Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, kama ulivyosema asubuhi, muda mrefu sikuwa hapa Bungeni kwa sababu nilikuwa na kesi ya uchaguzi. Namshukuru Mwenyezi Mungu amenirejesha Bungeni salama na nawashukuru wananchi wangu wa Rombo kwa kuniunga mkono wakati wote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sikuwepo, iko michango mingi sana ambayo ilitolewa hapa Bungeni tangu wakati wa kuchangia mpango na kadhalika, basi kama nitarudia kwenye eneo ambalo wenzangu waliligusa naomba ionekane tu kwamba nami nataka niweke rekodi katika mambo yaliyotokea katika Bunge hili.
Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ambalo ningependa nilizungumze ni ujumbe ambao nimetumwa na wapiga kura wangu na baadhi ya viongozi hasa viongozi wa dini tuliokutana kwenye mazishi, akaniomba nikifika Bungeni niuseme, nao ni kuhusu matangazo haya kutokwenda hewani kama ilivyokuwa zamani. Wamenituma niseme ifuatavyo: kwamba Bunge kuna kujichanganya kwa hali ya juu ambapo watu wanahoji, Bunge hili lina wasomi au sote tumegeuka kuwa vilaza? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wanasema hivi, mwanzoni ilisemekana Bunge ndilo linalohusika na kuzuia matangazo, lakini kadri siku zilivyokuwa zinakwenda, Serikali imejitokeza kuwa msemaji wa Bunge. Sasa wanashangaa, ni Bunge au ni Serikali? Katika Serikali kuwa msemaji wa jambo ambalo wanasema linahusu Bunge, Waziri wa Habari anasema kwamba hili linatokana na gharama, lakini Waziri Mkuu anasema ni ili wananchi wafanye kazi.
Mheshimiwa Spika, sasa wananchi wanajiuliza, hivi hii Serikali ni moja? Mambo yanaamuliwa kwenye Baraza la Mawaziri au mnaamulia kwenye chai? Kwa hiyo, wananchi wanataka kujua, jambo hili hatma yake ni nini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nami nataka niwaambie kuna faida kubwa ya kukaa nje ya Bunge, Mbunge wakati Bunge linaendelea.
Mheshimiwa Spika, nataka niishauri Serikali, msifikiri jambo hili linawaletea umaarufu, linawachanganya kweli kweli kwa sababu wananchi walichoshikilia ni kwamba mnazuia wananchi wasione kile ambacho wanapaswa kuona kwa sababu mnaogopa kukosolewa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nami ninachokiona ni kwamba yako mambo Bungeni hapa yanafanyika mazuri na Wapinzani, yanafanyika mazuri na upande mwingine, ni kwa sababu gani mnakataa wananchi wasipate haki yao ya kuona nini kinachoendelea? Kama sasa hivi katika bajeti hii, wananchi wanauliza, wao wanalipa kodi; Bunge hili la bajeti ndilo linalogawa mafungu ya zile kodi zao, kwa nini mnawakimbiza kulipa kodi lakini wasiwe na haki ya kuangalia ile kodi yao inavyogawanywa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni muhimu tuseme ili ibaki kwenye rekodi, kwa sababu tumekuwa tukiwashauri, lakini hamtaki kupokea ushauri, nitoe mfano wa ushauri ambao tumekuwa tukiwapa. Tarehe 27 Mei, 2015 katika Bunge hili Mheshimiwa Esther Matiko alishika shilingi katika Wizara hii kuhusu boti ya Dar es Salaam Bagamoyo.
Mheshimiwa Spika, alichosema Mheshimiwa Esther wakati ule ndicho CAG ambacho sasa hivi ame-confirm kwamba boti ile ilikuwa chini ya kiwango, kwamba gharama za kununua boti ile zilikuwa kubwa. Sasa sisi hatushauri kwa maslahi yetu, tunashauri kwa maslahi ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, umezuka mtindo katika Bunge hili Wizara ya Uchukuzi ikiguswa kwa sababu, Rais alikuwa Waziri hapa, kuna hisia za kuzuwiazuwia Wizara hii watu wasiseme maneno! Hatusemi kwamba, Rais akiwa Waziri alifanya ufisadi, inawezekana ni Katibu Mkuu, inawezekana ni watu wake! Na sisi tunamwambia kwa sababu, ya umahiri wake wa kutumbua atumbue hawa ambao walihusika katika kuharibu fedha za wananchi. Hili ni jambo ambalo kila mtu mwenye akili na anayeipenda nchi ataniunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ukitoka huko nenda kwenye barabara zetu. Mheshimiwa SavelinMwijage amezungumza hivi hakuna mtu anayeiona barabara ya Chalinze – Vigwaza mpaka Mlandizi? Hii barabara Mawaziri wanapita, Rais anapita na kila mtu anapita! Hivi haiingii kwenye fikra kwamba, hapa ni ufisadi umefanyika? Hapa ni wizi umefanyika? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa haya yanazuiwa na yanapozuiwa mnafikiri kwamba, ni kusaidia Serikali, hapana! Serikali inaumizwa kwa kiasi kikubwa sana. Ujenzi wetu wa barabara lazima uangaliwe, kuna ufisadi na wizi mwingi sana unatokea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna barabara ya kutoka Mwika – Mkuu kwenda mpaka Tarakea, Jimboni kwangu; ile barabara haina miaka mitatu, leo kuna mashimo! Sasa hivi tumeanza viraka, ni nini kimetokea? Feeder roads hazijatengenezwa! Kuna eneo moja linaitwa Mengwe, Keni na Mkuu; zile feeder roads tuta la barabara liko juu mtu anapanda na pikipiki kule haoni gari linapita kule! Matokeo yake watu wanauawa kila siku!
