Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Dr. Stergomena Lawrence Tax

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda nikushukuru kwa mara nyingine tena kwa kunipa nafasi hii ili niweze kutoa ufafanuzi na kufanya majumuisho ya mjadala ambao umeendelea asubuhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukupongeza kwa kuongoza na kusimamia mjadala wa bajeti yetu kwa umakini na umahiri mkubwa. Aidha, naishukuru Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa ushauri na miongozo waliyotupa kufuatia hotuba niliyoiwasilisha. Nawashukuru sana pia Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yenu mizuri sana. Tumeipokea michango yote na yotwe tutaifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niwashukuru sana, sana kwa pongezi mahususi mlizozitoa kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya na yenye tija katika kuimarisha Uhusiano wa Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi na ambazo mmezitoa kwetu sisi wasaidizi wake. Napenda kulihakikishia Bunge lako tukufu na Waheshimiwa Wabunge kuwa sisi wasaidizi wake katika Wizara tutaendelea kumsaidia ipasavyo na kutekeleza majukumu yetu kwa uaminifu, uadilifu na umahiri kadri ya uwezo wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwatambue na kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja niliyoitoa leo asubuhi na tumepokea maoni na ushauri na hoja kutoka kwa wajumbe 13 ambao wamechangia wote kwa kauli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya hoja hizo ambazo Waheshimiwa Wabunge na pia Kamati imezitoa zimejibiwa kwa ufasaha na Mheshimiwa Naibu Waziri wangu Mheshimiwa Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na kutokana na ufinyu wa muda, nitajitahidi kujibu baadhi ya hoja lakini tu niwahakikishie kwamba hoja zote zitajibiwa kwa maandishi. Wamechangia Waheshimiwa Wabunge 13 ikiwa ni pamoja na Kamati, lakini michango imekuwa mingi sana na mizuri, tunawashukuru, tutaijibu yote kimaandishi. Kwa hiyo, naomba sasa nijielekeze katika kutoa ufafanuzi katika baadhi ya hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hoja ya Mheshimiwa Kingu ambaye amesisitiza kwamba tuhakikishe tunaishirikisha Zanzibar kikamilifu. Naomba nikuhakikishie kwamba hili linafanyika na huu ndiyo msisitizo ambao tumepata muda wote kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wanaokumbuka wakati nikiapishwa, alisisitiza vitu vitatu na kimoja kilikuwa ni kuzingatia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inatambua pande zote mbili za Muungano. Kwa hiyo, sio mimi tu, Wizara kwa ujumla hili tunalifahamu na tunalitekeleza asilimia 100 ikiwa ni pamoja na uwekezaji katika maeneo mbalimbali. Katika misafara yote tunahakikisha tunajumulisha pande zote mbili za Muungano, katika majadiliano yote tunahakikisha tunafanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa nimetoa ufafanuzi kwenye hoja hiyo hoja, nyingine ambayo imejadiliwa kwa hisia na kwa msisitizo mkubwa ni kuhusu utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi. Hii imeongelewa na Kamati na Waheshimiwa Wabunge wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Diplomasia ya Uchumi, nianze kusema tu kwamba ni kitu mtambuka. Watekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi ni sekta zote na ni katika Sekta ya Umma na Sekta Binafsi. Kwa hiyo, mpaka sasa mafanikio yamekuwepo makubwa kama nilivyosema kwenye hotuba yangu katika utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi. Pia tumebaini kama mlivyosema wenyewe kwamba uelewa kuhusu Diplomasia ya Uchumi bado ni mdogo. Tunakiri hilo. Kwa kulitambua hilo na kwa msisitizo mkubwa ambao umewekwa na Kamati yetu ya Bunge ya NUU, tumeanza maandalizi ya kutekeleza mpango mkakati wa utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi. Mpango huu utatoa tafsiri, nini Diplomasia ya Uchumi? Mpango huu utaainisha wadau wote katika utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaposema wadau wote ni katika sekta zote; Sekta ya Umma, Sekta Binafsi, lakini katika Sekta ya Umma ninatambua kwamba tunakwenda mpaka chini. Tunakwenda mpaka TAMISEMI, tunaihusisha mikoa na Wilaya, na utaainisha majukumu na pia tutaweka mpango wa ufuatiliaji kujua inatekelezwa namna gani? Kwa sababu kulikuwa na hoja, kwamba tuwawekee malengo Balozi zetu. Wao