Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Spika, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendelo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (nation competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwapongeza wanamichezo wote kwa kufanya vizuri katika mashindano ya kimataifa. Kwa namna ya pekee napenda kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa hamasa na msukumo alioweka katika michezo yote na hasa mafanikio makubwa ya timu ya Yanga katika mashindano ya Kombe la Shirikisho (CAF Confederation Cup). Napenda pia kuwapongeza Klabu ya Yanga kwa kushinda ugenini Algeria katika raundi ya pili ya fainali na kufanya jumla ya magoli mawili kwa mawili kushika nafasi ya pili kikanuni ya Kombe la Shirikisho (CAF Confederation Cup). Kutokana na hamasa ya Mhe. Rais, Klabu ya Yanga imeandika historia na kuipa nchi yetu heshima kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inastahili pongezi kwa mkakati wake katika kuimarisha, kuziwezesha na kufanikisha ushiriki wa timu za Taifa na vilabu katika michezo na michuano mbalimbali ya kimataifa na kikanda. Kama sehemu ya mkakati huo Wizara iweke msukumo zaidi wa kuhamasisha kujenga, kukarabati na kuboresha miundombinu ya viwanja vya michezo hususani vya mpira wa miguu. Viwanja vingi vya mikoani vipo katika hali mbaya na kwa kiasi kikubwa ni sehemu ya changamoto katika maendeleo ya michezo nchini. Michezo na sanaa ni muhimu sana katika kujenga sura na sifa ya Taifa letu (nation brand). Hivyo ni muhimu kwa Serikali kuhakikisha inaweka umuhimu mkubwa wa ushiriki wa timu zetu za Taifa na kuwepo kwa mkakati wa kitaifa wa kuhakikisha timu zetu za Taifa na vilabu zinafanya vizuri kwenye mashindano ya kikanda na kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati huu katika michezo na sanaa ni nguzo muhimu katika kutekeleza Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026. Serikali itenge bajeti ya kutosha kuhakisha tija katika ushiriki wetu katika mashindano ya kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kuboresha miundombinu ya viwanja, Wizara ijikite katika kuibua vipaji mbalimbali vya michezo na sanaa kwa kuimarisha ushirikiano na Wizara nyingine hususani Elimu na TAMISEMI. Pamoja na kutokuwepo kwa miundombinu rafiki, mikoa mingi imekuwa inatoa wachezaji wenye vipaji vikubwa katika mpira wa miguu, riadha na hata sanaa mbalimbali. Imefika muda sasa wa kuwepo kwa mkakati wa kuibua na kuendeleza vipaji hivyo ambavyo vimekuwa vinaonekana kikanda zaidi kama vile riadha kwa Mikoa ya Kaskazini, Nyanda za Juu Kusini na Mikoa ya Kati. Pia kwa upande wa mpira wa miguu kumekuwepo na mikoa kadhaa ya vipaji vikubwa na huko ndio Serikali iweke msukumo zaidi wa kuibua na kuendeleza hivyo vipaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kwa wasanii, kuna Mikoa imekuwa inatoa idadi kubwa ya vipaji kwenye uigizaji, uimbaji ikiwemo nyimbo za injili ambazo zinapata umaarufu sana duniani. Kutokana na vipaji vingi vya michezo hususani mpira wa miguu na riadha, napendekeza Shule ya Sekondari Santilya ya Wilaya ya Mbeya iongezwe kwenye orodha ya shule teule za michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa Kiswahili kuwa Lugha rasmi Kimataifa, napendekeza uwekezaji zaidi katika kuitangaza na pia kuwezesha Ulimwengu kujua kuwa mizizi na ustawi wa Kiswahili ni Tanzania pekee na wengine wanaigiza kwetu. Serikali iendelee kuchukuwa hatua zaidi ya kukistawisha Kiswahili katika Mataifa mengine Barani Afrika na kwingineko kwa kushirikisha vyuo vikuu hapa nchini na vyuo vikuu mbalimbali duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.