Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia namuombea kwa Mwenyezi Mungu ambariki na sisi sote pia atubariki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili, nikupongeze wewe mwenyewe kwa kazi kubwa unayoifanya ya kusimamia Bunge hili vizuri na kwa kweli sheria uliyoisoma tunaiona matokeo yake. Nasema hayo kwa sababu wakati ule wa Azimio la Bandari kama hapo angekaa mtu ambaye haelewi elewi sheria yawezekana lile azimio lingerudi nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nitumie nafasi hii kuwaomba ndugu zangu wa kule Nyasa maana yake na wenyewe wamekuwa wanasema mama vipi huko, mama vipi huko? Hasa kuna dada mmoja anaitwa Angella Mayi kimsingi Bunge lipo imara na linafanya kazi zake kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi na tunashauriwa kupitia Mtume Paulo kwamba tusiwakwaze wenzetu wanapojaribu kufanya mambo mazuri, ni wajibu wetu kusaidia na kushauri kwa upole ili jambo liweze kutekelezwa ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jinsi ambavyo anaingoza Serikali vizuri humu Bungeni, lakini pamoja na Wabunge wote kama hasa wa CCM kama Mwenyekiti wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Nyasa, Tarafa ya Mpepo tunalima kahawa, safari hii malipo ya Stakabadhi Ghalani yale malipo ya awali yamechelewa sana kiasi kwamba yanaweza kuleta athari. Kwa hiyo, niwaombe wanaohusika washughulikie mapema ili kunusuru hali hayo, lakini pia hata kama kutakuwa na haja ya kufanya mabadiliko namna ya mfumo wa kuuza kahawa basi ni vyema wananchi wenyewe washirikishwe kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na Naibu wake na timu nzima ya Wizara ya Fedha kwa kazi kubwa waliyofanya, lakini pia hata elimu waliyotupa katika kipindi cha wiki hizi zilizopita imetusaidia sana kufahamu mambo mengi ambayo yanayohusika katika Wizara hii na kwa namna ya pekee nakupongeza kwa ajili ya suala la uliloliandika katika ukurasa wa kumi kifungu namba 16 kinachohusu watu wenye ulemavu kwa kutenga shilingi bilioni moja itakayoweza kuwasaidia katika kupata vifaa saidizi pamoja na mambo mengine ya mitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wenye ulemavu wana changamoto nyingi sana, ni mtu mpaka uishi nao ndiyo utazijua. Mtu mwenye ulemavu ni gharama yaani hata kumuhudumia ni gharama. Sasa hivi kuna mwanafunzi kwa mfano yupo pale Chuo cha IAA, Arusha anachangamoto kubwa kwa sababu ni mlemavu anayesota kwa matako, anatakiwa atembee karibu mita 500 kwenda darasani, wenzake wambebe na wenyewe hawapendwi kubebwa, wanapenda kujitegemea, wanapenda utu wao, wanashida.

