Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa hii ya kuchangia bajeti ya Serikali. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi alivyosimamia vizuri uchumi wa Tanzania katika hiki kipindi kigumu ambacho dunia na nchi zote sasa hivi zinapambana na hali mbaya ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli nchi yetu ukilinganisha yale malengo ambayo tulijiwekea wenyewe lakini ni malengo ya millennium (MDGs) tumefanya vizuri sana. Hongera sana Mheshimiwa Rais, lakini hongera sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa sababu wewe ndiyo uko mstari wa mbele kuhakikisha ya kwamba haya yanayotokea yanatokea kwa manufaa ya Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia ukuaji wa pato la Taifa nchi yetu ilikua kwa 4.7% ukilinganisha na nchi za Jangwa la Sahara 3.9%. Kwa hiyo, Tanzania imefanya vizuri kuliko nchi zingine ambazo zilikuwa na wastani wa 3.9%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile exchange rate ya kwetu kwa muda mrefu imekuwa himilivu ukilinganisha na wenzetu na kwa nini inabidi Mheshimiwa Waziri wa Fedha aiangalie sana hii exchange rate isije ikatuyumbisha kwa sababu ukiliangalia nakisi yetu ya bajeti nyingi ni fedha za kigeni. Kwa hiyo, tukiyumba kwenye fedha ya kubadilishia ya shilingi yetu ina maana uchumi wetu utayumba na hii hata inflation tunayoisema sasa hivi ya 3.4% hatutaimudu tena.

Kwa hiyo, tunakushukuru sana kwa hatua tuliyofikia mpaka leo ya kwamba tumeendelea kufanya vizuri, lakini hata ukija kwenye fedha za kigeni bado nchi yetu imefanya vizuri zaidi pamoja na kuongezeka kwa nakisi ya malipo, bado nchi yetu inaonesha kuwa tunaweza kuagiza bidhaa nje kwa miezi zaidi ya minne ukilinganisha na miezi sita ambayo ilikuwepo mwaka jana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ili tuweze kujirekebisha katika hali hii nilikuwa napendekeza Serikali iangalie vigezo ambavyo vinatufanya sisi tuwe washindani ukilinganisha na nchi zingine.

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Madini ndiyo inayotuletea fedha za kigeni. Nashukuru Mheshimiwa Waziri amesema kuwa Benki Kuu itaanza kununua dhahabu kama sehemu ya kuwekeza fedha za kigeni na hii ni hatua muhimu, kwa sababu Benki Kuu itanunua dhahabu kwa kutumia shilingi, lakini dhahabu itakayonunuliwa ni sawa na fedha za kigeni. Ombi langu ni kwamba Serikali iangalie jinsi ya kuwalipa hawa hasa wachimbaji wadogo bei ambayo ni nzuri ukilinganisha na wanunuzi wengine. Kwa hiyo, kila wakati Serikali iwe flexible kuwa itakachowalipa hawa wachimbaji wadogo wadogo bei yao iwe nzuri zaidi ili tuweze kukusanya dhahabu ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa ubunifu wake kwa sababu katika hii dunia ya ushindani bila ubunifu unaweza kwenda na maji. Juzi mimi nilikuwa shuhuda wa Serikali ilikuwa inasaini mikataba ya ujenzi wa barabara kwa njia ya EPC+F (Engineering, Procurement na Construction + Finance); huu ni ubunifu mkubwa mno. Sijawahi kuona ujenzi wa barabara kilometa zaidi ya 2,000 na mkataba wa shilingi trilioni 3.7 ambayo ni mbadala wa tulivyozoea ku-finance ujenzi wa miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nikiri kabisa inawezekana tulichelewa kufanya mifumo ya aina hii ya utekelezaji wa miradi yetu na nina imani kwa sababu mikataba imeshasainiwa, imani ya kwangu ni kwamba hizi kilometa zaidi ya 2,000 zitakamilika ndani ya muda mfupi. Serikali hapo haitaingiza tena mfukoni kwake kwa ajili ya kulipa ujenzi wa hizo barabara mpaka mradi utakapokamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wengi wanaweza kuwa wanajiuliza itakuwaje wakishamaliza? Kinachotakiwa hapa ni jinsi ya kufanya management ya ukwasi wa Serikali yetu. Kwa hiyo, planning ni muhimu kuhakikisha kuwa itakapoiva hii mikataba tuweze kuwalipa ili tuendelee hata katika miradi mingine. Ninashukuru vilevile katika hizi barabara, imo barabara ya TANZAM kuanzia Igawa mpaka Tunduma ambayo itakuwa ya njia nne na hii siyo barabara kwa ajili ya Tanzania peke yake, ni barabara pamoja na majirani zetu wa nchi za SADC ikiwemo DRC Congo, Zambia, Malawi, Zimbabwe lakini mpaka Afrika Kusini na hii ndiyo inabeba uchumi wa Tanzania kwa Dar es Salaam Corridor. