Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendeleo endelevu na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni “Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Serikali kwa kuanzisha mikopo inayotolewa kwa ajili ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha (KKK) ardhi. Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ni mnufaika wa programu hii na imekopeshwa shilingi 1,857,586,634. Mji Mdogo wa Mbalizi kumepimwa viwanja 35,000 kwa gharama ya shilingi 1,273,038,500 na Kijiji cha Mwashoma, Kitongoji cha Inolo vimepimwa viwanja 565 kwa gharama ya shilingi 584,548,134 na umefanyika kwa ufanisi mkubwa sana. Kutokana mahitaji makubwa na faida itayopatikana kwenye mauzo ya viwanja hivi, ipangiwe matumizi yanayolenga kuendeleza ardhi ikiwemo kuweka miundombinu kwenye maeneo yanayopimwa. Kutokana na mafanikio katika utekelezaji huu wa mwanzo, napendekeza Serikali iweke kipaumbele cha kuendeleza programu katika maeneo mengine hususani yanayolizunguka Jiji la Mbeya kutokana na mahitaji makubwa ya makazi yaliyopimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Serikali iendeleze programu hii katika vijiji vya Swaya; Lupeta; Nsenga; Ifiga; Nsongwi Mantanji; Nsongwi Juu; Izumbwe; Iwindi; Igoma; Ilembo; Idimi na Haporoto. Upimaji kwenye vijiji ambavyo ni vinakuwa haraka kuwa Miji (growing towns) utawezesha kupunguza na hata kuondoa kabisa makazi holela na pia kuongeza wigo wa walipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na programu ya makazi, Serikali iweke usimamizi wa matumizi bora ya ardhi ya kilimo ambayo inaendelea kupotea kwa matumizi ya makazi. Katika kupangilia matumizi mazuri ya ardhi, ihusishe Wizara za Kilimo, Wizara za Maji na Wizara inayosimamia mazingira. Kwa vile binadamu tunaongezeka ni muhimu kuhakikisha ulinzi kwa kuhifadhi ardhi inayofaa kwa kilimo na pia kutenga ardhi kwa ajili ya wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali kurejesha mahusiano mazuri kati ya TANAPA (Hifadhi ya Kitulo) na wananchi wa Kata za Ilungu, Igoma, Ulenje na Inyala suluhu haijapatikana. Serikali ichukue hatua pia za kumaliza mgogoro wa miaka mingi wa mpaka kati ya TFS na wananchi wa Kijiji cha Mwashoma. Wananchi wa Wilaya ya Mbeya wamekuwa walinzi wazuri wa hifadhi zetu na ni jukumu la Serikali kuhakisha uendelevu huu na kuondoa migogoro ambayo haina maslahi kwa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.