Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa mwisho katika wachangiaji wa Bajeti yetu ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo. Moja kwa moja nitangulie kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyoifanya kwa kuhamasisha na kuwekeza fedha nyingi kwa ajili ya kusaidia mchezo wa soka hasa kwa Vilabu vyetu vya Simba na Yanga ambavyo mwisho wa siku vimepata mafanikio makubwa. Hongera sana Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan na nimwombe tu Mheshimiwa Rais huko anakonisikia aendelee kutuunga mkono katika mchezo huu ambao unapendwa zaidi kuliko michezo yote duniani ili tuweze kusonga mbele zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia hapa hamasa ambayo imetolewa na Mheshimiwa Rais wetu imepelekea kushuhudia Vilabu vyetu vikifanya vizuri ndani na nje ya nchi kwenye mechi zake. Kwa mara ya kwanza tumeshuhudia Timu za Simba na Yanga zote kwa pamoja zikifanya vizuri katika medani ya soka. Pia tumeona Yanga imekwenda fainali, hongera sana, mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona Club ya Simba ikiwa na consistency kwa zaidi ya miaka mitano ikifanya vizuri na hivyo kupandisha kiwango cha soka kwa vilabu vyetu kwenye ranking za CAF. Kwa Club ya Yanga kutoka nafasi ya 63 hadi kwenda nafasi ya 18, kwa Club ya Simba kutoka nafasi ya 12 kwenda nafasi ya tisa na hivyo kupelekea Club ya Simba kutunukiwa nafasi ya kucheza Super League ya Afrika. Kwa taarifa nilizonazo nyepesi nyepesi hivi karibuni mashindano hayo yatafanyika na huenda yakafanyika nchini Tanzania. Hii itatuongezea fursa nyingine ya kuweza kuongeza zile fursa zilizotokana na royal tour. Kwa hiyo nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uwezeshaji wake kwa hamasa yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nihamie kwenye eneo la Sanaa. Sanaa yetu bado kuna maeneo haijafanya vizuri japokuwa juhudi kubwa zimewekezwa na Serikali yetu ya Awamu ya Sita. Katika Nchi za Uturuki, Marekani na hata Afrika Kusini, hapa Afrika kumekuwa na zile sinema au filamu zinazoendana na historia. Ukienda Uturuki kuna filamu ambazo zinatamba sana sasa hivi za akina Osman, Ertugrul Bey lakini hata Marekani kuna zile filamu za kivita za akina Rambo, Michael Dudikoff na zingine. Niliwahi kushuhudia sinema au filamu inayohusiana na utawala wa King Shaka kule South Africa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nafikiri wakati umefika hivi sasa kwa Serikali yetu kuwekeza kwa wasanii wetu kwa ajili ya kucheza picha ambazo zinaendana na historia. Kwa mfumo huu tutaweza kuongeza ajira katika filamu, lakini pia tutaongeza hisia za kizalendo, tutadumisha utamaduni zikiwemo lugha za asili ambazo Tanzania hapa zinatumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hainingii akilini kuona wale wasanii wetu hawawezi kucheza filamu ile ya Mtwa Mkwawa wakati alipowaongoza Wahehe kupambana na Wajerumani na akawashinda katika awamu ya kwanza na yule Jemedari Zelewski akauawa. Vijana wetu hawawezi hizo lakini hawawezi kucheza sinema ya Vita vya Maji maji ambavyo wananchi wa Kabila la Wamatumbi waliwaongoza wananchi wa kabila zingine kupambana na Wajerumani na katika battle la kwanza waliweza kuwashinda Wajerumani siku 31 mwezi Julai mwaka 1905, pale katika Kijiji cha Kibata. Je, hawawezi vijana wetu kucheza picha zenye mvuto ambazo za wale Walugaluga kule wakiongozwa na Chief Milambo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri kwa wakati huu sinema za namna hii zimekuwa maarufu sana duniani na zimekuwa zikiingiza kipato sio tu kwa nchi hadi kwa msanii mmoja mmoja. Kwa hiyo niwaombe Serikali tuweke mkakati mzuri, tuwezeshe hizi taasisi zetu za BASATA, COSOTA, TaSuBa pamona na Mfuko huu wa Wasanii Tanzania au Mfuko wa Sanaa tuwezeshe fedha kwa sababu tunajua sinema za namna hii au filamu za namna hii zinagharimu fedha nyingi. Tuwekeza, fedha itolewe ruzuku kwa sababu hili jambo lina manufaa ya kitaifa sio tu kwa msanii mmoja mmoja ili tuweze kuendeleza hizi filamu za namna hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hapa majuzi nilikuwa namsikia Katibu Mkuu wa Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo akizungumza na Deutsche Welle kuhusiana na fidia kwa waathirika wa vita mbalimbali ambazo Wakoloni wa Kijerumani walipambana na wananchi au mababu zetu. Alizungumzia Vita vya Maji Maji, akazungumzia vita vya Mtwa Mkwawa na Wajerumani, lakini ilitolewa mifano kule Namibia kulikuwa na Waherero na Wamakwa walipambana na Wajerumani, walilipwa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe Wizara itakapokuja ku-wind up kuhusiana na hii hotuba ambayo imetolewa, waje watuambie mkakati walionao katika kudai fidia, lakini sio fidia tu kudai pia zile malikale ambazo zilitaifishwa na Wakoloni wa Kijerumani kama dinosaur ambaye alitolewa kule Tendeguru, Lindi lakini pia hadi mafuvu na sijui wanayatumia kwa shughuli gani mpaka leo, yarudishwe nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ije itupe taarifa wamefikia wapi katika mkakati huo. Vile vile ningeomba jamii zilizo husika na vile vita katika kudai fidia washirikishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)