Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hoja ya makadirio ya Wizara ya Ardhi. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa majaliwa yake kwetu sisi sote na Taifa letu kwa ujumla maana yeye ndiye anayewezesha haya yote na uwepo wetu sisi lakini na baraka zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kumwombea na kumshukuru sana Hayati Baba wa Taifa Mheshimiwa Julius Kambarage Nyerere ambaye Serikali yake ya Awamu ya Kwanza iliona jambo hili la ardhi ya Tanzania kuwa mali ya Serikali ya Tanzania kinyume na nchi zinazotuzunguka. Hii imefanya thamani ya ardhi yetu kuwa mali yetu kama Watanzania lakini pia kutokuwa na mkanganyiko wa muingiliano kwa kuwa umilikishwaji wake unatolewa kwa Watanzania kwa dhamana ambayo Serikali inayo ili sisi wote kama Watanzania tuwe wapangaji kwenye ardhi. Kwa sababu tunaona migogoro mingi na umilikaji unaotumika katika baadhi ya nchi ambao unamilikiwa na watu kutoka nje na wageni na unao leta mkanganyiko kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza pia Mheshimiwa Rais. Zipo kazi nyingi sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amejitahidi katika Serikali ya Awamu ya Sita na Serikali zote zilizopita kwa jinsi ambavyo nchi yetu inakwenda mbele na tunasonga mbele katika muundo wa Serikali, lakini kwa maendeleo na huduma kwa wananchi. Serikali ya Awamu ya Sita imefanya kazi kubwa sana. Hatutaweza kupata muda wa kutosha kuzungumzia jambo hili tukiwa humu, niwaombe Wabunge wenzangu wote tuwe wakalimani wa kwenda kuyazungumza hayo kwa wananchi na kutafsiri kwa wananchi wetu. Ushahidi kila Mbunge anao kwenye Jimbo lake na katika eneo lake kwa jinsi ambavyo Serikali imejitahidi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pongezi pia kwa Wizara, Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji kwa sababu tunajua mapungufu hayataisha, lakini tunaona hatua zinavyochukuliwa na tunavyojaribu kusonga mbele na kupata mafanikio kupitia Wizara hii. Zipo changamoto nyingi lakini kwa ujumla nchi haijengwi siku moja. Kwa nini nasema hivyo? Kwa sababu tunampongeza Waziri na timu yake na wale Mawaziri waliopita, Mbulu Mji tumepewa fedha za upimaji na umilikishwaji lakini kupima, kupanga na kumilikisha. Ni fedha ya maoteo inayotolewa na Serikali kwa ajili ya kuendeleza zoezi hili la upimaji wa mipango miji. Zoezi hili la upimaji mipango miji na fedha hizi hazina riba, ni fedha zinazotolewa na Serikali na baadaye tunarudisha bila riba, lakini imefanya tatizo kubwa la ujenzi holela wa miji yetu kupungua kwa sababu kadri tunavyopima tunaondoa mgogoro wa upimaji, lakini pia tunaondoa mgogoro ambao unazalishwa na kesi za muingiliano na kesi za kunyang’anyana ardhi baina ya wananchi na wananchi, ama taasisi; ama mtu na mtu hali ambayo inaifanya na kuipeleka mipango miji, lakini na umilikaji wa ardhi kuwa na hatua nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi zilipotolewa katika Halmashauri mbalimbali na Mbulu ikiwemo imekumbwa na changamoto nyingi sana na changamoto kubwa ni uhaba wa watumishi. Unakuta kwenye Halmashauri moja Afisa Ardhi ni mmoja, Afisa Mipango Miji ni mmoja lakini wanaohitajika kwenye zoezi zima wanaweza kufika kumi na ilipofika hapo halmashauri nyingi zilitafuta makampuni kwa njia ya tender ama kwa njia ya nukuu za bei, lakini zile kampuni zilizopatikana kwa namna moja au nyingine hazijatusaidia kwa jinsi inavyopasa na jinsi ambavyo manufaa na matokeo mazuri ya zoezi hili au ya fedha hizi zinapatikana katika halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano fedha nyingi zinakwenda kwenye ukodishaji wa vifaa, kulipa wataalam lakini pia na uandaaji wa mipango kitu ambacho kinafanya eneo hili la upimaji kukosa mafanikio makubwa. Rai yangu hapa ni kwamba pengine Serikali katika mipango yake ya mwaka huu na miaka inayokuja iangalie zile kada muhimu sana za ajira katika Wizara hii ya Ardhi ili utekelezaji wa Serikali ipate ufanisi na mafanikio zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu huu wa watumishi katika Sekta ya Ardhi unakwaza shughuli nyingi. Kwa hiyo, tusipouondoa ina maana huna rasilimali watumishi lakini pia na ufanisi unatarajiwa ili kufikiwa katika hatua inayofaa. Mara nyingi fedha hizi zinapotolewa elimu kwa wananchi ni ndogo sana kwa wale wanaosema upimaji umekuwa na gharama kubwa tatizo kwenye upimaji sikuona kwa upimaji ushirikishi kwa sababu gharama zinazotolewa kupima viwanja ni gharama zinazotekelezeka, tatizo kubwa ni uhamasishaji, tafsiri ya mwanzo kwa wananchi katika elimu kwa jinsi ambavyo tunataka eneo hilo liwe kwenye mipangoo miji na liweze kupimwa na kupatiwa michoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa sasa nataka kuishauri Serikali, twendeni kwa pamoja kama Wizara tuone utatuzi wa jambo hili unafanyika ili kuondoa matatizo makubwa kwa sababu tayari shule zilizopimwa, taasisi zingine zilizopimwa lakini pia maeneo ya miji yaliyopimwa yana dosari mbalimbali na kwa zoezi lolote lile linalofanyika lazima lifike muda tufanye tathmini na changamoto zilizoko na mafanikio yaliyopatikana ili zoezi lililotarajiwa liweze kufanikiwa na kupata mafanikio mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumza hivi kwa sababu fedha hizi kwa kadri zilivyotolewa kuna migogoro, unakuta Wilaya na Wilaya kuna migogoro, Mikoa na Mikoa kuna migogoro na Mkoa wa Manyara una migogoro ya ardhi kwa kiasi kikubwa sana hasa hasa hizi za mipaka ya maeneo ya utawala, lakini pia migogoro ya taasisi na taasisi lakini pia na migogoro ya mtu na mtu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali walitupa Baraza la Ardhi kule Dongobesh, lakini hata hivyo msaada wa lile baraza utapatikana na utatoa tija endapo ardhi hii itapimwa, lakini pia mipaka ya kila mmoja ikaainishwa na zoezi hili likafanikiwa ili kuondoa kesi nyingi na malalamiko mengi kwa wananchi.

