Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata fursa hii ya kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii. Mchango wangu utakuwa kwenye maeneo kama matatu hivi. Nilitamani niongelee suala la reli lakini watu wengi wameliongelea, kwa hiyo sitaelekea huko, nitaelekea kwenye maeneo yanayohusu Jimbo langu la Ukerewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wengi mnavyojua Ukerewe inaundwa na visiwa zaidi ya 30. Mategemeo makubwa ya wananchi zaidi ya 300,000 wa Ukerewe kuunganishwa na mji wa Mwanza na maeneo mengine ni kupitia meli. Bahati mbaya usafiri wa meli kutoka Mwanza kwenda Ukerewe umekuwa na matatizo makubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri nimeona hapa kuna pesa zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya meli ya MV Butiama. Suala la MV Butiama limekuwa ni wimbo wa muda mrefu sana, miaka takribani mitano usafiri ni wa shida kweli kweli kwenye eneo lile. Sijui kama Serikali inafurahi muda wote iwe inatoa rambirambi kwenye mazingira kama haya, si jambo jema sana. Yametokea maafa pale Zanzibar, yametokea maafa ya MV Bukoba, sitamani sana jambo kama lile litokee kwenye eneo la Ukerewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna meli moja MV Clarias, napenda kuwapongeza kampuni binafsi ya Nyehunge, wanatoa huduma ya usafiri pale, lakini meli zile zinazotoa usafiri bado hazitoshi, wananchi wanataabika sana kwa usafiri wa meli. Kama kwenye bajeti mmetenga hii pesa kwa ajili ya kutengeneza hii meli ya MV Butiama, itengenezwe iweze kuhudumia wananchi wale. Si hiyo tu, hata meli iliyopo sasa hivi ya MV Clarias haiwezi kumudu muda mrefu, imekuwa ni meli ya muda mrefu sana kila wakati inasumbua, inaharibika. Kwa hiyo, pendekezo langu, pamoja na kutengwa kwenye bajeti shilingi bilioni tatu na point kwa ajili ya marekebisho ya MV Butiama, Wizara iangalie uwezekano wa kutengeneza meli nyingine mbadala wa MV Clarias ambayo ni ya muda mrefu na imechoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niombe Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kuangalia suala la uwekezaji katika visiwa hivi. Ukerewe ni eneo ambalo linaweza kutumika kwa shughuli za utalii, naomba kama kunaweza kufanyika ushawishi ufanyike au Wizara yenyewe itengeneze speed boat kwa ajili ya huduma za usafiri kuunganisha Mwanza na visiwa vya Ukerewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuongelea ni eneo la vivuko. Kama nilivyosema Ukerewe inaundwa na visiwa na kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeonesha kwa mwaka 2015/2016 kuna vivuko kadhaa ambavyo vimefanyiwa marekebisho kikiwemo kivuko cha MV Nyerere. Sawa, lakini kuna maeneo ambayo wananchi wanataabika sana kama kwenye visiwa vya Ilugwa, Izinga na maeneo mengine, niombe Wizara itengeneze vivuko vingine kwa ajili ya kusaidia wananchi wa maeneo yale ambao wanataabika sana na usafiri kutoka kwenye visiwa vile wanavyoishi kuja kwenye kisiwa kikubwa cha Ukerewe na hatimaye kutafuta mazingira ya kusafiri kwenda Mwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata hiki kivuko cha MV Nyerere ambacho kinafanya kazi kwenye eneo la Bugolola na Bwisa kisiwani Ukala, hivi kunakuwa na tatizo gani, kwa mfano Wizara ndiyo inayohusika na vivuko hivi na meli kutoka Mwanza kuja Nansio, ni kwa nini kusiwe na matching ya ratiba kwamba wasafiri wanaotoka Mwanza waweze kuingia Nansio lakini wakawahi vilevile usafiri wa Bugolola kwenda Kisiwa cha Ukala? Sasa hivi wananchi wanataabika sana, wanatoka Mwanza wanakaa Nansio pale zaidi ya saa sita wakisubiri ratiba ya ferry ya kutoka Bugolola kwenda Ukala.
Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri, inawezekana akatoa maelezo ni kitu gani kinaweza kufanyika lakini litakuwa jambo jema sana kwa maslahi ya wananchi wa Ukerewe, hususan kwenye visiwa vya Ukala ratiba hii itawekwa sawa angalau iweze kuwiana na ratiba ya kutoka Mwanza kwenda Ukerewe.
Vilevile uangaliwe uwezekano kutengeneza vivuko vingine kwa ajili ya kusaidia wananchi kwenye visiwa vidogo vidogo vinavyounganisha Ukerewe na maeneo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la tatu ambalo nilitaka nigusie ni suala la barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo sera ya Serikali hii ya kuunganisha mikoa yote ya Tanzania Bara kwa barabara za lami, kuna barabara ya kutoka Bunda – Kisolya - Nansio ambayo kimsingi inaunganisha mkoa wa Mara na Mwanza kupitia Ukerewe. Kwenye hotuba inaonekana kuna mpango wa kuendelea kujenga kati ya Bunda - Kisolya, lakini kuna kipande hapa cha kilometa 11 kutoka Lugezi kufika Nansio, ni kwa nini kipande hiki kisiunganishwe mradi huu ukakamilika wote kwa pamoja? Ni kilometa chache sana hizi, kwamba sehemu moja itengenezwa halafu hizi kilometa 11 zibaki zitafutiwe fedha nyingine au mradi mwingine ndipo ije ikamilike na barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Ukerewe. Tunasema tunatengeza Tanzania ya viwanda, ni muhimu basi tujenge mazingira ya kiuchumi ya wananchi wetu. Kwa wananchi wa Ukerewe, kama barabara hii itatengenezwa kwa kiwango cha lami itasaidia sana mawasiliano na hasa kiuchumi kati ya wananchi wa Ukerewe, Bunda na Mwanza Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe vilevile Wizara hii, ninaamini si eneo la Ukerewe tu, maeneo mengi barabara nyingi zimeharibika. Sasa niombe fedha za Mfuko wa Barabara ziwe zinatolewa mapema na kwa kiwango kile ambacho kinaweza kikasaidia ili Halmashauri zetu ziweze kurekebisha barabara zile zinazokuwa zimeharibika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, kutokana na barabara zetu kutokuwa katika hali nzuri, Halmashauri ya Ukerewe tuliomba kununuliwa greda kwa ajili ya kutengeneza barabara na Wizara ikale greda kwenye Halmashauri ya Ukerewe. Niombe Mheshimiwa Waziri kama anaweza kunisaidia hili, lile greda Halmashauri ya Ukerewe imekuwa haina mamlaka nalo sana kiasi kwamba ikitaka kulitumia liweze kurekebisha barabara za Wilayani Ukerewe inakuwa ni shida kweli kweli kulipata wakati kimsingi Halmashauri hii ndiyo iliyo-process mpaka greda hilo likapatikana. Ni kwa nini sasa kama Wizara msitoe mamlaka, kwa sababu Halmashauri hii ndiyo iliyoanzisha mchakato mpaka greda hili kununuliwa, kwa nini lisikabidhiwe kwenye Halmashauri ile? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jiografia ya Ukerewe ni ngumu sana, msiifananishe na maeneo mengine. Mkifanya hivi mtakuwa mmelisaidia sana eneo la Ukerewe kuboresha barabara zake na inawezekana ikapunguza gharama nyingini ambazo zingekuja kwenu Wizarani. Kwa hiyo, niwashauri kama Wizara, likabidhini greda hili kwenye Halmashauri hii ilisimamie. Kama kuna masharti na taratibu nyingine muhimu basi waelekezwe lakini greda lile liwekwe pale Halmashauri lifanye shughuli za kuboresha barabara za Ukerewe hatimaye basi mazingira ya Ukerewe yawe bora angalau ukilinganisha na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikiendelea kusisitiza, niombe tafadhali, kwenye hii barabara ya Bunda – Kisolya – Nansio, haina sababu kilometa 11 hizi kuziacha, ziunganisheni. Pia kulikuwa na mpango wa kujenga daraja kati ya Lugezi - Kisolya, sijui imefikia wapi Mheshimiwa Waziri nitaomba maelezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.