Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara yetu hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa anayoifanya katika sekta mbalimbali hapa nchini pamoja na sekta yetu hii ya maliasili na utalii. Lakini niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu nzima, kwa kazi kubwa na dhamira nzuri mliyo nayo katika kuiboresha sekta hii ya maliasili na utalii hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais, kwenye hili suala la The Royal Tour, limekuwa na mafanikio makubwa katika nchi yetu. Na moja kubwa ni kuitangaza nchi yetu kimataifa, la pili kuongeza idadi ya watalii hapa nchini na la tatu ni kuongeza fedha za kigeni katika uchumi wa Taifa letu. Kwa hiyo ni pongezi kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi hii kubwa iliyofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2025 pamoja na Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano (2021/22 – 2025/26) yako malengo ambayo tulijiwekea. Moja ni idadi ya watalii kufikia milioni tano kwa mwaka; la pili, mchango wa sekta hii ya utalii kuwa asilimia 15.5 kwenye Pato la Taifa; tatu sekta hii kuchangia asilimia 27 ya mapato yote ya kigeni. Ili kuyafikia malengo haya lazima kazi kubwa ifanyike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na la kwanza mimi napendekeza, ni kuongeza vitanda kwa ajili ya watalii. Katika eneo hili ni kushirikisha sekta binafsi. Kwa taarifa ya mwaka 2022, Tanzania tuna vitanda 132,684 lakini nchi jirani ya Kenya ina vitanda 1,200,000. Kwa hiyo kuna kazi ya kufanya katika eneo hili kuongeza vitanda kwa kushirikisha sekta binafsi, kujenga hoteli za nyota mbalimbali ili kuhakikisha kwamba tuna vitanda vya kutosha kwa ajili ya watalii wanafika katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili katika eneo hili ni kuboresha miundombinu yetu kwenye masuala mazima ya utalii. Jambo la tatu ni kuboresha huduma (customer care) kwa watalii wetu. Jambo la nne utakumbuka wakati tulivyogawa fedha za UVIKO-19 sekta hii ya utalii tuliipa bilioni 90.2. Kazi ilifanyika nzuri sana na Kamati yangu ya Bajeti ilipata ziara katika maeneo mbalimbali, tumeona mafanikio makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napendekeza kwenye dirisha hili la ECF ambalo lilikuwa na nia ya kupunguza matatizo ya urari wa malipo kwa nchi zetu basi Serikali itenge fedha pia kwa sekta hii ya maliasili na utalii ili kuboresha sekta nzima ya utalii ambayo inachangia katika uchumi wetu vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuendeleza na kumaliza migogoro mbalimbali kati ya hifadhi na maeneo yetu mbalimbali hapa nchini. Katika eneo hili niendelee kuipongeza Serikali kwa sababu kazi kubwa imefanyika. Iko timu ya mawaziri nane ambayo imezunguka katika nchi yetu, wamefanya kazi kubwa, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna baadhi ya maeneo yetu bado kuna migogoro. Nitatoa mfano wa Jimbo langu la Babati Vijijini; kuna Vijiji nane ambavyo vinapakaa na Hifadhi nzuri sana ya Tarangire; Vijiji vya Gedabung’, Ayamango, Gedamar, Mwada, Sarame, Sangaiwe na Vilimavitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kuna dhamira nzuri sana ya Mheshimiwa Waziri ya kumaliza migogoro hii. Tumesikia hotuba yake, ameongea masuala mazuri sana. Mheshimiwa Waziri, twende kama timu pamoja, liko jukumu la kwangu kama Mbunge na wananchi wangu, liko jukumu la Serikali, twende kwa pamoja tukamalize miigogoro hii ya muda mrefu ili kuwe na uhusiano wa ujirani mwema kati ya hifadhi na wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Mheshimiwa Waziri umejipanga vizuri, nami nakuhakikishia kabisa ntakuunga mkono katika suala zima la kumaliza migogoro katika maeneo haya yote ya Babati Vijijini ili wananchi waendelee kuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la kifuta jasho wananchi wanapoharibiwa mazao na wanyama wakali. Tunaipongeza Serikali kwanza kwa kuwakumbuka wananchi, walau hata kwa hicho kidogo wanachokipata. Lakini kifuta jasho kinachelewa, hakiji kwa wakati. Kwa hiyo tuombe sana Serikali basi kile kifuta jasho kije kwa wakati lakini pia walau kiakisi ule uhalisia wa uharibifu uliofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana katika eneo hili kuwe na tathmini ya uhakika ili wananchi wapate walau kifuta jasho kitakachosaidia familia zao na kisaidie uchumi katika maeneo hayo. Pia viwango vifanyiwe mapitio, ni vya muda mrefu. Kwa hiyo niishauri Wizara iangalie namna ya kupitia viwango hivi vya fidia kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, otherwise nashukuru sana kwa kupata nafasi hii, na mimi naiunga mkono hoja hii kabisa, na Mheshimiwa Waziri nakutakia kila la heri katika mafanikio yako. Ahsante sana. (Makofi)