Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii, nianze kusema kwamba mmoja wa wasemaji pale wa UKAWA amesema kwamba taarifa yangu ya jana, mimi ndiyo Mwenyekiti wa Kamati ya TAMISEMI ina tarehe zilizokosewa, imeandikwa Aprili, 2015, ni kweli imekosewa, lakini hili siyo kosa langu wala siyo la Kamati yangu, ni matatizo ya uchapaji tu ya Idara ya Takwimu Rasmi za Bunge, Hansard siyo kosa la Kamati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna methali ya Kiingereza kwamba kama unaishi nyumba ya vioo usiwe wa kwanza kutupa mawe. Taarifa ya Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Mheshimiwa Lucy Mollel ilisomwa jana baada ya mimi pale, tarehe 27 mwezi wa Nne, lakini imeandikwa tarehe 28 mwezi wa Nne; na yenyewe imekosewa sasa sijui alichokuwa anasema ni kitu gani. Bora angeangalia zote mbili kwanza akajiridhisha na hali ilivyo ni makosa si ya kwetu wala sio ya Lucy Mollel, ni ya Hansard. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa kazi anazozifanya, kazi nzuri sana yenye tija, anatetea wanyonge, amesema sasa hivi hapa kutumbua majipu na mengine. Kubwa sana kupambana na ufisadi, aliahidi alipokuwa anagombea mwaka jana kwamba akiwa Rais ataanzisha Mahakama ya Mafisadi na juzi amesema kwamba mwezi wa Saba Mahakama hiyo inaanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri wengine wanaohusika, Waziri wa Sheria na Mawaziri wengine, Mahakama hii ikianza ianze na fisadi namba moja anajulikana, fisadi namba moja nchi hii anajulikana. Aligombea urais kupitia chama fulani, alikuwa na ndege kadhaa za kukodi siku sitini na nne anakodi ndege kadhaa, hela aliipata wapi? Alikuwa na magari mengi, msururu, alikuwa na watu mia tano anahama nao kila Mkoa ili aonekane ana watu wengi, hiyo hela aliipata wapi, anawapa posho, anawapa nauli, malazi, hiyo hela aliipata wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ianze na huyo ajieleze kusudi kama sio fisadi mahakama itamsafisha. Hata hivyo, CHADEMA waliandika kwenye orodha yao ya list of Shame walimwandika kwamba ni fisadi namba moja, watafurahi sana nafikiri akishtakiwa yule. Ashtakiwe ili na wenyewe waridhike, wapate amani kwamba fisadi wao ameshtakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais Dkt. Magufuli alipokuwa kwenye kampeni Kagera mwaka jana aliahidi mambo kadhaa. Mojawapo ni meli pale ziwa Viktoria, bahati nzuri tumeona kazi zinafanyika, meli tumeiona kwenye vyombo vya habari inatengenezwa huko nchi za Ulaya. Tunaomba meli hiyo isimamiwe haraka, ikamilike na nyingine ya Lake Tanganyika, Lake Nyasa zije zituhudumie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Bukoba leo mfuko wa cement shilingi elfu ishirini na moja, Dar es Salaam shilingi elfu kumi na tatu, tofauti hii ni sababu ya usafiri wa malori, gharama kubwa sana na inaharibu barabara. Tukipata meli tutapata nafuu kubwa, ni usafiri mzuri una nafuu hata ya gharama na ni salama zaidi, tupate meli hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia aliahidi kushughulikia suala la ushuru kwenye mazao ya kahawa, tulimwambia kuna kodi ishirini na sita na alivyokuwa hapa alirudia kwamba kodi hizi ataziondoa, Mawaziri wanaohusika naomba mshughulike na jambo hili, hu ushuru na kodi ziondolewe kwenye mazao, kahawa, korosho, pamba na kwingineko ili wakulima wapate jasho la matunda yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Bukoba kahawa inapelekwa Uganda ambapo bei ipo juu, kwa nini Uganda bei iwe juu hapa iwe chini, ushuru upunguzwe, kodi zipunguzwe wananchi hawa wapate kuuza mazao yao hapa na tuweze kupata hela ya kigeni, tujenge barabara, tupate huduma ya maji, tujenge shule na hospitali badala ya kuwanufaisha wenzetu wale wa nchi jirani wa Uganda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mradi wa mabasi yaendayo kasi wa Dar es Salaam (DART). Nimesoma jana pale kwenye taarifa yangu lakini nisisitize, niishukuru Serikali kwa kazi kubwa iliyofanya mradi umekamilika ule, barabara zimekamilika, vituo vimekamilika, miundombinu ipo sawasawa, mabasi yapo zaidi ya mia ngapi pale jangwani na vitu vingine. Sasa uanze bado vitu vidogo tu, gharama kubwa imetumika kwenye mradi ule, uanze tarehe 10 mwezi wa Mei, tuondokane na kero ya misongamano barabarani ambayo inaweka uchumi mbovu, watu wanachelewa kazini, wanachelewa hospitali na huduma nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia takwimu za NBS mwaka 2014 hasara ya foleni za Dar es Salaam wanasema ilisababisha hasara ya shilingi bilioni 411 kwa mwaka mmoja, foleni za Dar es Salaam. Ule mradi Awamu ya Kwanza Kimara mpaka feri na hii ya Morocco na Msimbazi imegharimu shilingi bilioni 622, ni chini ya hasara ya mwaka mmoja ya foleni za Dar es Salaam. Kwa hiyo, kwa kweli mradi huu uanze tuondokane na kero hii na hasara kubwa ambayo tunaipata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tena kwamba niwapongeze wenzangu wa UKAWA, leo wameanza kuchangia baada ya mgomo waliokuwa nao, nawapongeza. Saa hizi asubuhi walianza kuchangia kwa kudai televisheni ya Taifa iwaonyeshe; nasema hakuna kwa sababu haiwezekani TV ije hapa kuonyesha miongozo, taarifa, fujo, matusi, haiwezekani. TBC hawana fedha wameshasema kwamba hela yao haitoshi hawawezi kuja hapa konyesha fujo na kelele. Tena wasije kabisa hata ile asubuhi ingefutwa, tufanya kazi humu ndaniā€¦
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti naendelea, nizungumzie vyuo vya VETA...
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Vyuo vya VETA, naomba Wizara inayohusika...
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwe na vyuo vya ufundi kila wilaya, ufundi ni kila kitu, maendeleo yote ni ufundi, nyumba nzuri kama hii ni ufundi ndiyo maendeleo, barabara ni ufundi, kuleta maji vijijini au mitaani ni ufundi, kujenga reli na barabara na madaraja ni ufundi, tuwe na vyuo vya ufundi kila mahali. Kagera hakuna chuo cha VETA mkoa mzima. Hii nitataka maelezo kwa mhusika atakapokuwa anatoa taarifa pale mwishoni, tupate maelezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Halmashauri zetu kuna Halmashauri ambazo zina wizi wa kutisha, wanaiba pesa, wanahamisha matumizi, nimemwandikia CAG Halmashauri ya Bukoba kuna wizi nayo inataka maelezo, nimempa nakala Waziri, naomba waje wafanye ukaguzi maalum pale tubaini wezi ili washughulikiwe. Hili na lenyewe nitataka maelezo kutoka kwa Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anajumuisha hoja yake,
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naunga mkono hoja.