Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Awali ya yote nianze kwa kumpongeza sana kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna alivyoamua kutoa mwelekeo wa jinsi anavyotaka sekta hii ifanye kazi, lakini namna anavyotaka Watanzania wanufaike na sekta hii ya uhifadhi, lakini pamoja na utalii kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda nitakwenda haraka kwenye maeneo matatu. Eneo la kwanza, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu yote ya Wizara na taasisi zao zote kwa kupata imani ya Mheshimiwa Rais kuendelea kuongoza Wizara hii. Mheshimiwa Waziri nimesema nimpongeze kwa sababu, yako mambo mawili nataka kumshauri yeye na wenzake kwenye Wizara.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza Mheshimiwa Waziri, nimekupongeza ili nikushauri. Pamoja na kuwa Waziri wa Wizara hii, Wizara hii ni muhimu, taasisi za uhifadhi zinafanya kazi kubwa na kazi nzuri. Nakuomba usiwe Waziri tu, ukawe baba na ukawe mlezi wa Wizara hii. Ukawe baba na ukawe mlezi wa watumishi wa sekta na taasisi zote zinazosimamiwa na Wizara yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ninalotaka kumshauri Mheshimiwa Waziri, kwa miaka kadhaa tumekuwa na changamoto kidogo kwenye Wizara hii. Kila ukija uongozi yanakuja mambo mapya, zinakuja kauli mpya, inakuja mikakati mipya; nakuomba kwenye awamu yako uache alama. Katengeneze mifumo ya uhakika itakayoweza kufanya kazi kwenye Wizara hii, hasa kwenye eneo la sekta ya utalii ili utalii uweze kufanya vizuri ulete matokeo kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ninalotaka kulizungumza ni kuhusu wanyama wakali na waharibifu. Changamoto hii ni kubwa sana na iko kwenye maeneo mengi. Ni changamoto ambayo inawatesa na kuwaumiza sana wananchi wetu, malalamiko na manung’uniko ya wananchi yamekuwa makubwa. Ukienda Korogwe, zaidi ya kata nane tembo wanaharibu mazao ya wananchi, tembo wanaua na wanaharibu mali za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natambua, nathamini na kupongeza juhudi kubwa inayofanywa na Serikali. Imefanyika kazi kubwa sana kuanzisha vituo vya Askari, kuongeza Askari wa Doria, kununua magari, kununua pikipiki, lakini kubwa sana ni utayari wa Serikali kuendelea kulipa kifuta machozi kwa wananchi wetu. Mambo haya ni makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo haya ambayo Serikali imefanya, bado tatizo hili ni kubwa, lazima kama nchi na Serikali mjue yako mambo lazima tuendelee kuyafanya. Jambo la kwanza nishauri, Wizara hii iwe serious kwenye shughuli ya kuongoa shoroba zetu. Pili, mapitio ya Wanyama, mapito ya wanyama yaweze kutambulika vizuri na yasilete madhara kwa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili. Tujifunze kwenye nchi nyingine teknolojia mbalimbali za namna ya kukabiliana na hali hii ili tuwasaidie wananchi wafanye kazi zao kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, Mheshimiwa Waziri amesema, moja ya changamoto na sababu kubwa ya changamoto hii ni ongezeko kubwa la watu na ongezeko kubwa la shughuli za kibinadamu. Kwa mujibu wa Taarifa za Sensa, mwaka 2022 tulikuwa na watu milioni 44 na ukiangalia idadi ya watu mwaka 2022 ukilinganisha na sensa ya mwisho 2002 nyuma yake, ongezeko lilikuwa ni la asilimia 2.7. Sensa ya mwaka 2022 tumefika Watanzania milioni 61,741,000 na wastani wa ongezeko la watu kwa mwaka kwa mujibu wa Taarifa za Sensa ni asilimia 3.2. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ongezeko hili siyo dogo. Unaweza kutumia ongezeko hili kuvuta picha ya miaka 10 inayokuja hali itakuwaje? Miaka 20 inayokuja hali itakuwaje? Tukiendelea kupiga kelele hapa bila kuweka mikakati madhubuti hatuwezi kumaliza jambo hili.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali; Wizara ya Ardhi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Kilimo tukae pamoja tuweke mpango wa kupanga nchi hii. Haiwezekani tukalima kila mahali, haiwezekani tukachunga kila mahali, haiwezekani tukajenga kila mahali, lazima tuje na mkakati wa Kitaifa wa kupanga nchi yetu ili mambo haya yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho ninalotaka kuchangia siku ya leo ni zoezi la kuhamisha watu kwa hiyari kutoka kwenye Hifadhi, Eneo la Ngorongoro. Nakushukuru Mheshimiwa Waziri amelisema vizuri kwenye hotuba yake na ametoa tamko kwamba halijasitishwa na hakuna mabadiliko yoyote. Ninamshukuru sana na ninampongeza kwa jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka mwezi Novemba mwaka 2022 na kwenye Taarifa ya Kamati tumesema, kaya ambazo zilikuwa zimeshahama ni 489, watu 2,629 na mifugo 14,000, lakini tunapozungumza tangu wakati huo wa Novemba, tayari kuna kaya 1,524 zimejiandikisha na ziko tayari kuhama ambazo hizi kaya zina watu 8,715. Hizi kaya zina mifugo 32,842 pamoja na tamko ambalo amelitoa Mheshimiwa Waziri. Nafurahi kwamba nachangia wakati Waziri Mkuu, ambaye ndio Mtendaji Mkuu wa shughuli za Serikali akiwa ndani ya ukumbi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anasema jambo hili halijasimama na hakuna mabadiliko, lakini tangu tumemaliza awamu ya kwanza ya kuhamisha watu kutoka Ngorongoro ni miezi sita. Mlikuja kwenye Kamati mwezi wa Pili na mwezi wa Tatu mkasema mna mipango ya kutafuta fedha. Tumekaa miezi sita, fedha hazijapatikana? Kwa nini zoezi hilo haliendelei? Sawa ametuambia kwamba jambo hili lipo na halijabadilika, lakini haiwezekani kwa zoezi kubwa, kwa zoezi muhimu kama hili ambalo Bunge hili tulilibariki, nchi hii imelikubali, inakwenda kuiokoa na kulinusuru eneo la Hifadhi ya Ngorongoro tukakaa miezi sita tunasubiri. Tunasubiri nini miezi sita? Hizi kaya zaidi ya 1,000 zipo tayari zinasubiri. Zinasubiri kwa muda gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inawezekana jambo hili likawa siyo la maliasili peke yake. Nimesema nimefurahi kwa sababu Waziri Mkuu yupo. Tunapokwenda kuhitimisha bajeti hii ya maliasili Serikali ituambie. Pamoja na kauli kwamba kazi hii inaendelea na jambo hili halijabadilika, mtuambie tumekwama wapi? Ni kwa nini jambo hili haliendi mbele? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, athari ya jambo hili ni kwamba likipoa, yanaanza mambo mengine ya ajabu ajabu. Mmeona watu wamekwenda mpaka Ulaya kuanza kushitaki, wameanza kulalamika, tumerudishwa nyuma. Inawezekana labda kuna mtu anataka kuhujumu hili zoezi. Kama hakuna mtu anataka kuhujumu suala la kuhamisha watu Ngorongoro tukiwa tunahitimisha bajeti hii, Wizara, Serikali kwa ujumla mtuambie. Msituambie tu maneno kama zoezi linaendelea, mtuambie mmefika wapi? Kama kuna changamoto, ni nini? Tunataka kuona zoezi hili likikamilika ili tuendelee na hatua nyingine za mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)