Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja hii. Kwanza niwashukuru sana wananchi wa Wilaya ya Mpwapwa kwa kutuchagua sisi Wabunge wawili na wote tunaitwa George, kwa hiyo tuwashukuru sana Madiwani wote thelathini na tatu wote ni wa CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Magufuli, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya. Hata hivyo, mwaka jana wakati wa kampeni aliwaahidi wananchi wa Wilaya ya Mpwapwa kwamba barabara ya kutoka Mbande - Kongwa - Mpwapwa mpaka Kibakwe itajengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpwapwa ni ya zamani sana, sasa ina zaidi ya miaka mia moja tangu mwaka 1905 Mpwapwa ipo, lakini hakuna hata barabara ya lami, barabara zote za mjini ni vumbi. Kwa hiyo, naomba sana hili litekelezwe na barabara za Mpwapwa Mjini kilometa kama kumi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI anaifahamu vizuri Mpwapwa, basi aweke lami katika barabara zote hizi hata Kibakwe aweke lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru, niwapongeze Mawaziri kwa bajeti zao nzuri, lakini niishukuru Serikali kwa kuongeza bajeti, toka asilimia ishirini na saba mpaka asilimia arobaini. Hata hivyo, tuna tatizo, amezungumzia Mheshimiwa Tizeba hapa kwamba miradi mingi imekwama, haijatekelezwa, hapa kazi yetu Bunge ni kupitisha bajeti, ni matarajio yetu kwamba tukipitisha bajeti fedha zinapelekwa Halmashauri na fedha zile basi zifanye kazi ya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingi imekwama katika Wilaya zetu, fedha zinachelewa kuletwa kwenye Halmashauri, hatujui sababu ni nini, ni nani anayekwamisha hii, fedha zinakuja zimechelewa, wakati fulani zinaletwa fedha kidogo, si kile kiwango ambacho Bunge limepitisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano Wilaya ya Mpwapwa kwa jimbo langu na lina vituo viwili vya afya sasa ni miaka kumi havijakamilika, Kituo cha Afya cha Mima na Kituo cha Afya cha Mbori. Miaka kumi fedha haitengwi kwa nini, akinamama wanapata taabu kujifungua kupelekwa mpaka Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa, wengine wanafia njiani. Kwa hiyo, naomba sana katika bajeti hii, Serikali ihakikishe vituo vile vinakamilishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali ya Awamu ya Tano, Mheshimiwa Waziri Mkuu yupo hapa, hebu simamia hizi fedha ziende kwenye miradi ya maendeleo zisichelewe, kwa nini hizi fedha zinacheleweshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni mradi wa maji katika Mji wa Mpwapwa. Mji wa Mpwapwa kulikuwa na mradi wa maji ambao gharama yake ilikuwa ni bilioni nne na milioni saba, lakini mradi umekamilika Mheshimiwa na wananchi wanapata maji, wakazi zaidi ya hamsini elfu lakini tatizo kuna mota moja imeungua, kwa hiyo, maji yamepungua wananchi wanapata shida. Hivi naiuliza Serikali hivi mota ya shilingi ishirini na tano milioni, Serikali inaweza kushindwa kununua kweli, naomba sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu barabara, Wilaya ya Mpwapwa ina mtandao wa barabara kilometa elfu moja na mia saba, barabara ya kutoka Mpwapwa kwenda Gulwe, Kibakwe, rudi mpaka Chipogoro ile barabara ni ya TANROAD lakini kwa sababu mvua zimenyesha, tunamshukuru Mwenyezi Mungu ametuletea mvua, lakini barabara ile ni mbaya inapitika kwa shida. Kwa hiyo, naomba TANROAD ijitahidi kutengeneza zile barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Mpwapwa - Gulwe - Berege - Mima - Pufu tulikwishaomba Serikali, Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa haina uwezo wa kukarabati au kutengeneza hizi barabara. Kwa hiyo, ombi langu kwamba zile barabara basi naomba TANROAD wachukue ili waweze kuzitengeneza iwe chini ya TANROAD ile barabara iweze kukarabatiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni TASAF, ni chombo cha Serikali na TASAF inawasaidia sana Watanzania, Awamu ya Kwanza imejenga shule, zahanati Awamu ya Pili, sasa Awamu ya Tatu ni kusaidia kaya maskini, hivi karibuni tumetembelea miradi ya TASAF Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Mwanza. Tatizo wanaonufaika zaidi sio wale maskini, wanaonufaika zaidi ni Wenyeviti wa Mitaa, ndiyo wanachukua zile pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la kusikitisha sana kila Halmashauri ya Wilaya ina mratibu wa TASAF, kwa nini wasisimamie pesa hizi na kila bajeti tunatenga fedha kwa ajili ya TASAF, kila halmashauri. Kwa hiyo, naomba sana waratibu wa TASAF wasimamie hizi pesa zifanye kazi iliyokusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, MKURABITA tumetembelea Wilaya ya Magu, wananchi wengi hawana elimu, hawajapata elimu kuhusu MKURABITA, ndiyo maana tumekwenda pale wananchi wanalalamika kwamba kununua hati shilingi elfu thelathini na tano ni nyingi sana. Kwa hiyo, wengine wameshindwa mpaka sasa tumekuta hati zaidi ya mia tisa zipo pale hazijachukuliwa, wananchi wanachodai kwamba zile hati ukipeleka benki hawazitambui.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba sana wale waratibu wa MKURABITA kila Halmashauri wajitahidi sana kutoa elimu kwa ajili ya mradi huu. Miradi hii inasaidia sana, tunapata fedha za wafadhili, TASAF fedha za wafadhili na bajeti kidogo ya Serikali na MKURABITA. Zikitumika vibaya wale wanaotusaidia kuna siku watasema hapana tumepeleka hii fedha haikuweza kuleta maendeleo, mmeitumia vibaya, kwa hiyo sisi tunaondoa hii misaada; litakuwa ni tatizo kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, nakushukuru sana na naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.