Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mheshimiwa Dkt. Pindi Chana (Mb) na Naibu wake Mheshimiwa Hamis Mohamed Mwinjuma (Mb), Katibu Mkuu Bwana Saidi Yakubu, Naibu Katibu Mkuu Ndugu Nicholaus Mkapa pamoja na timu ya wataalam kutoka Wizarani kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita kwenye utekelezaji wa agizo la Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan wa kujadiliana na mamlaka husika kurudisha mafuvu ya vichwa vya machifu wetu na vyombo vya sanaa vilivyochukuliwa kikatili na kupelekwa Ujerumani na wakoloni. Agizo hili alilitoa kwenye uzinduzi wa Tamasha la Utamaduni Kilimanjaro lililoandaliwa na uongozi wa machifu wa mkoa huo tarehe 22 Januari, 2022. Suala hili linazihusu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mamia ya mafuvu ya binadamu yaliyochukuliwa na Wajerumani kutoka makoloni yake ya zamani ikiwemo Tanzania. Inakadiriwa kuwa kuna mafuvu zaidi ya 200 kutoka Tanzania ambayo yako Ujerumani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya mafuvu ya watu maarufu ni pamoja na majemedari wa kabila la Wangoni wajulikanao kama Nduna na Mbano kutoka Songea. Wengine ni Machifu maarufu kama Mkwawa wa Iringa, Sina wa Kibosho, Meli wa Old Moshi na wengine wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafuvu hayo yalichukuliwa na Wajerumani kutoka kwenye maeneo ya maziko hasa makaburi. Mengine yalichukuliwa kutoka kwenye maeneo ya kunyongea watu yaliyokuwa yameasisiwa na Wajerumani hapa Tanzania. Kwa mfano, eneo alikonyongewa Mangi Meli wa Old Moshi katika Jimbo la Moshi Vijijini limehifadhiwa kama sehemu ya makumbusho kule Moshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mangi Meli aliuawa mwaka 1900 kwa kupambana dhidi ya utawala wa ukoloni wa Ujerumani. Baada ya kuuawa mwili wake ulikatwakatwa na kichwa chake kikasafirishwa kwenda nchini Ujerumani. Pia kichwa cha Chifu Mkwawa kilikatwa na kupelekwa Ujerumani akiwa kwenye mapambano na wakoloni wa Kijerumani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kilio kikubwa hapa nchini Tanzania kutoka kwa makabila yenye mashujaa hawa kutaka masalia ya mafuvu ya wapendwa wao kurudishwa nchini. Kilio hiki ni pamoja na kurudisha mafuvu wa Machifu Sina wa Kibosho na Meli wa Old Moshi ambao wametokea Jimbo la Moshi Vijijini, hili ni jimbo langu la uchaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hili, Rais Samia Suluhu Hassan akiwa katika tamasha la Utamaduni, Kilimanjaro lililoandaliwa na uongozi wa machifu wa mkoa huo tarehe 22 Januari, 2022 aliagiza majadiliano ya kurudisha mafuvu ya vichwa vya machifu wetu yafanyike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakfu wa urithi wa kitamaduni wa Prussia huko Berlin, Ujerumani umeridhia kurejesha mabaki kadhaa ya binadamu na kazi za sanaa ambazo ziliibwa na Wajerumani walipokuwa wanatawala baadhi ya nchi za Kiafrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna taarifa zinazoeleza kuwa watafiti wa Ujerumani wameshafanya utafiti wa kuyatambua mafuvu kutoka Tanzania. Kwa mfano, katika utafiti huo, mjukuu wa Mangi Meli kutoka Old Moshi alifanyiwa vipimo vya kinasaba (DNA) ili kusaidia kusaka fuvu la babu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana, wawakilishi kutoka Ujerumani walilitembelea Bunge letu hapa Dodoma na wanashauku kubwa ya kukamilisha zoezi hili. Ninaishauri Serikali kupitia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Wizara ya Maliasili na Utalii walivalie njuga jambo hili kwa pamoja na kukamilisha zoezi la kurudisha mafuvu ya mashujaa wetu nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.