Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania wenzangu kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali za ustawi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuungana na wananchi wa Jimbo langu la Mbulu Mjini kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi anavyoliongoza Taifa letu na Serikali yetu nzima ya Awamu ya Sita kwa utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020 & 2025 kwa kila sekta, Mwenyezi Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Pindi Chana - Waziri, Naibu Waziri na watendaji wakuu wa Wizara hii kwani kuna mafanikio makubwa sana katika Wizara hii muhimu kwa ajili ya kuibua vipaji vya Watanzania na kuchochea fursa ya ajira kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuungana na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Watanzania wenzangu wote kuipongeza sana timu yetu ya Yanga kwa kweli wametuheshimisha mbele ya kimataifa hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia hotuba ya mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii muhimu ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, na maoni ya Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge, Serikali iangalie utaratibu wa kuweka kalenda ya mashindano mbalimbali za vipaji kupitia makundi kwenye ngazi za wilaya. Hata hivyo kuna vijana wengi walioko katika ngazi za shule zetu za sekondari na msingi nchini ambao wanakabiliwa na chagamoto mbalimbali katika kufikia ndoto zao mara nyingi. Kwa hiyo, kuna haja kubwa ya kuimarisha Kamati za Michezo ngazi za Wilaya na Mikoa ili kuelekeza mpango kazi zao kila mwaka na kushirikisha washiriki wa vipajj ngazi za chini ili kufanikisha mpango wa Taifa wa kuwa na washiriki wenye uwezo mkubwa kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iangalie uwezekano wa kila halmashauri nchini kuwa na walimu wa fani ya michezo ili kuendeleza vipaji kwa vijana wetu shuleni. Aidha, Serikali ielekeze halmashauri kama mdau wa sekta hii kutenga fedha za utamaduni, sanaa na michezo kupitia mapato yake ya ndani katika bajeti ya mwaka wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna umuhimu mkubwa sana katika Taifa letu wa kulinda, kuendeleza, kutunza na kustawisha lugha ya Kiswahili kuwa rasilimali tulizonazo kitaifa na kutumia kukipigania ukuaji wake Kimataifa na hapa tuna kila sababu ya kumkumbuka, kumuenzi na kumwombea Hayati Mheshimiwa Julius Kambarage Nyerere Baba wa Taifa letu kwa kutuunganisha sisi Watanzania kutumia lugha moja Kitaifa na kuwa nchi ya mfano Barani Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iwe na data bank ya maeneo ya michezo nchini kuanzia ngazi za vijiji, wilaya, mikoa, na kuzipima na kuendeleza maeneo hayo. Nayasema hayo kwa sababu maeneo mengi yamevamiwa na kutumika kinyume na matarajio ya awali hali itakayohatarisha maendeleo ya sekta ya michezo nchini kutoweka na athari kwa kizazi kijacho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa michezo, utamaduni na sanaa ni fursa kubwa ya ajira nchini tunaiomba Serikali yetu iongeze bajeti ya Wizara hii na kutafuta wadau watakaotuunga mkono ili kupata mafanikio makubwa sana Kitaifa. Aidha, kuna haja ya kuendeleza miundombinu ya michezo nchini na kupangia matumizi kikanda na kimikoa ili kuchochea tasnia ya utamaduni, sanaa na michezo. Naomba pia Serikali yetu itusaidie kutuma wataalam wa Wizara kwa ajili ya kuendeleza na kukarabati Nyerere stadium iliyoko Jimbo la Mbulu Mjini, ni uwanja mkubwa katika mkoa wetu wa Manyara ili kupata mpango mkakati wa kuboresha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho siyo kwa umuhimu naomba kumkumbusha Mheshimiwa Waziri ombi langu la kuwa mgeni rasmi katika fainali ya Kombe la Mashindano ya Jimbo la Mbulu Mjini mwezi wa Julai 2023 ambayo kwa miaka saba sasa kombe hilo huanzia ngazi ya vijiji mwezi Aprili, ngazi ya kata mwezi Mei, ngazi ya tarafa mwezi Juni na kuhitimishwa ngazi ya Jimbo mwezi Julai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Mawaziri/Naibu Mawaziri waliotangulia kwa ushirikiano wao katika kuhitimisha kombe hilo kila mwaka kwa jinsi walivyoshiriki na kutambua mchango wa wananchi na wadau wa michezo katika Jimbo la Mbulu Mjini, asanteni sana, na karibuni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.