Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kutoa shukrani nyingi sana kwa kupewa nafasi hii ya kuchangia katika Bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri wa Elimu, Profesa Adolf Mkenda, Katibu Mkuu na watumishi wote wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa hotuba nzuri ya bajeti ya suala ambalo ni muhimu sana ambalo ni elimu na maarifa, sayansi na teknolojia kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuliendeleza gurudumu hili la mapitio ya uboreshaji wa Sera ya Elimu na Mitaala katika nchi yetu. Serikali ya Awamu ya Sita imefanya jambo kubwa sana kukamilisha sera hii na sasa kuileta kwa wananchi ili wananchi waweze kuijadili na kutoa maoni yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Elimu ni muhimu sana. Serikali ya Awamu ya Sita na zilizopita zimewekeza sana katika miundombinu (hardware). Yawe ni majengo, ziwe ni maabara na sasa inajikita katika eneo muhimu sana la kuwekeza katika software na software ya elimu ni sera na mitaala. Hili ni zoezi muhimu na ni vyema niiombe Wizara makongamano na mijadala hii ambayo tumeiona iendelee katika maeneo mbalimbali ya Tanzania ili wananchi watoe maoni yao katika jambo hili muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja ambalo napongeza sana katika mwelekeo mpya wa sera ni sasa kuitoa elimu ya lazima kutoka darasa la saba na sasa kwenda kidato cha nne. Takribani sasa miaka 58 toka elimu ya lazima ilipotolewa darasa la nne kwenda darasa la saba na maamuzi yale ya kijasiri yaliyofanywa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1968 kutoa elimu ya lazima toka darasa la nne kwenda darasa la saba. Katika kipindi cha mpito kuanzisha shule ambazo ziliitwa extended primary school, yaani zile shule za darasa la nne zikaongezewa darasa la tano, la sita na la saba na wale wanafunzi walipofika darasa la saba wakafanya mtihani mmoja na wanafunzi wa darasa la nane middle school na ndiyo ikawa mwisho wa middle school. Kwa hiyo mambo haya yanayofanyika ni mambo makubwa takribani miaka 58 baada ya kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naunga mkono suala la kuwa na elimu ya msingi ya miaka sita ikifuatiwa na elimu ya sekondari ya miaka minne. Jambo hili pia siyo jipya sana, wale waliosoma miaka ya 1920, 1930 na 1940 palikuwa na aina mbili ya shule wakati ule, mmoja wa hao waliosoma ni Baba yangu. Palikuwa na District Schools na kwenye District Schools wanafunzi walisoma darasa la kwanza mpaka darasa la sita na baada ya hapo wakaenda kwenye central schools. Kwenye central schools walisoma miaka miwili, darasa la saba na la nane na baadaye wengine walikwenda kwenye taaluma kama vile Ualimu kwa miaka mitatu na wengine waliendelea darasa la tisa na darasa la kumi ili kupata sifa ya kwenda kusoma diploma ya elimu Makerere. Tutakapopata muda wa kuchangia haya tutayachangia zaidi ili kuzidi kuboresha hili jambo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo naomba nichangie katika maeneo mawili au matatu kama muda utaruhusu. Eneo la kwanza ni FDC, Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na eneo la pili elimu ya watu wazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa katikati palitokea upotoshaji kwamba Vyuo vya Wananchi - FDC ni vyuo vya CCM, siyo kweli. Vyuo vya Wananchi -FDC vilivyoanzishwa mwaka 1975 vilikuwa ni wazo la Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere baada ya kutembelea nchi za Nordic na hasa Sweden alipokuta kule wana aina hii ya vyuo na vyuo hivyo ndiyo vikaanzishwa mwaka 1975 na kwa miaka mingi sana vilikuwa vina hisaniwa na Shirika la Fedha la SIDA la Sweden na lilipojitoa watu waliona labda vyuo hivi vitakufa lakini nashukuru vinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Wizara ya Elimu sasa iwekeze kwa kiasi kikubwa sana katika hivi Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na ikiwezekana Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi viwe katika kila Kata ya nchi yetu. Kwanini nasema hivyo? Bado tuna kundi kubwa la wanafunzi waliomaliza darasa la saba hawakufaulu kwenda sekondari. Bado tuna kundi tena la wanafunzi waliomaliza Kidato cha Nne lakini hawakufanikiwa kupata taaluma. Pia tuna kundi la wanafunzi ambao wamesomea fani mbalimbali hata Vyuo Vikuu lakini hawana cha kufanya katika maeneo wanayoishi kutokana na kukosa stadi mbalimbali katika kilimo, ufugaji, ujasiriamali na ili waweze kujitegemea ninaona vyuo vya kufanya kazi hiyo ni Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mabadiliko haya ya Sera na Mitaala, kijana atakayemaliza Kidato