Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Rahim kwa kuturuzuku uhai na kutujalia afya ya kukutana leo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua nafasi hii kukushukuru kunipa nafasi ya kuchangia katika hotuba ya bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Nshirikiano wa Afrika Mashariki. Nichukue hatua hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa Diplomat Number One kwa kuimarisha sauti ya Tanzania katika medani ya uhusiano wa Kikanda na Kimataifa pia kwa msukumo mkubwa aliouweka katika diplomasia ya uchumi na matunda ya juhudi hizo yako dhahiri kwetu sote. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza diplomat number two Mheshimiwa Dkt. Stergomena Lawrence Tax, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa umahiri alioudhihirisha katika kuendeleza na kuimarisha diplomasia ya Tanzania, leo kwa hotuba yake ya kwanza katika Bunge hili aliyoitoa kwa ustadi na umahiri mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja naye nawapongeza Naibu Waziri Mheshimiwa Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk, Katibu Mkuu Balozi Dkt. Samwel William Shelukindo, Naibu Katibu Mkuu Balozi Tatma Mohammed Rajab na watumishi wote wa Wizara kwa kazi nzuri mnayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo mawili ambayo na mimi ningependa niongeze sauti yangu na Wizara imeyafanya vizuri sana. Moja ni eneo la diaspora na la pili ni eneo kuhusu diplomasia ya utamaduni (cultural diplomacy) ikiwa ni sehemu na nguzo muhimu ya diplomasia ya uchumi (economic diplomacy). Hapa nikiazima maneno ya Prof. Ali Mazrui, diplomasia ya utamaduni itatupa soft power ambayo yeye aliita Parks Tanzaniana akituweka katika kundi moja na Parks Americana na Parks Britannica.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Uhusiano wa Afrika Mashariki kwa kuanzisha hii digital hub ya kuwaandikisha diaspora. Hatua hiyo ni hatua muhimu sana ya kuwasajili diaspora wote wa Tanzania walioko nje ili tuweze kujua wako wapi, wanafanya nini na kujua mchango wanaoweza kuutoa katika maendeleo ya uchumi na kijamii ya nchi yetu, hiyo itaiwezesha Serikali kuwa na mkakati wa kushirikisha diaspora ya Tanzania katika maendelo ya uchumi na jamii ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalisema hili mimi mwenyewe nikiwa na uzoefu kwa kuwa nimeishi Ujerumani kwa miaka tisa, siku sita na siku tatu. Kwa hiyo hii hatua ni muhimu na ninaipongeza sana na niwashukuru washiriki wote ambao wamewezesha Wizara kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naipongeza Wizara kwa kuwa katika hatua za mwisho za maandalizi ya kuwapatia hadhi maalumu watu wenye asili na nasaba ya Tanzania ambao wameacha kuwa raia wa Tanzania baada ya kuchukua uraia wa nchi nyingine. Hiyo itakuwa ni hatua muhimu ya kuondoa usumbufu na changamoto za watu hawa wanazozipata hasa wanaporejea nyumbani kuja kuona ndugu zao au kufanya shughuli nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la hadhi maalumu ndilo lenye muafaka hapa Tanzania, nami nasema ni bora kama wanavyosema waswahili ni bora kenda mkononi kuliko kumi porini. Sasa tuna kenda mkononi ambayo ni hadhi maalumu. Mimi ningeomba Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje pia Wizara ya Mambo ya Ndani ikamilishe jambo hili ili hawa wenzetu waweze kupata hadhi maalumu waondokane na usumbufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni bora kuliko lile ambalo tunaendelea kulisema na tunajua bado halina muafaka, suala la uraia pacha bado halina muafaka hapa nchini lakini halina muafaka duniani, kwa hiyo tushikilie hili ambalo tuna muafaka nalo tulisukume kwa haraka ili liende. