Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa na nianze kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Waziri wetu wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Innocent Bashungwa, Katibu Mkuu Dkt. Faraji Mnyepe, Mkuu wa Majeshi Generali Jacob John Mkunda na Mnadhimu Mkuu wa Jeshi Luteni Jenerali Salim Haji Othman pamoja na Mkuu wa JKT Meja Jenerali Rajab Mabele na Makamanda wote nchi hii kwa kazi nzuri mnayofanya, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ni Amiri Jeshi Mkuu kwa jinsi alivyoipa kipaumbele sekta ya ulinzi kwenye Taifa letu. Tunamshukuru sana Rais wetu kwa hilo kwa sababu, tunaona hata bajeti ya Wizara ya Ulinzi imeongezeka kwa 6.9 percent. Hiyo inaonesha dhamiri njema ya Rais wetu kwenye kuboresha ulinzi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jeshi letu la Wananchi ni Jeshi imara sana na ni Jeshi bora, linaongozwa kwa misingi ya uzalendo, utii na nidhamu ya hali ya juu. Amani tunayoringia hapa nchini kama Watanzania inatokana na uimara wa Jeshi letu. Jeshi letu liko imara na sisi Watanzania tunafurahia sana uwepo wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama Taifa nchi yetu imeshafanya mambo mengi sana ambayo nitataja kwa haraka haraka mambo machache. Kwanza kabisa ilishiriki kwenye vita vya kukomboa Mataifa ya Kusini mwa Afrika. Pili, ikafundisha Majeshi ya Vyama vya Ukombozi katika nchi hizi ambazo tulizikomboa. Tatu, kikubwa kuliko vyote, tulimtandika nduli Iddi Amini na kumsambaratisha moja kwa moja, ile vita ilikuwa nzuri na ni nchi ambayo iliweza kuliondoa Jeshi la nchi nyingine madarakani moja kwa moja na kulisambaratisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile Jeshi letu limeshiriki katika operations mbalimbali hapa duniani kwenye kulinda amani, kikubwa pia, limeshiriki katika shughuli mbalimbali za kuokoa watu, kwa mfano, Mheshimiwa Waziri amesema juzi walikuwa huko Malawi, hapa nchini wala hatusemi. Kule kwangu Kilimanjaro walikuja wakazima ule moto kule mlimani, sisi tunawshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla Jeshi letu ni la Wananchi kwelikweli na siyo mchezo. Ukiangalia kona zote nilizotaja wanafanya mambo ambayo yanaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa katika mchango wangu leo nitajikita kwenye vijana wanaojiunga na JKT, wale wa kujitolea, kwa miaka miwili na wanapoondoka ni nini kinatokea, nitashauri ni nini kifanyike kama makamanda mtanisikiliza.

Mheshimiwa Spika, Jeshi letu la Kujenga Taifa lina lengo la kulea vijana wetu na wanawafundisha vitu vingi sana, ikiwepo umoja, uzalendo, mbinu za kuzalisha mali na mafunzo ya ulinzi, hawa vijana wamepatiwa hivyo vitu, vijana hawa huchaguliwa kwa kuangalia walivyofaulu, kwa mfano, kama wewe ni darasa la saba una cheti, unachaguliwa, wanaenda mpaka form six na ukishinda masuala ya ukakamavu unaingia Jeshini.

Mheshimiwa Spika, wanapoingia kambini vina wetu huwa wanafundishwa na makamanda ambao wamesoma, Jeshi letu lina wasomi wazuri sana kwenye sekta mbalimbali, wanafundishwa na watu wenye degree na diploma. Mafunzo wanayopata kule Jeshini yanakwenda kwenye ulinzi wa Taifa, uzalendo, kilimo, ufugaji, ujenzi, useremala, ufugaji nyuki, ufugaji mifugo na ujasiriamali kwa ujumla hata biashara wanafundishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa katika stadi nilizotaja hapo juu huwa zinatolewa kwa nadharia na vitendo kwa hiyo, hawa vijana wanafundishwa darasani na kwa vitendo na wakitoka pale wanakuwa wameiva vizuri kabisa, lakini baada ya mafunzo ya miaka miwili vijana wetu hawa hurudi uraiani, niwe mkweli, wengi wao huwa hawafanikiwi kuendelea, kwa mfano walivyokuwa kwenye kilimo hawaajiriwi kwenye sekta za kilimo, hawaendi kwenye sekta za mifugo na kwenye ajira za Serikali. Tunalishukuru sana Jeshi la Polisi, Magereza, Zimamoto, Uhamiaji na Jeshi la Wananchi Tanzania, huwachukua hawa vijana walio na cheti cha Jeshi na kuwapa kazi. Huwapa kipaumbele cha kuwaajiri, lakini wale waliosoma kilimo na vitu vingine haiwasaidii, haionekani inawasaidia mahali popote pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninafikiria sasa ni wakati ambapo jeshi letu lichukue ushauri wa kushirikiana na mamlaka zinazotoa vyeti vingine. Kwa mfano, nimeona Waziri amesema wana ushirikiano mzuri sana na Wizara ya Kilimo na Mifugo. Washirikianenao sasa watangeneze mitaala inayofaa iwe kwenye National Qualification Framework ili hawa vijana wanapotoka pale wanapofundishwa na Wanajeshi wetu ambao wamesoma, amefundishwa uzalendo yuko vizuri, apate diploma au cheti. Ni kitu kirahisi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule Jeshini kuna kitu ambacho kimeshatokea kwenye Kambi yetu ya Monduli, pale Arusha. Wanashirikiana vizuri sana na chuo cha, taasisi ya Accounts ya Arusha (Institute of Accounts Arusha) na wanatoa degree ya Shahada ya Kwanza ya Sayansi za Kijeshi, hapo wamefanikiwa. Sasa ninashauri JKT ibadilike tuwatafute hawa watu kama ni VETA, mtu wa darasa la saba apate cheti, kama ni mtu wa NACTE apate diploma, na kadhaika hata ikiwezekana degree wapate. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanapotoka hawa vijana wetu wakimaliza haya mafunzo ambayo nimeyataja kwenye hizi sekta ambazo wanawafundisha kule, wakiwa na cheti cha diploma au certificate au degree kutoka Jeshini, nakuhakikishia tutawapigania kama mpira wa kona kuwapa kazi. Kwa sababu watakuwa wamefundishwa ukakamavu, uzalendo na hakuna mtu atakayemkimbia mtu ambaye amepata mafunzo kupitia kwa hawa makamanda wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nihitimishe kwa kusema kwamba naomba hili jambo lipewe kipaumbele ili hii effort ambayo vijana wanatumia miaka miwili isiishie pale ambapo wamepata vile vyeti tu vya Jeshi, wapewe na hizi qualifications nyingine ili waweze kusaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)