Mheshimiwa Spika, nilisema mwaka jana na mwaka huu nasema tena! Isifikiriwe kwamba, Serikali itapendwa kwa kuambiwa halafu haitekelezi! Ninyi mmeficha wananchi wasitusikie, sisi haya tunakwenda kuwaambia! (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, barabara ile ilijengwa na Wakandarasi wawili. Mkandarasi wa kwanza alipeleka vifaa akaviweka kwenye eneo la kiwanja cha michezo cha watoto wa shule pale Mengwe, mpaka leo hii miaka 10, matingatinga yako pale! Magari yanaozea pale! Watoto hawana mahali pa kuchezea! Tumeshahangaika kila mahali yale yaondolewe, hayaondolewi! Sasa mimi sijui Serikali ya Hapa Kazi Tu ningefikiria kwamba, haya mambo ambayo yamelalamikiwa miaka iliyopita ndio ingeyachukua sasa iyafanyie kazi.
Mheshimiwa Spika, kuna eneo katika barabara hiyo, wamejenga mto unapita juu ya barabara, Kikelelwa kule! Sasa hivi hapa jinsi mvua zilivyonyesha, maji yote yanaenda kwenye majumba ya watu. Watu wanateseka! Tumesema na tunaendelea kusema. Sasa huwezi hata siku moja ukawaridhisha wananchi wakati kero zao hazishughulikiwi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, najua muda unaniishia, lakini niseme sisi tumepata mafuriko mwaka huu kule Rombo. Kati ya mtandao wa barabara za Halmashauri, kilometa 285, kilometa 167.7 zimebomoka zote. Fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara za Halmashauri katika bajeti ya 2015/2016 mpaka robo tatu ya mwaka wa fedha tulikuwa hatujapata hata shilingi moja! Naiomba Serikali ituletee hizo fedha kwa sababu, sasa hivi wananchi katika vijiji vyote, katika Kata zote hakuna jinsi, barabara zimevunjika na kwa hiyo, wanategemea sana wapate fedha hizi ili waweze kurekebisha barabara maisha ya wananchi yaende kama ambavyo wanataka yawe.
Mheshimiwa Spika, la mwisho, yapo maeneo korofi maana maendeleo yakija yanakuja na tabu zake; yapo maeneo korofi ambayo tulishaomba yawekewe matuta. Kwa mfano, kuna eneo moja linaitwa Mamsera, juzi nimerekodi mtu wa 22 kuuawa kwa sababu ya speed kubwa.
Mheshimiwa Spika, nimekwenda TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro mara chungu nzima, Baraza la Madiwani, Halmashauri iliyopita na hii ya sasa hivi wamekwenda wameomba jamani pale pawekwe matuta watu wanakufa! Hivi ndiyo niseme kwamba, Serikali inapenda kusikia watu wake wanauawa?
Mheshimiwa Spika, juzi uso kwa macho, nimeona mweyewe mtu wa 22 ameuawa! Eneo la Tarakea, eneo la Kikelelwa, eneo la Keni, ni maeneo ambayo ni korofi! Mimi ni mmoja kati ya watu ambao tunapinga matuta, lakini wakati mwingine lazima tuyaombe kwa sababu ya wakorofi wachache. Naomba sana Waziri awaagize watu wa TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro waweke matuta eneo la Mamsera, eneo la Keni, eneo la Holili na eneo la Tarakea.
Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, moja kati ya vitu vinavyochangia hizi barabara kuharibika, niliwaambia yapo magari yanabeba pozzolana kutoka Holili na mengine yanabeba mizigo mizito yanapita kwenye ile barabara inakwenda Kenya, wekeni mizani hata ya kamba! Ni leo, ni kesho, ni leo, ni kesho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali ya Awamu ya Nne imekwenda imekuja sasa Serikali ya Hapa Kazi Tu, wekeni basi hiyo mizani! Huu nao ni ushauri tunawasaidia kwa sababu, ile barabara inavunjika. Barabara zinatengenezwa kwa pesa nyingi, lakini wakorofi wachache wanasababisha zivunjike. Sasa tuseme namna gani, ili mtuelewe? Maana tukisema kwa kutetea rasilimali hamuelewi! Tukisema kwa kelele mnasema sisi tunapayuka, tunapiga kelele.
Mheshimiwa Spika, naomba sana kwamba, haya niliyoyasema Wizara iyafanyie kazi. Nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa.