Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi - Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula na Naibu Waziri Mheshimiwa Geofrey Pinda, Katibu Mkuu - Ndugu Anthony Damian Sanga pamoja na wataalam wa Wizara kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia kuhusu umuhimu wa kupima ardhi yote hapa Tanzania, na migogoro ya umiliki ardhi katika jimbo langu la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa sehemu iliyopimwa na kupatiwa hati hapa Tanzania haijafikia asilimia 30. Hali hii imesababisha Taifa letu kushindwa kuweka mipango thabiti ya maendeleo katika maeneo mbalimbali, na kulinyima Taifa fedha ya kodi ya viwanja vilivyopimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupima ardhi ya Tanzania ni ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Jukumu hili hutekelezwa kupitia Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi (NLUPC).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali ilivyo sasa hivi kuna umuhimu wa hii tume kupiga kambi kwenye maeneo yote nchini na kusaidia kupima maeneo yote na kuyapatia hati. Watumishi wa tume hii watoke maofisini waende mashambani kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria za Ardhi upimaji wa mipaka ya vijiji ni lazima uwe shirikishi kwa kuwahusisha Halmashauri za Vijiji kwani wao ndio wasimamizi wa ardhi za vijiji. Ni muhimu sana kuwashirikisha ili kuondoa migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili zoezi la upimaji liwe na mafanikio, baada ya makubaliano ya mipaka, ni muhimu kuwekwe alama za kudumu (beacon) au zikatumika alama za kudumu kama vile maumbile ya asili ya kudumu ikiwemo mito au milima. Ni vyema kwenye kuweka kumbukumbu vizuri, muhtasari wa makubaliano yakawekwa kama kumbukumbu ili zitumike kama rejea ikiwa litajitokeza tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jimbo langu la Moshi Vijijini kuna migogoro ya umiliki wa ardhi baina ya wakulima na wafugaji katika Kata za Mabogini (Kijiji cha Mserekie) na Arusha Chini (Mikocheni na Chemchem) zilizoko maeneo ya tambarare.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro hii imeshasababisha madhara makubwa ikiwemo vifo na uharibifu mkubwa wa mali kama mazao ya wakulima. Mpaka sasa Serikali ya Wilaya na Mkoa haijaweza kupambana na changamoto hii, kwani tatizo hili linajirudia mara kwa mara. Migogoro ya wakulima na wafugaji jimboni kwangu inasababishwa na uhaba unaoendelea kukua wa rasilimali ardhi. Kutokana na hali hii, wakulima wamekuwa wanafungua mashamba kwenye maeneo ya wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro hii kwa kiasi kikubwa husababishwa na yafuatayo; kwanza, Serikali haijayapima maeneo ya wafugaji na wakulima na kuyamilikisha kwa wahusika kwa kutoa hati za kimila na za Serikali.

Pili, kubadilika kwa tabia nchi kunakopelekea malisho kukauka na kusababisha uhaba wa chakula cha mifugo na kuwafanya wafugaji kulisha mifugo yao kwenye mashamba ya wakulima; na tatu, kupanuka kwa shughuli za kilimo na makazi ya watu ambapo maeneo ya ufugaji yamepungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto hii ninaishauri Serikali kama ifuatavyo:-

a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri fedha za ndani za Serikali na zile za mikopo kutoka nje zitumike vizuri kuwezesha Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi (NLUPC) kukamilisha jukumu lake la kupima ardhi yote ya Tanzania. Idadi kubwa iende kazini na si kwenye makongamano, mafunzo na semina.

b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na migogoro inayoendelea jimboni kwangu, kuna umuhimu wa Serikali kuingilia jambo hili na kuhakikisha kuwa maeneo husika yamepimwa na kumilikishwa rasmi kwa wahusika. Pa kuanzia Serikali iharakishe zoezi hili kwa kutumia mifumo ya hati za kimila zinazotambuliwa kisheria na baadaye wapewe hati za Serikali za kumiliki ardhi.

c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mazingira ya Kitanzania, ninaishauri Serikali ipitie sera za umiliki wa ardhi zenye utata zinazoweza kuchochea migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji. Sera nzuri na rafiki itasaidia kutoa haki bila malalamiko.

d) Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishauri Serikali, Wizara za sekta husika (Ardhi, Kilimo na Mifugo na Uvuvi) zishiriki kikamilifu kwenye zoezi hili, na kila Wizara itenge bajeti ya kusaidia kupima ardhi na kushughulikia changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.