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hii EPC+ Finance, lakini Serikali imeonesha kuwa sasa hivi miradi mingi tutakwenda kwa mfumo wa PPP. Kwa muda mrefu Mradi wa PPP ilitakiwa uanze lakini ilichelewa kutokana na sheria yetu ilikuwa siyo rafiki kwa wawekezaji. Bunge lako mwezi huu limeshapitisha marekebisho ya hiyo sheria na kutokana na hayo marekebisho, itaanza na ujenzi wa barabara ya Kibaha – Chalinze – Morogoro ambayo itakuwa ni express highway lakini baadae itakuja Morogoro mpaka Dodoma na itakuja na ring road au barabara ya mzunguko hapa Dodoma na nina imani vilevile itaenda kwenye ujenzi wa reli ya Kusini Mtwara – Mbamba Bay, lakini na barabara ya Kaskazini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu mfumo wa PPP ndiyo mifumo inayotakiwa sasa hivi katika utekelezaji wa miradi ya miundombinu kwa sababu risk yote ya miradi unaihamishia kwa sekta binafsi ikiwemo na EPC ni kwamba risk zote unakuwa umezihamishia kwa watu binafsi, kwa hiyo, Serikali kinachotakiwa ni kuisimamia na kuhakikisha kuwa kile tulichokubaliana kinaenda sawia, lakini vilevile na ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni imani yangu kutokana na maboresho ya bandari ambayo yanafanyika sasa hivi, nina imani kuwa fedha za kigeni zitakuja za kutosha kwa ajili ya kuhimili madeni haya yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ninachoomba Serikali pamoja na hayo maboresho kutakuwa na ongezeko la mizigo, tuhakikishe tunakamilisha SGR kwa muda mfupi, lakini tukamilishe vilevile reli ya TAZARA ni muhimu kwa ajili ya biashara ya bandari yetu kwa sababu hiyo mizigo asilimia 70 yote haitakuwa bora yaanze kupita tena kwenye expressway, tupitishe kwenye reli ambayo itatufanya gharama za usafirishaji za kwetu ziwe za chini ukilinganisha na nchi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kupambana na hali hii ya uchumi, naiomba Serikali iangalie zaidi na iweke kipaumbele cha kwanza kuhakikisha inaboresha biashara ya madini. Madini ndiyo yanayotuletea fedha zetu za kigeni kwa sasa hivi. Nimeona juzi nampongeza tena Mheshimiwa Rais ameidhinisha kulipa fidia ya wananchi wa Liganga walipwe zaidi ya shilingi bilioni 15 kwa ajili ya kufufua ule mradi mkubwa. Ule mradi utailetea Tanzania FDI zaidi ya shilingi bilioni tatu ambayo ni fedha nyingi sana. Ajira zaidi ya 30,000 lakini utakapochimba chuma na haya makaa ya mawe naomba haya yachakatwe hapa hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naiomba Wizara ya Madini Serikali iharakishe vilevile machimbo ya madini ya niobium kule Mbeya kwa sababu yale ndiyo utakuwa mgodi wa kwanza Afrika na mgodi wa tatu duniani na madini ya niobium ni kwa ajili ya kutengeneza kifaa kinaitwa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 malizia Mheshimiwa.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, madini ya niobium ni kwa ajili ya kutengeneza chuma kinaitwa ferroniobium ambacho kinahitajika sana kwenye ujenzi wa madaraja pamoja na reli zetu, lakini vilevile naiomba Serikali tunaporekebisha hiyo miundombinu vilevile na barabara ambazo zinalisha hizi barabara kuu kama barabara ya Mbalizi – Shigamba nayo ipewe kipaumbele, barabara ya Isyonje – Kikondwe ipewe kipaumbele, barabara ya Mbalizi – Chang’ombe – Makongorosi ipewe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)