zahanati tano mpaka kumi, zahanati hizi zinatumia bajeti ile ile ya miaka mitano iliyopita. Hii inapelekea watu hawa kupata mgao mdogo tofauti na uhalisia uliopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu tupeleke hizi dawa, tupeleke hizi fedha kulingana na hali halisi iliyopo kwenye mazingira hayo. Tunajua na mnajua kwamba Serikali sasa hivi inafanya kazi, kila siku tunajenga, kila siku tunasajili basi tunaposajili tuingize kwenye mfumo na sealing isomeke na dawa ziende kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yangu yalikuwa haya naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)