Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi jioni hii ili niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyopo mbele yetu. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake na watendaji wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanayoifanya. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa namna anavyofikika kirahisi pamoja na Naibu wake, lakini naomba nitoe case study ndogo kwa Mheshimiwa Waziri Ummy pamoja na Mheshimiwa Angellah Kairuki kupitia Fedha za Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO–19. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walipatiwa fedha bilioni 69.1 kwa ajili ya kununua magari ambulance na magari ya kusambazia dawa, chanzo lakini walipoona bei ya supplier ni kubwa waliamua kufanya mazungumzo na UNICEF. Kwa hiyo, wakaweza kununua magari haya moja kwa moja kwa mzalishaji. Bei waliyopewa na mzabuni ilikuwa milioni 144.3 kwa ajili ya basic ambulance na gari la chanjo milioni 163, lakini badala yake walinunua ambulance kwa milioni 99 na la chanjo wakanunua milioni 162. Kwa hiyo waliokoa fedha taslimu bilioni 13.2 na hivyo wakaongeza magari kutoka 503 hadi 663. Kukawa na ongezeko la magari 160 na magari hayo 160 yana uwezo wa kusambazwa katika halmashauri zote zilizopo nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hapa tunalo la kujifunza, tuendelee kuangalia Sheria zetu za Manunuzi, tuiruhusu Serikali au taasisi kunapokuwa na manunuzi makubwa wanunue moja kwa moja kwa mzalishaji. Tutaokoa fedha nyingi ambazo zitafanya kazi nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hivyo hivyo naomba nijielekeze…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, hilo analolizungumza Mheshimiwa Mbunge ni sahihi kabisa na lilifanyika chini ya GPSA na Wizara ya Afya wakaamua kumuacha GPSA na kuenda kununua hayo magari na kuokoa zaidi ya bilioni kumi na kitu ambazo zimetajwa. Kwa hiyo ule msimamo wa Mheshimiwa Rais ni kweli GPSA lazima waondoke kwa sababu walitaka kuiangamiza Wizara ya Afya kwenye ununuzi wa magari. Ahsante sana na hongera kwa mchangiaji. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ummy haya ndio nataka uandike kwenye taarifa yako uyaseme. Haya Mheshimiwa Leah.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, naunga mkono hoja kabisa kabisa yapo manunuzi makubwa yanafanywa tunaendelea kupoteza fedha kwa kupitia watu wa kati badala ya kwenda moja kwa moja kwa mzalishaji. Suala hili pia lipo upande wa manunuzi wa madawa, tuiruhusu MSD kunapokuwa na manunuzi makubwa waende moja kwa moja kwa mzalishaji na haya yafanywe, sheria iletwe hapa tuweze kufanya mabadiliko ya sheria. Niombe sheria upande wa madawa isilingane na vifaa vingine kutokana na umuhimu uliopo kwa dawa za binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kabisa MSD ina changamoto ya upatikanaji wa fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa na sisi Kamati ya Bajeti mwaka jana tulipendekeza unapoanza mwaka wa fedha wakopeshwe bilioni 150 na Benki Kuu ili wanunue madawa. Hospitali zinapohitaji dawa MSD wakutwe wanazo, sio hospitali zinapohitaji dawa ndio MSD waende wakanunue. Suala hili halijatekelezwa lakini naunga mkono maombi yao ya kuomba bilioni 592 kuweza kufanya maboresho MSD.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba hizo fedha zina mgawanyo, uwekezaji, ujenzi wa maghala pamoja na usambazaji wa madawa kwenye item ya madawa, naomba kutoa ushauri mnapoenda kufanya maboresho, lakini maboresho haya bila kuziba mianya ya uvujaji wa dawa, bado katika jambo hili watakuwa hawajafanya kitu chochote. Niwaombe katika fedha walizoomba wameweke kipengele cha udhibiti cha TEHAMA, kuwepo na mfumo katika upokeaji na utoaji wa dawa hadi kwa mgonjwa ili tuweze kujifunga wapi dawa zinapotelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe mfano kwa Hospitali yetu ya Taifa ya Benjamin William Mkapa, inayo mfumo mzuri wa utoaji wa dawa. Naomba na hospitali za mkoa nazo basi zijifunze kupitia Benjamini Mkapa na hapo tunaweza tukajua wapi dawa zinavuja, wapi dawa zilipotelea, lakini pia wataalam wetu wa hospitali hawana weledi wa kutosha katika matumizi ya mfumo na hii inapelekea fomu nyingi kuweza kukataliwa Bima ya Afya. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi/Kicheko)