Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, kwa kupata nafasi ya kuchangia Hotuba ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Utawala Bora. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais na Serikali yake kwa kazi nzuri wanayoifanya, Watanzania tuko nyuma yenu, tunawaunga mkono na Mheshimiwa Rais, Wabunge wa CCM tunakuunga mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo mawili, matatu ya kuchangia kama ushauri, lakini mwisho kuna haja ya kuendelea kuwaeleza ndugu zetu namna ya kuendesha nchi yetu tofauti na wanavyozungumza wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Halmashauri yangu ya Uyui ni Halmashauri mpya, ambayo tumekuwa tukiomba pesa kwa sababu ya ujenzi wa Halmashauri yetu, tuna miaka mingi pesa hazijafika, tunaomba Serikali ituangalie tuweze kumaliza ujenzi wa Halmashauri yetu. Kujenga jengo la utawala, tuna ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, tunaomba Serikali katika bajeti ya mwaka huu ituangalie tuweze kukamilisha hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tuna maombi ya kupata Halmashauri mpya ya Igalula, kutoka katika Halmashauri yetu iliyopo ya sasa, haya ni maombi ya muda mrefu, tunaomba pia liangaliwe tuweze kupata Halmashauri yetu ya Igalula.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Vitongoji. Wenyeviti hawa wanafanya kazi kubwa sana, ni kiungo muhimu sana katika utendaji wa shughuli zetu katika maeneo yetu. Ni wasimamizi wa maendeleo katika maeneo yetu. Miaka mingi wemekuwa wanasahaulika hawa pamoja na kazi kubwa wanayoifanya, tunaomba Halmashauri zetu ziangalie namna ya kuwalipa posho zao. Vilevile posho zenyewe ni ndogo, tunaomba tuangalie uwezekano wa kuziagiza Halmashauri zitenge hizi pesa, na ziwafikie Wenyeviti wetu wa vitongoji na vijiji. Posho zenyewe ni shilingi 10,000, naomba ikiwezekana tuwaongeze posho hizo, ikiwezekana tutengeneze utaratibu pia wa kuwapatia posho Wajumbe wa Serikali za Vijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia maendeleo katika maeneo yetu, pesa kubwa, pesa nyingi zinakwenda kwenye Serikali za Vijiji, utekelezaji wa miradi mingi ya maendeleo unafanyika katika Serikali zetu za Vijiji. Hawa watu wasipoangaliwa, wasipojaliwa maslahi yao, utendaji wao wa kazi utakuwa ni mdogo, na uwajibikaji utakuwa ni mdogo, tunaomba tuliangalie sana hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna Watendaji wa Vijiji na Watendaji wa Kata, watendaji wa vijiji na Kata hatujaangalia maslahi yao vizuri, Watendaji wa Vijiji wa Kata wanafanya kazi katika mazingira magumu sana. Hawana usafiri, maeneo yao ya kazi ni makubwa, wanapata taabu sana kufanya kazi hizo katika maeneo ya vijijini. Ushauri wangu Serikali iangalie uwezekano wa kuwapatia usafiri hata wa pikipiki, ili waweze kutimiza wajibu wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watendaji wa Vijiji ndiyo wanajenga sekondari, ndiyo wanajenga zahanati, wanajenga nyumba za walimu, lakini Watendaji wa Vijiji wanakaa nyumba za kupanga. Tuone uwezekano pia wa Serikali kupata kuwajengea nyumba Watendaji wa Vijiji, na Watendaji wa Kata. Maslahi yao pia bado ni madogo, Serikali ione uwezekano wa kuwaongezea maslahi yao watendaji wetu wa Vijiji na wa Kata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumzia suala la Halmashauri yetu ya sasa ya Uyui kwa maana Iskizia, tulikuwa tunapata pesa kwa sababu ya kuendeleza Halmashauri yetu mpya. Lakini mpaka sasa hatuna nyumba za wafanyakazi pale Isikizya kiasi kinawafanya wafanyakazi wetu waishi mbali na makao makuu ya Halmashauri yetu. Tumejengewa nyumba za shirika la nyumba pale wanaziita nyumba za low cost housing, lakini ukiziangalia nyumba zile gharama yake moja ni shilingi milioni 52, wafanyakazi wetu hawana uwezo