pia watakuwa ni sehemu ya utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mtuunge mkono tukamilishe kazi hii ambayo tumejipangia kuikamilisha mwishoni mwa mwaka huu kama ambavyo pia Kamati imesema tukamilishe mwisho wa mwaka wa fedha ujao, lakini sisi lengo letu ni kukamilisha kufikia Desemba mwaka huu 2023. Kwa hiyo, baada ya kuwa tumekamilisha hili, basi tutaweka bayana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba pia ieleweke kwamba sisi kama Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kazi yetu ni kuratibu, watekelezaji ni sekta zote. Nimesikia hoja kwamba tuweke dirisha Wizarani la kufuatilia utekelezaji. Tukishamaliza mpango huu, tutajua kila mmoja anajukumu gani na mmoja atatakiwa kutekeleza mahali pake. Kwa hiyo, sisi kama Wizara, kazi yetu itakuwa ni kufuatilia tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili linakwenda pamoja na hoja kwamba tuweke wataalamu mahususi kwenye maeneo muhimu katika Balozi zetu. Tutaweza kulifanya hilo baada ya ya kukamilisha huu mkakati. Kwa sababu mkakati huu pia unalenga kujua katika nchi mbalimbali tunalenga nini? Tukishajua tunalenga nini kule, tutajua pia tunaweka wataalamu wa aina gani? Kwa hiyo, tuvute Subira, tutaendelea kufanya hivyo, lakini siyo kwamba hatupeleki wataalamu, tunapeleka wataalamu hata sasa ambao ni wataalam mahususi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imeongelewa kwa mkazo ni kuhusu Sera ya Mambo ya Nje kuikamilisha. Hili naomba tu niwahakikishie kwa kujiamini kabisa kwamba sera hii tunaikamilisha ndani ya mwaka huu wa fedha. Tuko mbali sana, tunajua umuhimu wake, Kamati imetusukuma kweli kweli na sisi tumesukumika, kwa hiyo, tunaahidi kwamba sera hii sasa itakuwa tayari. Imechukua muda kidogo kwa sababu mwanzo tulidhani kwamba tunaandaa sera mpya, lakini kadri tulivyoendelea tukabaini kwamba hatuna haja ya sera mpya. Iliyopo misingi yake inakidhi, tunachotakiwa sasa ni kuweka maeneo mapya ambayo yanapungua kama nilivyoyaainisha kwenye hotuba yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imejitokeza kwa sana ni suala la Hadhi Maalum na Uraia Pacha. Nashukuru wachangiaji na nimefurahi kwamba alichokisema Mheshimiwa Prof. Kabudi kimejitokeza hata kwenye mijadala yetu kwamba bado hili suala halijawa na muafaka wa pamoja, siyo nchini kwetu tu, lakini hata nchi za nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kwa kutambua umuhimu wa kuhakikisha kwamba Diaspora ambao wapo nje ya nchi ambao ni raia na wale wenye asili, tuna definitions mbili za Diaspora kama zilivyotolewa, wote wanapata haki, kwa hiyo, akatoa msisitizo kwamba tufanye mchakato wa kutoa Hadhi Maalum. Pamoja na kwamba Katiba yetu inasema nini, lakini msingi ni kuhakikisha kwamba wote wanapata fursa tunazoweza kuziandaa katika Hadhi Maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi nyingine, Mheshimiwa Prof. Kabudi ametoa takwimu kama ni nchi 49 tu zinazotoa Uraia Pacha. Sasa ukitoa Uraia Pacha kwa sasa hivi wakati hakujawa na muafaka kitaifa na kidunia, kuna wale watakaokosa fursa, kwa sababu kwenye nchi ambazo Diaspora zipo na zile nchi hazitambui Uraia Pacha, sisi tukitoa Uraia Pacha, wale hawatapata fursa ambazo tunatarajia kuzitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili kuweza kutoa fursa kwa wote, Mheshimiwa Rais kwa busara yake akahimiza kwamba tutoe hii Hadhi Maalum, tena kwa haraka. Huu mchakato Waheshimiwa Wabunge umefika mbali sana, kufikia mwisho wa mwaka huu hii Hadhi Maalum itakuwa imetolewa. Inatoa fursa nyingi tu. Walileta mapendekezo kumi, mapendekezo yote hayo tumeyazingatia na yote yataingizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mchango wa Mheshimiwa Prof. Kitila, bahati mbaya katika yale mapendekezo hakukuwa na pendekezo la Haki ya Kimungu. Kwa hiyo, tutaenda kuliangalia hilo pendekezo la Haki ya Kimungu linaingia namna gani, lakini siyo miongoni mwa mapendekezo yaliyoletwa na Diaspora. Diaspora wanachotaka ni kuweza kuingia nchini, kumiliki ardhi, kupata huduma kwenye taasisi za fedha na kadhalika na yote hayo yamezingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kabla sijamalizia hoja hii, napenda sana kuzishukuru Taasisi zinazotusaidia. Tumepongezwa hapa kuhusu mfumo wa kuandikisha Diaspora wetu kidigitali. Tumefanya kazi hii na sekta binafsi ikiwa ni