Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima na Naibu wake Mheshimiwa Mwanaidi Ali Khamis na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa kutenga kiasi cha shilingi 74,223,193,000 kutekeleza shughuli za Wizara.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kuhusu hali ya wazee hapa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika vipaumbele 10 vya Wizara kwa mwaka wa 2023/2024, kipaumbele namba nane kinasema; "kuratibu na kuwezesha upatikanaji wa haki za watoto na huduma za ustawi wa jamii kwa wazee."

Mheshimiwa Spika, kutokana na kipaumbele hicho cha Wizara hapo juu, ni dhahiri kwamba masuala ya wazee yanahitaji msukumo wa kipekee. Tunaishukuru Wizara kwa kutenga shilingi bilioni 1.8 kusaidia wazee kwa mwaka huu wa pesa wa 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, wazee ni watu muhimu ambao wengi wametulea. Wazee wengi huko vijijini wamechoka, hawana uwezo na inalilazimu Taifa kuwatazama.

Mheshimiwa Spika, wazee wengi wanachukuliwa kama tabaka lililotengwa, hivyo ni vyema wakahudumiwa na kupatiwa matibabu, makazi, vyakula, kuwasaidia fedha za kujikimu kama ilivyo kwenye mataifa mengine na majirani zetu wa Zanzibar kupitia Pension Jamii.

Mheshimiwa Spika, kuna sera inayosema matibabu ni bure kwa wazee, lakini wakienda hospitali wanaambiwa ni wale wasiojiweza na wanakosa dawa na matibabu.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine inayowakabili wazee wetu ni ukatili dhidi yao. Ukatili huu umekuwepo kwenye baadhi ya jamii yetu kwa miaka mingi. Jambo hili halijatiliwa mkazo unaostahili katika baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Spika, ukatili huu unafanywa katika ngazi ya kaya na vijiji na watu wa karibu ambao ndiyo hutambulika kama wasaidizi wa karibu wa wazee katika ngazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu, ninaishauri Serikali ifanye yafuatayo: -

Kwanza, Serikali ishiriki kwenye kujengea uwezo mashirika yanayojihusisha na masuala ya wazee, mabaraza ya wazee ngazi ya mikoa na wilaya, asasi za kutetea haki za binadamu na kuchukua juhudi za kuielimisha jamii juu ya haki za wazee na umuhimu wa kumlinda mzee.

Pili, Serikali ipange bajeti ya kutosha ya kuwahudumia wazee wasiojiweza na kuhakikisha wanapata tiba, makazi na chakula. Kiasi cha shilingi bilioni 1.8 zilizotengwa kwa mwaka 2023/2024, hazitoshi.

Tatu, Serikali iwalipe wazee Pension Jamii kama ilivyo huko Zanzibar.

Nne, Serikali itenge fungu maalumu kuwasaidia wazee waanzishe miradi ya kujiongezea kipato kama vile ufugaji wa kuku, nyuki, mbuzi na ng’ombe.

Tano, Serikali ifikirie kuwa na wawakilishi wa wazee huku Bungeni kama kundi maalumu kwani makundi ya vijana na akina mama wana uwakilishi.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu naunga mkono hoja.