wa kuzinunua. Halmashauri yetu haina uwezo wa kuzinunua. Tunaomba Serikali ione namna ya kutusaidia ili wafanyakazi wetu wa Halmashauri ya Tabora kwa maana ya Uyui, waweze kukaa karibu na eneo la kazi ili waweze kuwa na ufanisi mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tarafa ya Kizengi ilitangazwa muda mrefu, karibu miaka mitatu, minne iliyopita. Pamoja na kutangaza Tarafa yetu ya Kizengi mpaka sasa haijaanza kazi rasmi, hatuna Afisa Tarafa na hili naomba liangaliwe sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamezungumzia kuhusu asilimia kumi inayotengwa kwa sababu ya vijana na akina mama. Tunaomba kujua hili suala ni la kisheria au ni kwamba Halmashauri ikiamua inatenga au laa. Maeneo mengi hizi pesa hazitengwi, maeneo mengi vijana hawanufaiki na hizi asilimia tano na akina mama katika maeneo yetu. Tunaomba Halmashauri zote ziagizwe ni lazima zitenge hizi asilimia tano kwa sababu ya kuwasaidia vijana na asilimia tano kuwasaidia akina mama na ufuatiliaji wake uwekewe utaratibu mzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mengi lakini kwa sababu ya muda, nijikite kwenye masuala mawili, matatu ya mwisho. Unapozungumzia demokrasia kuna mambo mengi ndani yake, Wazungu wanasema charity begins at home. Kuna msemo mmoja sungura alikuwa na hamu ya ndizi, alivyozikosa zile ndizi akaanza kuimba sizitaki mbichi hizi, wenzetu wanazungumzia demokrasia kwamba katika chama chetu hakuna demokrasia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapotaka kutoa uchafu kwenye jicho la mwenzako angalia uchafu kwenye jicho lako kwanza. Kuna Wabunge wamepata Ubunge wakiwa wako CCM, lakini leo wapo CHADEMA; wapo watu ambao wamekitumikia chama kile kwa muda mrefu, wamekuja kuingia kwenye dirisha dogo juzi. Sasa demokrasia hiyo, ukiangalia wao na sisi nani ana demokrasia?
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia hotuba ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusiana na TAMISEMI; amezunguzia suala la kuonekana kwenye tv, anayezungumza anazungumza kuhusu kuonekana kwenye tv. Mimi nataka niseme, unaposema kwamba wananchi hawapati fursa lakini…
TAARIFA...
MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakataa taarifa yake. Yeye amelelewa ndani ya Chama cha Mapinduzi ndiyo maana leo tuko naye hapa. Mimi nimechaguliwa na wananchi kwa kura za kutosha.
MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilinde muda wangu. Mimi nimechaguliwa na wapigakura kwa kura zaidi ya 38,000, mgombea wa CHADEMA alipata kura 4,000. Kwa hiyo nimekuja Bungeni kwa nguvu ya wapigakura wangu na mtoto wa simba ni simba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani kuhusu Utawala Bora na amezungumzia kuhusu watumishi hewa. Naomba ni-quote ukurasa wa tisa, anasema; “Mheshimiwa Spika, sababu kubwa ya kushindwa kutatuliwa kwa tatizo la watumishi hewa ni kukosekana kwa uadilifu katika mfumo mzima wa utumishi wa umma. Watumishi hewa ni tatizo la kutengenezwa kwa makusudi.”
Mheshimiwa Mwenyekit, kwa bahati mbaya sana aliyekuwa Katibu Mkuu wa Utumishi ndiye alikuwa anasoma hotuba ya Upinzani. Nadhani anajua siri kubwa sana ya watumishi hewa. Mheshimiwa Magufuli atusaidie kuangalia namna ya waliotengeneza watumishi hewa, inawezekana na wengine tuko nao humu ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili ni la kuliangalia sana maana unapomnyooshea mwenzako kidole kimoja vitatu vinaweza vikawa vinakuangalia wewe mwenyewe. Kuna haja kabisa Mheshimiwa Rais aangalie namna anavyotumbua majipu haya na macho mengine yaangalie humu ndani, inawezekana kabisa wakatusaidia katika kuweka mambo haya sawa sawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nataka niseme haya kwa kifupi, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.