pamoja na CRDB, NMB na NSSF. wanafanya hivyo kwa uzalendo wao, lakini kwa kujua kwamba na wenyewe ni wanufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fursa tunazoziongelea ni pamoja na huduma mbalimbali. Kwa hiyo, diaspora anapojiandikisha katika mfumo huu, watapata fursa za kiuchumi na kijamii, watapata fursa za ajira na pia watapata fursa zinazotolewa na taasisi mbalimbali ikiwa ni pamoja na hata Uhamiaji. Kwa hiyo, nihamasishe diaspora wetu waweze kujiandikisha na kutumia huu mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine iliyoongelewa ni suala la majengo kwamba Balozi zetu ziko katika hali mbaya. Ni kweli lakini hapa suala wala siyo kukosekana kwa fedha kutoka Hazina. Maana yake nisije nikarudi Hazina Mheshimiwa Mwigulu akaninyima pesa, akasema wewe umeenda kusema pesa hazitoki wakati na upungufu pia uko kwako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumebaini kwamba tulikuwa hatuko tayari. Ndiyo maana Kamati imesisitiza kwamba tuhakikishe taratibu zinakamilika mapema na maombi ya pesa yanapelekwa mapema. Hilo niwahakikishie Kamati tutalifanya, lakini pesa ya Serikali haitoshi. Ndiyo maana tumeandaa huu mpango ambao nimeueleza katika hotuba yangu kwamba tuna mpango wa kushirikisha sekta binafsi. Tumeshaainisha miradi yote ya kipaumbele, tumeshaainisha changamoto zote, tumeshaainisha mfumo tutakaotumia na tumeshaainisha jinsi ya kutatua hizo changamoto. Habari njema ni kwamba tayari miradi miwili tumeanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hatua kubwa sana kwamba NSSF wanashirikiana na sisi katika kujenga kitega uchumi chetu na Ubalozi wetu Nairobi, na sasa tuko katika hatua za mwisho pia waanze kufanya Kinshasa, lakini wapo hata na wabia waliotoka nje ya nchi ambao tuko katika mazungumzo nao. Kwa hiyo, tuna imani kwamba hili sasa linaenda kufanyika. Naomba tu mtuunge mkono na mtutafutie hao wabia ambao wako tayari kuja kufanya kazi na sisi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona muda wangu umeisha. Kulikuwa na hoja ya kutotumia fursa zitokanazo na ushirikiano wa kikanda, tunalipokea tunalifanyia kazi na tumeendelea kulifanyia kazi. Misaada ya asasi kutoka sekta zisizo za kiserikali tuiangalie, tumeipokea; ajira nchi za nje, Mheshimiwa Naibu Waziri amelitolea maelezo; ajira katika Mashirika ya Kimataifa, tunafanya kazi, siyo kwamba halifanyiwi kazi, ila labda tuongeze juhudi, kwa sababu hapa kuna changamoto za ndani, za nje na kuna za uelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Neema kwa kusisitiza kwamba yako maeneo ambayo hata kama tunatoa Hadhi Maalum na Uraia Pacha ni maeneo mabayo lazima kama nchi tuyalinde. Nakushukuru sana kwa msisitizo huo. Chuo cha Diplomasia tumepokea. Kuhusu vikwazo kwa wafanyabiashara, kweli ni tatizo na tunavifanyia kazi. Hapa kulikuwa na tatizo kubwa ambapo wafanyabiashara wetu walikuwa wamenyimwa vibali ili watoe mahindi Zambia ambalo limechukua muda mrefu, lakini napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba sasa suala hili limetatuliwa na wafanyabiashara hawa wamepewa vibali siku ya leo. Kwa hiyo, tutaendelea. Haziwezi kwisha. Katika ushirikiano wa kimataifa na kikanda, vikwazo vinakuwepo. Kinachotakiwa ni kwamba muda wote kuwa macho na kushirikiana na wale wenzenu na kuhakikisha kwamba vikwazo hivyo vinatatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuhitimisha, naomba niseme kwamba baadhi ya mambo ambayo yamesisitizwa hapa ni mambo ambayo yanafanyiwa kazi katika Kamati iliyoundwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, baada ya kuwa ameshazibaini changamoto mbalimbali zinazoikwaza Wizara yetu. Kamati hii isichukuliwe kwamba inapima utendaji wa Wizara kama utendaji wa Wizara kwa maana ya watumishi, inaangalia picha kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi haya mliyosema ya Diplomasia ya Uchumi, mambo mliyosema kwamba ni aina gani ya watumishi tuwe nao, mambo gani tujipange, tunajipanga namna gani, dunia ya sasa inakwenda namna gani? Twende namna gani? yote yataangaliwa katika kazi inayofanywa na hii Kamati. Kwa hiyo, ni matumaini yangu kwamba Kamati hii itakapomaliza kazi yake, basi tutakuwa tumepata suluhu ya mambo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa nitoe hoja. (Makofi)

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.