Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

Hon. Mwantum Dau Haji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nichukue fursa hii ya kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Mwanaidi Khamisi kwa jitihada zao wanazozichukua katika Wizara hii wanafanya kazi sana usiku na mchana kutokana na shughuli zetu hasa hizi za wanawake na watoto pamoja na maendeleo mengine yaliyokuwemo humu nchini, nakushukuruni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuendelea kwanza nizungumzie kuhusu suala la mgogoro wa ndoa. Mgogoro wa ndoa hapa nchini, wamefanya jitihada katika taarifa yao humu nimeisoma wamefikia malengo makubwa lakini bado, bado katika kazi ya hii inaendelea mgogoro huu wa ndoa, bado wanawake wananyanyasika ndani ya ndoa zao. Kwa sababu kama mnavyojua hii nchi yetu ni kubwa ina mambo mengi mengi tu kuhusu wanawake na hasa masuala ya ndoa bado nazidi kuzungumzia kwamba wanawake wanajitihada kubwa, ndoa zao na wanajitahidi kwamba wakae na ndoa zao ndani ya majumba yao ili wakae na waume zao ndani ya majumba yao na watoto wao.

Mheshimiwa Spika, matokeo yake wananyanyasika kutokana na hizi ndoa ndani ya nyumba. Wanajitahidi na wanahangaika huku na kule, wanachukua mpaka mitaji yao ili ndoa zao zidumu lakini bado, bado kabisa. Mheshimiwa Waziri hili suala litizame kwa kina juu ya Serikali yetu lizidi kuchukua fursa hii ya kuweza kukaa na hawa wanawake wetu wa ndoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuendelea kuhusu wanawake, wanawake wamepatiwa fursa ya kujengewa uwezo wa kupatiwa elimu ya kodi, urasilimishaji wa biashara, hifadhi. Lakini kutokana na biashara hizo wanazozifanya waliyopatiwa kweli hii fursa ya kujengewa uwezo lakini na wao pia tasema bado fursa ingali ndogo.

Mheshimiwa Spika biashara zao wanapokuwa wanazifanya hawana masoko ya uhakika japokuwa humu mmeandika kwamba yapo masoko wafanye mpaka China imefika kusema humu lakini wengine hawana uwezo huo wa kufanyia biashara zao wakafikia malengo hayo.

Mheshimiwa Spika, wanawake bado vilevile tunanyanyasika humu nchini kutoka na biashara zetu tunazozifanya ni biashara ndogo, ndogo hazikidhi kufikia malengo mpaka wakafikia hatua ya kupata masoko ya uhakika ili kufanya biashara zao wakaendelea kufanya vizuri kwenye biashara zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazunguzia kuhusu udhalilishaji sasa, kuhusu udhalilishaji Mheshimiwa Waziri pia umeuzungumzia humu kweli mmechukua hatua kubwa za udhalilishaji lakini bado udhalilishaji umeongezeka kama watu waliyoambiwa kafanyeni makusudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanawanyanyasa watoto wetu, wanawanyanyasa wanawake kijinsia bila tatizo hata kama mtu kapata ule uthibitisho kwamba huyu kweli kanyanyasika. Hili sasa hivi ndiyo linalonishughulisha, anakwenda kunyanyaswa mwanamke au wananyanyasa Watoto wetu kijinsia lakini akienda zake Mahakamani anachukuliwa dhamana yule mfanyaji wa kile kitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kweli hapa siye tutafika mahali? Hatufiki mahali kwa sababu tayari kaishachukuliwa hatua yule mwanaume atoke aende zake akakae nje, sijui kama aende akabake tena? au sijui akajitetee kivipi? Lakini hili suala bado halijawa zuri hapa nchini kwetu ingali lina nyanyasa watoto wetu na wanawake na anapochukuliwa dhamana huyu anakwenda zake, anakwenda kufanya vitendo vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri bado hili suala halijafikia malengo kabisa, halijafikia malengo na nasema hapa Mheshimiwa Condester, alisema hapa juzi kuna pombe hizi watu wa humu wanapokunywa wanakuwa hawana nguvu za kiume. Kwa nini hawapewi ili wakatoka hizi nguvu za kiume? Tukatokana na hili suala lililokuwa tunalo hapa nchini, wapewe wanywe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana kuhasiwa hawataki, kuhasiwi lakini wapewe hizi pombe wanywe ili wakatike nguvu za kiume labda tunaweza kupata suluhisho la hawa watoto wetu kunyanyasika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri naomba chonde chonde hili suala bado kabisaa halijafanyiwa kazi na huko nje bado watoto wetu wananyanyasika hizi pombe hizi wapewe ili waweze kuvunjika nguvu za kiume na watoto wetu waweze kupona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri naunga mkono hoja, asilimia mia moja Wizara hii ya Wanawake na Watoto hapa tulipo hivi sasa hivi tunaipitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi/Vigelegele)