Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi basi niweze kuchangia na kutoa ushauri wangu kwenye sekta hii muhimu ya Maliasi na Utalii, sekta ambayo ni muhimu sana kwa nchi yetu Tanzania, lakini pia kwa Mkoa wangu wa Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ni muhimu sana kwa kutuingizia fedha za kigeni. Tumeona zaidi ya asilimia 25 ya fedha za kigeni zinatokana na sekta hii lakini pia asilimia 17 ya Pato la Taifa inachagiwa na sekta hii muhimu ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile inachangia kwa kaisi kikubwa ajira kwa Watanzania. Na mpaka sasa tumeona ajira za moja kwa moja na ajira zisizo rasmi takribani milioni 1.6 za Watanzania wameajiriwa kwenye sekta hii muhimu. Utaona kabisa mnyororo wa sekta hii ya utalii ni mrefu sana na unagusa sekta mbalimbali kama za usafirishaji, kilimo na nyingine. Sekta hii inachangia pia kukuza sekta mbalimbali kama nilivyozitaja, kwa hiyo ni muhimu sana Serikali ikatilia mkazi kwenye sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyojua sasa hivi kwenye uchumi wa mataifa kuna changamoto kubwa za fedha za kigeni, na Tanzania pia tuna changamoto hiyo ikiwemo upatikanaji wa dola. Lakini Serikali ikiweza kutilia mkazo kwenye sekta hii muhimu ya utalii itaweza kutatua changamoto hii kwa kiasi kikubwa. Naamini kabisa tukiweza kuilea na kuiendeleza sekta hii hata kwenye uchangiaji wa dola tunaweza tukafikisha takriban asilimia 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba nimpongeze sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kuendelea kutangaza sekta hii ya utalii kimataifa. Lakini naiomba Wizara iweze kufanya kazi zaidi ili basi iendane na kasi hii ya Mheshimiwa Rais wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuondokane na utalii wa kimazoea, twende sasa kwenye utalii wa kimkakati. Tukiweza kufanya hivi, tutaweza kushirikisha sekta binafsi ili tuweze kushirikiana nao katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali, lakini vilevile hususan kwenye ujenzi wa hoteli zenye hadhi ya kitaifa ya kulaza wageni wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa hivi nchi yetu tuna vyumba 122,532 tu, lakini ukiangalia nchi jirani wana vyumba zaidi ya milioni mbili. Ukiangalia pia nchi nyingine ambazo zimeendelea kwenye sekta hii kama Seychelles, Mauritius na hata iwe nchi jirani ya Kenya hawakuanza tu hivihivi, waliondokana kwenye utalii wa mazoea, wakaenda kwenye utalii wa kimkakati. Walianzisha programu mahususi, programu za kimkakati kwa ajili ya kuendeleza hoteli nchini mwao. Strategic Hotel Investment Programmes lazima zianzishwe ili tuweze kuondokana na changamoto hii. Kwa hiyo ushauri wangu kwenye eneo hili la hoteli, hata sisi itabidi tuanzishe fedha mahsusi na za kimkakati ili basi tuweze kuondokana na changamoto hii ya hoteli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ninalotaka kuchangia jioni ya leo ni kuhusiana na kodi na tozo sumbufu kwenye sekta hii ya utali. Kwanza kabisa nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa tamko lake la kusamehe kodi kwa wafanyabiashara wetu ambazo zimezidi miaka mitano. Na nitumie fursa hii kwa niaba ya wafanyabiashara wa Mkoa wa Arusha kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa tamko lake hili. Sasa, niombe mamlaka husika zote ziweze kufuata maagizo haya ili basi wafanyabiashara wetu wasiwe na usumbufu kwenye biashara zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwenye sekta hii ya utalii utaona kwamba kuna tozo mbalimbali ambazo ni kero sana kwa wafanyabiashara wetu ambao wanahusika moja kwa moja na biashara hii ya utalii. Ukiangalia biashara zile mpya zote, kijana leo anahitimu shule akitaja kujiajiri kwenye sekta hii ya utalii ni lazima alipie leseni dola 50 ili aweze kufanya kazi za u-tour guide. Mbona kazi nyingine hazitakiwi kukatiwa leseni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba sana Wizara iangalie kodi zote na tozo mbalimbali ambao ni kero kwa wafanyabiashara wetu ili waweze kwenda vizuri na kuendeleza sekta hii muhimu ya utalii. Na ikiwezekana, naomba biashara zote zile mpya, wafanyabiashara wale wapya wanaotaka kuingia kwenye sekta hii wapewe angalau likizo ya miezi mitatu mpaka pale biashara zao zitakapokuwa ndipo waweze kutozwa tozo hizi. Tukiweza kufanya hili tutaongeza ajira lakini vilevile tutaongeza wigo wa kodi nchini kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ninaloomba kuongelea jioni ya leo ni kuhusiana na kupanua wigo wa mazao ya utalii na kutangaza pia vivutio vile ambavyo hatuna mazoea navyo. Ukiangalia kwenye sekta hii takriban asilimia 80 tumejikita kwenye utalii wa wanyamapori, na hii ni changamoto kubwa sana ya sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumebarikiwa vivivutio vingi zikiwemo fukwe, mito, milima na utalii wa kiutamaduni. Ukisoma hata hotuba hapa ya Mheshimiwa Waziri, pamoja na maoni ya Kamati, hauoni vipaumbele vya kwenye vivutio vingine kama milima. Tuna mlima mrefu Mlima Kilimanjrao lakini vilevile katika Mkoa wangu wa Arusha kuna Mlima Meru ambao ni namba mbili Tanzania, lakini wa nane Afrika, lakini sijaona jitihada ya Serikali kabisa kwenye kuutangaza mlima huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukianza kutangaza vivutio hivi vingine, tutaweza kuongeza idadi ya watalii, na tutaongeza idadi ya siku watalii wanazokaa hapa nchini. Kwa sababu wakishatoka mbugani kule watakuja hapa watapanda mlima, watatembea kwenye mito, na tukiongeza idadi ya siku ambazo mtalii anakaa nchini, basi tunaweza tukaongeza pia Pato letu la Taifa, lakini na ajira pia kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho ninaloomba kuongelea ni kuhusiana na Chuo chetu cha Taifa cha Utalii. Kwanza kabisa niishukuru Serikali, nimeona kwenye bajeti mmetenga fedha kwa ajili ya kaunzisha tawi la Chuo cha Utalii katika Mkoa wangu wa Arusha; hilo ni jambo jema kwa sababu itawapa fursa vijana wengi wa Mkoa wa Arusha na maeneo jirani yote katika kupata mafunzo ya Utalii na ukarimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hatujaweza kutumia chuo hiki kwa ufanisi. Bado tuna changamoto kubwa ya utoaji wa huduma bora za utalii pamoja na ukarimu hapa nchini. Katika kipindi hiki ambacho tunategemea watalii waongezeke hadi zaidi ya milioni tano kama mlivyosema kwenye hotuba yenu, nashauri tutumie chuo hiki kwa ufanisi ili tuweze kupata wahitimu wenye ubora wa kimataifa wa kuweza kuhudumia wageni wetu. Nishauri pia, kama mlivyofungua tawi katika Mkoa wa Arusha, basi katika maeneo yote ambayo yana vivutio muweze kufungua matawi ili kuweza kuendeleza vijana wetu waweze kupata elimu ya huduma ya kimataifa kwa ajili ya kuwahudumia watalii wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)