Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa ili na mimi niweze kuchangia hii Taarifa ya Kamati ya Sheria Ndogo kama ambavyo imewasilishwa na Mwenyekiti na ni-declare kabisa mimi ni Mjumbe wa Kamati hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya utungaji wa sheria ndogo kama ambavyo Taarifa ya Mwenyekiti wa Kamati imezungumza na jinsi alivyobainisha, changamoto ya utungaji wa sheria ndogo katika Halmashauri; changamoto ya kwanza, zinatungwa sheria ambazo zinatofautiana, kwa mfano, viwango vya tozo na ushuru vinatofautiana kutoka Halmashauri moja kwenda Halmashauri nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ya sekta kama za mifugo, uvuvi, kilimo, zinatofautiana na kusababisha malalamiko makubwa kwa wananchi wanapoona kwamba wenzao wanatozwa kidogo na wao wanatozwa pakubwa. Kwa mfano katika katika uvuvi, ushuru wa samaki, maeneo mengine wanatoza ushuru wa shilingi 100 kwa kilo sehemu nyingine wanatoza shilingi 300 kwa kilo. Suala hili limekuwa likileta usumbufu mkubwa sana na kuwasababishia wananchi manung’uniko kila sehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la pili ni kuwepo kwa utitiri wa sheria ndogo nyingi mno. Kutokana na kuruhusiwa kila Halmashauri moja inatunga sheria zake, kila kijiji kimeruhusiwa kutunga sheria zake, kila manispaa imeruhusiwa kutunga sheria zake, matokeo yake tumekuwa na sheria nyingi kiasi kwamba tumeshindwa hata kuzisimamia. Tumekuwa na sheria ndogo nyingi mno kiasi kwamba hatuwezi kuzisimamia sheria hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwa mujibu wa Taarifa ya Auda’s Index pamoja na Taarifa ya JUTA Index of Subsidiary Legislations inaonesha kwamba tangu mwaka 1920 tumeshatunga sheria ndogo 41,051 ambapo sheria ndogo zinazofanya kazi mpaka sasa hivi ni 25,000, na kila mwaka tunatunga sheria ndogo zaidi ya 500. Sasa ukishakuwa na sheria ndogo nyingi namna hii huwezi tena kuzisimamia na zitaendelea kuleta madhara tu kwa wananchi kwa sababu haziwezi kuwa kwenye scope nzuri ya usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la tatu kwenye Halmashauri ni kuwepo kwa upungufu mkubwa wa wataalam, jambo ambalo linasababisha sasa zinatungwa sheria ambazo zina mapungufu makubwa, zinatungwa sheria ambazo zinaweka adhabu na faini kubwa kuliko hata zile zilizoko kwenye sheria mama, zinatungwa sheria ambazo zina masharti na makatazo ambayo ni kinyume na sera, makatazo ambayo ni kinyume na Katiba ya nchi yetu, zinatungwa sheria ambazo zinapeleka dhuluma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukishakuwa na utaratibu huu wa utungaji wa sheria unatuletea madhara makubwa sana katika Serikali yetu na malalamiko makubwa sana ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napendekeza kufanyike nini; kwa nini tusiachane na huu utaratibu wa kila halmashauri inatunga sheria yake, kila kijiji kinatunga sheria zake, kila halmashauri ya mji inatunga sheria yake, kila manispaa tukawa na sheria moja tu kwamba halmashauri zote ziongozwe na sheria ndogo itakayotungwa na Waziri na itumike kwa halmashauri zote, yaani uniform by-laws, kwa kuzingatia makundi yote manne ya halmashauri ambayo ni mamlaka za mji, mamlaka za wilaya, mamlaka za miji midogo, mamlaka za halmshauri za vijiji, tunaweza tukafanya hivyo na tukafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa bahati nzuri sheria inaturuhusu, Sheria ya Serikali za Mitaa, Sura 287 na Sura 288 zinampa Waziri mwenye dhamana ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kutunga kanuni ndogo ambazo zitakuwa ni uniform kwa maeneo yote ambayo niliyoyataja na kwa kufanya hivyo ni rahisi tu kwa sababu itatulazimisha kufanya amendment kwenye vifungu vya sheria hiyo ya Serikali za Mitaa, Sura ya 287 na Sura ya 288 katika vifungu vinavyozipa mamlaka hizo, Mamlaka za Miji, Mamlaka za Wilaya, Mamlaka za Miji Midogo na Mamlaka za Halmashauri za Vijiji kuziondolea yale mamlaka zilizopewa kwa mujibu wa sheria, kutunga sheria na badala yake akatunga tu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kutungwa kwa sheria ndogo nyingi zenye dosari, lakini zinaanza kutumika kabla hazijahakikiwa na Bunge, kabla Bunge halijafanya sehemu yake ya oversight function tayari hizi sheria zinaenda kutumika. Madhara yake ni nini zinapoenda kutumika?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwenyekiti wa Kamati amezungumza na mimi ninazungumza kwamba moja, wananchi wanaadhibiwa kwa makosa ambayo si yao. Sheria imetungwa na Serikali, inaenda kutekelezwa ikiwa na dosari, wananchi wanaonewa kwa mambo ambayo ni kinyume cha sera ya nchi, kwa mambo ambayo ni kinyume na sheria za nchi, kwa mambo ambayo ni kinyume na Katiba ya nchi, lakini yameruhusiwa. Imeenda kutungwa kule sheria na kwenda kuleta madhara makubwa sana kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa bahati mbaya hata inapokuja kutokea kwamba sheria ile ilikosewa, kinachofanyika ni sheria ndogo tu inarekebishwa, halafu madhara waliyoyapata wananchi hakuna anayefidia; mtu aliyesababisha kuingia kwenye matatizo hayo hawajibiki na wala hachukuliwi hatua yoyote. Jambo hili limekuwa likituletea matatizo makubwa sana, lakini pia ni kinyume pia hata ya Ibara ya 8(1)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inazungumzia ustawi wa watu.

