Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mheshimiwa Dkt. Stergomena Tax na Naibu wake Mheshimiwa Balozi Mbarouk Nassor Mbaroruk na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya na mchango wangu utajikita kwenye suala la uraia pacha hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Watanzania wenzetu ambao wamezaliwa hapa nchini wakiwa na uraia wa asili wa kuzaliwa hapa Tanzania. Wenzetu hawa wengi waliondoka wakiwa watu wazima na uraia wetu wa kuzaliwa kwenda nje ya nchi na kupata uraia wa nchi nyingine kama sharti la kupata ajira huko ughaibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiuhalisia tukitafakari kwa undani, hawa ndugu zetu waliomba uraia wa nchi hizo kwa sababu za kiuchumi na ustawi wao wa kijamii na hii haiondoi ukweli kwamba wao ni Watanzania kwa kuzaliwa na kwa damu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria yetu ya Tanzania hairuhusu uraia pacha. Mtanzania akishapata uraia wa nchi nyingine, moja kwa moja sheria yetu inamnyang'anya uraia wa Tanzania. Baada ya kuukosa uraia wa Tanzania, miongoni mwa haki wanazozikosa nchini walikozaliwa ni pamoja na kutokuwa na haki ya kumiliki ardhi na kutokuchagua viongozi wala kushiriki kugombea nafasi ya umma katika uchaguzi nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uraia wa Tanzania unaongozwa na Sheria ya Uraia Sura ya 357 Toleo la mwaka 2002 ambapo Serikali hairuhusu uraia pacha kwa watu wazima isipokuwa kwa watoto wenye umri chini ya miaka 18 ambao wanakuwa na uraia wa Tanzania na uraia wa nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kumekuwa na kilio cha kuomba uraia pacha kutoka kwa wenzetu waliozaliwa Tanzania kiasili na kupata uraia wa nchi nyingine, wakati sasa umewadia kwa Serikali yetu kuangalia muswada huo wa sheria na kuruhusu uraia pacha nchini kwa kuyaangalia maslahi mapana ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia, inafaa uraia pacha utolewe kwa wale ambao walizaliwa Tanzania na kupata uraia wa nchi nyingine. Tumeona sehemu zilizoruhusu uraia pacha kwenye baadhi ya nchi kumewezesha kupata viongozi wa juu wanaoongoza mataifa makubwa na mfano mzuri ni Waziri Mkuu wa Uingereza Rishi Sunak ambaye ana asili ya Taifa la India.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uraia pacha utaruhusu yafuatayo; kwanza Watanzania wanaoishi nje ya nchi watapata haki za kumiliki mali na ardhi, kufanya biashara, kupata huduma za afya, na kushiriki katika shughuli za kisiasa; pili, itawawezesha diaspora kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kijamii na kiutamaduni ya nchi yao. Diaspora hawa huko waliko tayari wameshasaidia kudumisha na kukuza utambulisho wa Kitanzania; na tatu uraia pacha utawawezesha Watanzania wenzetu kushiriki kikamilifu na kuleta miradi ya maendeleo ya jamii, elimu, afya na mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, diaspora inayokuwa na uraia pacha inaweza kuleta ujuzi, maarifa na mtaji wa kiuchumi kutoka nchi wanazoishi kuja Tanzania. Hii inaweza kusaidia katika kukuza sekta mbalimbali za uchumi kama vile viwanda, kilimo, utalii na huduma za kitaalamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, raia kutoka nchi jirani za Afrika Mashariki kama vile Kenya, Rwanda na Uganda zimeruhusu uraia pacha. Ni vyema ikiipendeza Serikali yetu kujifunza kutoka kwa majirani zetu na kuchukua hatua stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, kuna umuhimu wa kuangalia sheria yetu ya uraia wa Tanzania na ikiipendeza Serikali ifanye mabadiliko ya sheria ili kuruhusu kuwezesha uraia pacha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.