Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema kwa kunipa fursa hii ya kuendelea kuvuta pumzi hii ya bure. Nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa sana anayoifanya kwenye maeneo yote yanayohusu huduma za jamii kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Ukerewe ni wanufaika wakubwa sana wa mapenzi mema ya Dkt. Samia Suluhu Hassan. Nikupongeze Mheshimiwa Waziri,Dada yangu Ummy, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara. Mheshimiwa Ummy na Naibu Waziri, ninyi ni watu wema sana, ni watu wasikivu, ni watu wafuatiliaji lakini zaidi ni watendaji wazuri na watendaji bora sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sijui nini nitawalipa lakini Mwenyezi Mungu atawalipeni. Hamna baya kwangu na ninaamini hamna baya kwa wananchi wa Ukerewe, hasa kwa mapenzi mema mliyonayo na mipango mliyonayo kwa wananchi wa ukerewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ukerewe nimekuwa ninasema kila wakati tuna changamoto nyingi lakini huduma za afya ni moja kati ya changamoto zinazotusibu sana wananchi wa Ukerewe. Nishukuru kwa miaka michache hii kuna jitihada kubwa za kuboresha upatikanaji wa huduma za afya. Tumeongeza zahanati, tumeongeza vituo vya afya, Serikali imetuletea pesa tumejenga kituo cha afya cha Ilugwa. Mwaka 2022 tumepata pesa tunaendelea na ujenzi wa kituo cha afya cha Murutilima lakini pamoja na zahanati nyingi zinazoendelea, tumejenga Kituo cha Afya cha Igala, yote ni mema.

Mheshimiwa Naibu Spika, maombi yangu kwako Mheshimiwa Waziri, pamoja na changamoto tulizonazo lakini niombe sana vituo hivi tulivyovijenga bado havina vifaa. Niwaombe sana mtusaidie vituo hivi vitatu vya afya vipate vifaa. Lakini zahanati ambazo tumejenga kwa kushirikiana na wananchi, zahanati zaidi ya sita, vilevile, tupate vifaa ili zianze kutoa huduma kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, pale Bwise mmetuletea pesa tumekamilisha ujenzi wa kituo cha afya kikubwa sana ambacho tumekipandisha kuwa Hospitali ya Wilaya na Kituo cha Afya cha Muliti, bado vituo hivi havina majokofu kwa ajili ya kutunzia miili ya wenzetu walioaga dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotokea kwa mfano pale Muliti hata pale Ukara, ikitokea mwenzetu kaaga dunia inabidi tusafirishe kupeleka hospitali ya wilaya kumhifadhi halafu ndio taratibu nyingine ziendelee. Ni mateso kwa wananchi wetu, mtusaidie ili tuweze kuboresha kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna changamoto ya watumishi. Mheshimiwa Waziri, nishauri sijui kama itawezekana lakini ni jambo jema. Sisi pale Ukerewe kwa sababu za kijiografia wanakuja watumishi lakini muda mfupi wanaondoka kwa sababu mbalimbali. Mnaonaje mkianzisha chuo cha uuguzi na uganga pale Ukerewe? Ili kupitia Chuo kile wanafunzi wakiwa wanapata mafunzo yao pale wakiwa wanatumia muda wao wa mafunzo kufanya mazoezi kwenye zahanati, hospitali na vituo vyetu vya afya, inawezekana ikasaidia sana kupunguza changamoto ya watumishi tuliyonayo kwenye hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri na wizara kwa ujumla, tulileta kilio kwenu kuonesha changamoto tulizonazo kwenye visiwa vya ukerewe hasa tunapopata wagonjwa wa dharura wanaohitaji rufaa kwenda kupata huduma kwenye hospitali ya mkoa. Mlitusikiliza mkaridhia kujenga hospitali ya rufaa kwa ngazi ya mkoa kwenye Visiwa vya Ukerewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni jambo jema sana ninashukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Ukerewe. Lakini niwapongeze sana kwa changamoto zilizojitokeza namna mlivyotusaidia kuzishughulikia mpaka hapa tulipo leo. Mheshimiwa Waziri, ulinipa jukumu la kutafuta eneo ili tuendelee na ujenzi wa hospitali yetu ile ya rufaa ngazi ya Mkoa. Nikuhakikishie tayari kwa kushirikiana na viongozi wenzangu tumekwisha kamilisha mchakato huo eneo limepatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe baada ya bajeti yako kupitishwa, ninaimani wala sina shaka tutaipitisha, twende ukerewe, ukajiridhishe na eneo lile ili kazi iendelee. Hautakuwa na baya kwa wananchi wa Ukerewe, hautakuwa na baya kwangu na kama nilivyosema wema wenu Mwenyezi Mungu atawalipeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na haya yote bado tuna changamoto ya madawa, kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma za afya bado shida kubwa sana ni upatikanaji wa madawa. Wamesema wenzangu waliotangulia kuchangia, kwenye eneo la MSD ambao tunatarajia kwamba wawe waokozi wetu kwenye eneo la madawa, bado kuna shida kubwa sana kwamba hawana mtaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, ili kuweza kuondokana na hili na Kamati yetu inayohusika na masuala ya Afya wametoa pendekezo, Mheshimiwa Waziri, niombe sana tuwawezeshe MSD. MSD wakipata uwezo kwa mfano kwa mapendekezo yaliyotolewa na Kamati, wakipata fedha hizi bilioni 500 ninaamini matatizo makubwa tunayokutana nayo sasa kwenye upatikanaji wa huduma za afya hasa kwenye eneo la madawa inawezekana tukaondokana nalo.

Mheshimiwa Naibu Spika kwa hiyo, niungane na waliopendekeza hasa Kamati, tuwape mtaji MSD, tukiwapa mtaji MSD haya matatizo tunayokutana nayo inawezekana yakaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa Waziri, pamoja na kazi kubwa sna mnayofanya na pamoja na kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais, bado kuna shida hasa kwenye sera yetu ya afya kwenye utoaji wa huduma za afya kwenye kundi la wazee, lakini na watoto wachanga chini ya miaka mitano. Bado kuna tatizokubwa! Kuna kila sababu ya Mheshimiwa Waziri kupitia shida iko wapi? Kwenye eneo la watoto wachanga, kinamama wajawazito lakini vilevile kwenye kundi la wazee. Ili changamoto zilizopo basi tuzifanyie marekebisho ili sera yetu tuitekeleze kikamilifu na watu wetu waweze kupata huduma ile inayotarajiwa. Kama tutaweza kuboresha eneo hili hata changamoto tunazozipata katika ku-initiate hili suala la Bima ya Afya kwa watu wote inawezekana tukaondokana nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niliona nichangie kwenye maeneo hayo; lakini nimalizie kwa kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri na timu yako yete kwa kweli mnafanya kazi kubwa sana. Mmetembelea Ukerewe mmetutia moyo na changamoto tulizokuwa nazo mmezifanyia kazi, na niwaombe muendelee kuzifanya kazi. Zaidi ya yote niendelee kuwashukuru sana na kuendelea kuwakaribisha Jimboni Ukerewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa na ninaunga mkono hoja. (Makofi)