cha Nne na sasa anaamua haendelei anakwenda kijijini au anakwenda kujiajiri bado atahitaji kuwa na mafunzo ya orientation. Mafunzo ya kumuandaa kwenda kwenye jamii, mafunzo ya kumuandaa kwenda kufanya anachokitaka kukifanya na chuo cha kufanya kazi hiyo mimi naona ni Chuo cha Maendeleo ya Wananchi - FDC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wale ambao tayari watakuwa wamejiajiri wana fani mbalimbali, wana taaluma mbalimbali, wana kazi mbalimbali, kila mara watahitaji kupata mafunzo ya maeneo mapya yanayojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliusikiliza kwa makini sana mchango wa Mheshimiwa Jumanne Kishimba katika kongamano lile la sera mpya ya elimu na mitaala mipya ya elimu. Alipoeleza kwamba leo kuna uhitaji mkubwa sana wa mafundi wa simu, leo kuna uhitaji mkubwa sana wa mafundi wa pikipiki. Sasa ili kufanya mambo haya hatuwezi kuitegemea VETA ifanye hivyo. Mimi naona vyuo vya kufanya kazi hiyo vitakuwa ni Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kwa sababu vyenyewe vinaweza kuwa na mafunzo ya muda mfupi lakini pia kuwa na mafunzo ya outreach program kuwafikia vijana na kuwafikia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuweke umuhimu sana katika vyuo hivi na sasa tuwekeze zaidi, na mimi niishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutoa shilingi 645,764,808 kukarabati Chuo cha Kilosa cha Maendeleo ya Wananchi pale Ilonga. Chuo kile sasa kina mandhari nzuri, kina kazi nzuri lakini kinapungukiwa na vifaa, kinapungukiwa pia na wakufunzi. Kwenye suala la wakufunzi ningependa katika Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi tuwe na aina mbili ya wakufunzi. Tuwe na wakufunzi wa kudumu ambao ni permanent lakini pia tuwe na wakufunzi wa kujitoela katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili nalitilia umuhimu sana kwa sababu nchi hii inahitaji aina hii ya vyuo ili kuwawezesha vijana wetu na wananchi wote kila wakati kunoa maendeleo yao na kuendelea kuwa muhimu katika jamii zao. Kwa hiyo, tuviongezee fedha vyuo hivi. Tuviongezee rasilimali vyuo hivi, tuviongezee wataalam vyuo hivi, lakini ningependa pia nimuombe Waziri wa Elimu, suala hili la FDC sasa pia liingie ndani ya sera ya elimu ambayo tunaifanyia mapitio na maboresho sasa ili iwe ni sehemu ya mfumo wa elimu katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo ningependa kulichangia ni elimu ya watu wazima. Mara baada ya kupata uhuru, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alitangaza maadui watatu ambao ni ujinga, umaskini na maradhi. Kwenye ujinga tulikuja na suala la elimu ya watu wazima na tumefanya vizuri sana, mkazo wa elimu ya watu wazima wakati ule ilikuwa ni katika eneo la kusoma, kuandika na kuhesabu. Katika kusoma, kuandika na kuhesabu tumefanya jitihada kubwa sana lakini wakati umefika sasa na hili pia ningependa liingie katika sera ya elimu, tuje na mtazamo mpya kuhusu elimu ya watu wazima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya watu wazima siyo tu kwa wale ambao hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu. Elimu ya watu wazima inahitajika na watu wote hata wenye Phd kama mimi. Hata mimi pia nahitaji elimu ya watu wazima, maana yake tuwe na mtazamo mpya sasa wa elimu ya watu wazima ambayo itawagusa watu wote wa rika zote, wa elimu zote, wa mahitaji yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili kutokana na uzoefu. Katika miaka ya 1990 na miaka ya mwanzo ya 2000 ilionekana kuna umuhimu sasa wa kutunga Sheria za Mazingira na kuwafanya Majaji na Mahakimu wetu wazimudu sheria mpya za mazingira na wawe na elimu ya mazingira, mimi ni mmoja wa watu ambao Umoja wa Mataifa ulinichukua niwe mmoja wa wataalam waelekezi wa kuandaa mitaala ya kuwasaidia Majaji na Mahakimu kujua elimu ya watu wazima. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya jambo hilo niliona umuhimu wa kujifunza elimu ya watu wazima kwa ngazi zote. Kwa hiyo, nisisitize sana umuhimu wa elimu ya watu wazima katika nyanja zote na sera iliangalie hilo katika upana wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na mengine ya kuchangia katika suala la sayansi na teknolojia, tuwekeze katika maeneo mapya lakini hilo nitatoa mchango wangu kwa maandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikujua kwamba muda ni mfupi lakini nashukuru sana. Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi, Elimu ya Watu Wazima iingie katika sera ya sasa ya elimu ili tuweze kusonga mbele kama Taifa jipya linalojitambu na kujifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)