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti nilioufanya huko duniani ni asilimia 49 tu ya nchi duniani zinaruhusu uraia pacha na asilimia 51 duniani hazirihuisu uraia pacha. Utaona asilimia 51 bado haziruhusu uraia pacha, maana yake jambo hili hata katika ngazi ya dunia bado halijapata muafaka. Hii ni pamoja na nchi ambazo tuna uhusiano nao wa karibu ambapo wako Watanzania wenye asili ya nasaba ya Tanzania bara, asili ya nasaba ya Tanzania Zanzibar ambao wako Oman. Oman hairuhusu uraia pacha, Saudi Arabia hairuhusu uraia pacha, lakini pia ziko nchi ambazo zina diaspora wengi sana duniani ambazo pia haziruhusu uraia pacha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri ni India, ina diaspora wengi sana nje lakini katika Katiba yake imekataza kabisa uraia pacha lakini imekuja na hadhi maalumu kuwatambua watu wanaowaita Persons of India Origin au Overseas Indians ambao wanapewa kitambulisho na wanakuwa na haki zote. Nchi nyingine ya kiafrika ambayo ina diaspora wengi sana duniani Ethiopia, ina diaspora karibuni milioni tatu Marekani na Ulaya na yenyewe pia haikubali uraia pacha, lakini inatoa kitambulisho maalumu kwa waethiopia waliokuwa nje, ambao wakirudi nchini kwao Ethiopia wanakuwa na haki zote ambazo wanazihitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika nchi za Umoja wa Ulaya. (Europian Union). Nchi 15 zinakubali uraia pacha, nchi 12 hazikubali uraia pacha na ambazo hazikubali uraia pacha ni pamoja na Ujerumani, Uholanzi, Austria na Denmark. Kwa upande wa Ujerumani, wao hata mtoto aliyezaliwa Ujerumani na watu ambao siyo raia wa Ujerumani hapewi hadhi yoyote, ndiyo maana baadhi ya sisi ambao watoto wetu wamezaliwa Ujerumani tuliporudi hapa walivyofikisha miaka 18 tulipoambiwa twende Ubalozini kuomba wakane uraia wa Ujerumani, Wajerumani walishangaa kwa sababu toka walipozaliwa wao hawakuwa raia wa nchi hiyo, kwa sababu kwa Wajerumani uraia ni damu. Aina yao ya uraia ni Jus Sanguinis ni uraia wa damu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hapa Tanzania suala la uraia pacha lina hisia kali, it is an emotive issue. Katika utafiti nilioufanya nimeona kwamba Bunge Oktoba Mwaka 1960 wakati tuna Serikali ya Madaraka, uliletwa Muswada Bungeni kuhusu uraia wa Tanganyika na aliyekuwa Waziri Kiongozi wa wakati huo au Chief Minister Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na hiyo iliwekwa kwenye Hansard katika suala la uraia, lilileta msuguano mkubwa na hasa baada ya kuwa mwaka 1958 Waingereza walipotupa masharti ya uchaguzi wa kura tatu. Kila Jimbo liwe lina Mbunge Mzungu, Muafrika na Muasia na kundi kubwa la vijana wa TANU, kujitoa TANU na kuunda Chama Cha African National Congress of Tanganyika wakisema Tanganyika ni kwa Waafrika tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu aliyasema haya Tarehe 28 Oktoba Mwaka 1961 katika Hansard na naomba nimnukuu na ndiyo msingi wa kwa nini uraia pacha Tanzania haukukubalika wakati huo. “Now Sir, what we are trying to do, we are establishing a citizenship of Tanganyika, what is going to be the best of this citizenship of Tanganyika. We, the Government kwa sababu alikuwa Chief Minister, elected by the people of Tanganyika say loyalty to the country is going to be the basis of determining the citizenship of Tanganyika. In order to be certain as far as human responsible to be certain, the citizens of Tanganyika are going to be loyal to Tanganyika and Tanganyika only. We have said although other countries do accept it, we are not going to accept dual citizenship in Tanganyika” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ni maneno ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere akiwa Waziri Kiongozi katika Bunge la Tanganyika, Bunge la Madaraka tukijiandaa kupata uhuru wa nchi yetu.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Prof. Palamagamba Kabudi.

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)