Kwa hiyo, Serikali na Bunge haziwezi kuruhusu mambo yanayokinzana na ustawi wa nchi yanaenda kutungwa na kwenda kwa wananchi wakati yanakatazwa kwa mujibu wa Katiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tatu katika hili eneo ni Bunge kunyang’anywa mamlaka yake; kwa mujibu wa Katiba, Ibara ya 97(5) ambayo imetupa mamlaka ya kukasimu utungaji wa hizi sheria ndogo, umekuwa ukivunjwa mno sasa hivi na mamlaka tulizozikasimiwa kufanya hilo jukumu. Sasa kama zinavunjwa na wananchi wanaenda kutengenezewa mgogoro mkubwa na matatizo makubwa ni lazima kama Bunge hili tuone kwamba tusikubali tena mamlaka yetu hayo yakatumika vibaya. Wananchi wanajua Katiba imelipa mamlaka Bunge la Jamhuri ya Muungano kutunga sheria na hivyo mtu yeyote atakayetunga sheria ya aina yoyote ikaenda kutumika kwa wananchi, moja kwa moja limetunga Bunge. Sasa Bunge hili lijitoe katika hilo, lisikubali tena hizi sheria ndogo kutungwa na kuanza kutumika bila kufanyiwa uhakiki kwanza na Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, kuchelewa kufanyiwa marekebisho ya dosari; hata dosari hizo tunapozibaini tunakuja hapa tunaagiza zikafanyiwe marekebisho, zimekuwa zikichelewa mno na wananchi wanaendelea kupata matatizo makubwa katika kanuni hizo. Marekebisho hayafanywi, kwa mfano, tulifanya maamuzi katika kipindi cha Februari, 2023 ambapo mpaka sasa hivi dosari 19 katika kanuni 10 bado hazijafanyiwa marekebisho na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuweze kutoka katika jambo hili, nashauri kwamba tuziondoe changamoto nilizozitaja (a), (b) na (c); sasa napendekeza kila sheria ndogo inapotungwa na kutangazwa katika Gazeti la Serikali, isitumike kwanza hadi hapo Bunge hili litakapokuwa limefanya uhakiki wa sheria hizo na Bunge hili litafanya uhakiki wa sheria hizo kupitia Kamati ya Bunge ya Sheria Ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ninalotaka kuzungumza, Mwenyekiti wa Kamati amempongeza Mwanasheria Mkuu wa Serikali nami nampongeza na jambo moja ninalompongeza, hata ukimpigia simu saa saba za usiku anapokea na anakujibu. (Makofi)

Sasa suala la kujiuliza ni kwa nini Sheria Ndogo hizi zinatungwa, zinafanyiwa vetting na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, lakini zinaendelea kuwa na dosari kiasi hiki? Tatizo ni nini katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali? Tatizo ni sheria hizi zimekuwa nyingi wameshindwa kuzi-manage? Tatizo ni kwamba kuna upungufu wa fedha au wana upungufu wa watumishi au ni nini katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali? Mwanasheria Mkuu wa Serikali lazima atuambie ukweli juu ya jambo hili ili nchi hii isiendelee kupata matatizo inayoyapata hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu isikubali haya mambo yakaendelea kutokea na wananchi wetu wakaendelea kupata madhara makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba Bunge hili sasa lisiruhusu hizi kasoro ziendelee kutokea, wananchi wetu wakaendelea kutozwa tozo kubwa kuliko uhalisia, wananchi wetu wakaendelea kutozwa faini kubwa kuliko uhalisia, wananchi wetu wakaendelea kufukuzwa kwenye makazi yao bila sababu za msingi, wananchi wetu wakaendelea kutaifishiwa mifugo yao kinyume cha sheria na sera za nchi, wananchi wetu wakaendelea kutozwa kodi kubwa na tozo kubwa za maji, simu na mambo mengine kama umeme, unashtukia tu ghafla tozo na ushuru wa umeme umepandishwa na wananchi wanalazimishwa kulipa.

Mheshimiwa, Naibu Spika, haya yote yanafanyika kwa sababu ya Bunge hili kukasimu madaraka ya utungaji wa Sheria Ndogo kama Ibara ya 97(5) inavyosema, lakini eneo hili linatumika vibaya.

Sasa kupitia Bunge hili leo tukatae hayo kwa kuhakikisha kwamba hizo Sheria Ndogo ambazo zinatumika kama uchochoro wa kufanya dhuluma, wa kufanya uonevu kwa wananchi wetu kwa kisingizio cha kutunga Sheria Ndogo, sasa tukatae rasmi kupitia uchochoro huu kwa kukataza hizo sheria zote kupitia kule na matokeo yake ziletwe kwenye Kamati zetu ili tuzifanyie uhakiki kabla hazijenda kuumiza wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa na leo nashukuru nimemaliza yale niliyoandaa kusema. (Makofi)