Kwa hiyo, naiomba Serikali eneo la Mkoa wa Manyara, ukienda Wilaya ya Simanjiro ni migogoro isiyoisha. Nikupongeze Mheshimiwa Waziri na timu ya Mawaziri imeenda mara kadhaa, Wilaya ya Kiteto ni migogoro isiyoisha Wilaya ya Babati ni migogoro isiyoisha, Wilaya ya Mbulu ni migogoro isiyoisha. Niombe tathmini ya ile timu ifanyike, mrejeshio upelekwe kwa wananchi baadae, na tafsiri ya Sheria zitakazokuja baadae zitolewe kwa wananchi kwamba baada ya mapendekezo yaliyotolewa fikra za wananchi wale, mrejesho wa wananchi upatikane na tuweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze eneo la mabaraza ya ardhi; Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi Dongobesh Mheshimiwa Waziri anahudumia mabaraza mawili, kwa hiyo kesi nyingi huwa zinakwama pale Dongobesh kwa ajili ya kwamba anakuwa anahudumia Wilaya nyingine kule Ngorongoro na huku anahudumia Mbulu.

Nilikuwa naomba kwenye bajeti hii kama itawezekana baadhi ya mabaraza yaliyo anzishwa yapate Wenyeviti wake ili walau kupunguza msongamano wa kesi katika maeneo mengi na hili tuweze kupata manufaa ya wananchi kuhudumiwa kwa wakati, lakini pia kutokinung’unikia chombo hiki ambacho kinatarajiwa kutoa utatuzi wa matatizo hayo yaliyoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi sana yanahitaji kufanyiwa kazi katika sekta ya ardhi na kwa sababu hiyo eneo la Wizara hii tunaishukuru Serikali imeitengea fedha kwa yale mapungufu yanayoonekana basi Mheshimiwa Waziri mimi nikupongeze, lakini pengine Serikali ione kwa umuhimu fedha inazotenga kwenye Wizara hii ipeleke kwa kiasi kilichopendekezwa ili kutatua matatizo ya wananchi katika eneo hili la ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo mahususi yatolewe na Wizara kwenda kwenye Halmashauri zetu. Shule za msingi, taasisi za dini, shule za sekondari, na maeneo mengine na mipaka ya vijiji yakipewa kipaumbele ina maana tunaenda chini kwa kadri ambavyo kila eneo tunakwenda kupima na kuonesha mipaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna zoezi linalolalamikiwa kwenye KKK; zoezi la KKK limekumbwa na tatizo, mwanzoni wakati tunakwenda kwa wananchi tunasema tunakuja kupima, halafu tunakuja na umilikishwaji. Katika hatua ya umilikishwaji hatufiki tunaishia kupima na kuweka beacon, kampuni zile zinaondoka, zikiondoka maeneo yale yaliyowekwa alama yanabaki kukosa alama za kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilikuwa nashauri, kuliko kuchukua eneo kubwa la upimaji lenye kupigwa nondo bila beacon na ambalo halipewi hatimiliki, mimi nadhani ni muhimu tukapima eneo dogo tukakamilisha zoezi letu, lakini kwa tafsiri ya makubaliano ya pamoja kati ya Halmashauri zetu na wale wanopimiwa ili wapate hati na tujue zoezi la eneo hilo limekwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu zile kampuni zikiishaondoka unakuta zile beacon baada ya muda hazina alama kwa sababu ni nondo zilipigwa, alama zile zinafutika, awamu nyingine tunaenda tena kupima yale maeneo na zile kampuni kwenye usimamizi na maombi ya fedha zilishaomba kwamba watamaliza mchakato wote na kila aliyepimiwa atapewa hati ili fedha zile ziwe na tija na manufaa kwa wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumza suala la Mabaraza ya Ardhi; Mabaraza ya Ardhi katika meneo mengi yanakaa kwa muda mrefu. Swali langu kwa Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay na muda wako umekwisha.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie nashukuru sana na naunga hoja mkono kwa asilimia mia moja.