Ushauri wangu ni kwamba pamoja na fungu hili uone ni namna gani linaweza kutumika katika kusaidia hasa vile vyuo ambavyo havijaweka sera rasmi ya kusaidia watu wenye ulemavu, kupata vifaa saidizi na kwa hii na kukabidhisha huyu binti Sayuni yuko pale Arusha, naomba umsaidie apate angalau kibajaji hata kama kitakuwa ni cha shule aweze kukitumia atakapomaliza watatumia wenzake, inakuwa ni changamoto kubwa sana, naongea kwa uchungu mkubwa kama mzazi na kwa uzoefu mkubwa wa suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kusema kwamba Serikali inasikiliza, siku zote watu tunafikiria tunasema Wabunge wanaongea tu, wanaongea tu, Serikali ina masikio, masikio ninayoyaona hapa sasa ni jinsi ambavyo Wabunge kwa muda mrefu walikuwa wanazungumzia kusaidia kuchangia wanafunzi wanaosoma katika Vyuo vya Ufundi na Sayansi kwa ujumla. Nimefurahi kupitia ukurasa namba 29 mnasema kwamba mtaondoa ada/mnachopendekeza kuondoa ada katika vyuo hivi vya DIT, MUST, ATC kwa kuanzia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nawapongeza sana, lakini naomba kuongeza Chuo cha NIT hakiko hapa, nacho mkiangalie, sasa hivi tunatengeneza reli, tunafanya mambo ya usafirishaji (logistics) chuo hiki ni muhimu sana katika masuala hayo, naomba kama kilisahaulika kiongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na ukurasa wa 38 kwenye sensa, matokeo ya sensa tumeyapata na hayo tumeambiwa kwamba idadi za watu zisaidie katika kuhakikisha kuwa mipango ya rasilimali inatumika vizuri. Mimi ninachoomba kuongezea isiwe idadi ya watu tu na umbali wa upatikanaji wa huduma uzingatiwe, ukubwa wa maeneo uzingatiwe, mambo yote tusiende tu kiurahisi rahisi kama yale ambayo tulikuwa tunayasikia pengine haya hapa pateni kumi na tano, kumi na tano ngapi hapana. Tuangalie na mambo mengi ya mapungufu yaliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo niwashukuru sana pia kwa suala hili la ujenzi wa reli ya Mtwara mpaka Mbamba Bay ambayo iko kwenye hatua za manunuzi. Tunashukuru sana sisi wa ukanda ule, lakini hata Taifa kwa ujumla reli hii itakuwa na msaada mkubwa sana katika shughuli za kimaendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuishukuru Serikali kwa kusikiliza Wabunge kupitia hoja ambayo niliitoa katika bajeti iliyopita juu ya changamoto ya watu kuhamisha ardhi, gharama kubwa za uhamishaji wa ardhi baada ya kununua. Lakini nimefurahi kupitia ukurasa wa 98 mpaka 99 kifungu (b) Sura 332 ya Sheria ya Kodi inazungumziwa kupunguza kodi hiyo kutoka asilimia 10 mpaka tatu na kwa wale ambao wametunza kumbukumbu zao vizuri asilimia 10 ya yale mauzo ambayo yalifanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naona hii itasaidia sana kufanya masuala ya kiuwekezaji yaende kiurahisi, lakini kuwa na taarifa sahihi ya wamiliki wa ardhi, ndiyo maana mara ya mwisho nimesikia Mheshimiwa Waziri wa Ardhi anakilalamika kwamba kuna hati zimeshatengenezwa zaidi ya 2,000 lakini watu hawajachukua, hawajachukua kwa sababu yawezekana hayo majina hayapo sasa hivi, hayahusiki ndiyo maana watu walikuwa hawajaenda kuchukua. Lakini kwa mabadiliko haya ya sheria hii nayaunga mkono sana na napongeza sana na naamini yataleta mabadiliko makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda pia katika suala ambalo Mheshimiwa Waziri wa Fedha ulitoa commitment kipindi kile kuhusiana na kupata fedha maalum au tozo maalum kwa ajili ya kusaidia afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunahangaika kufanya masuala ya kidigitali ya tusaidie katika kufanya shughuli zetu na mifumo ya afya ni vizuri sana ikaongea, unaweza kukuta sehemu nyingine wanadawa sehemu nyingine hawana dawa, unaweza kukuta sehemu nyingine kuna watumishi wengi sehemu nyingine hakuna watumishi wa kutosha, lakini kupitia mifumo hii ya kidigitali tutaweza kupata mambo mengi ambayo yanatuunganisha na kuweza kuboresha katika hizi huduma za afya.

Kwa hiyo, kwa misingi hiyo nazidi kusisitiza eneo la afya ni muhimu sana labda pengine tulichelewa haijaingia katika bajeti hii, lakini ni muhimu ifikie mahali sasa wananchi hawa wapate matibabu yao vizuri, bila shida, mmefanya kazi kubwa sana kujenga vituo vya afya, zahanati na maeneo mbalimbali ambayo yanatoa huduma za kiafya, lakini changamoto ambayo imebakia ni hiyo ya kuimarisha huduma za msingi pamoja na vifaa tiba.

Mheshimiwa Spika, wengine mpaka wanasema kwamba tumekosea, tumejenga vituo vya afya vingi sana, lakini ukiwafatilia wanaosema hivyo ni wale wanaoishi mjini ambazo huduma zote zipo. Haiwezekani mama mjamzito alazimike kusafiri kilometa 20 anaenda kupata sehemu ya kujifungulia, huyo mama lazima tu ataamua kubaki na kujifungua nyumbani. (Makofi)

Kwa hiyo, wakati mwingine tunasema tupunguze vifo vya kinamama na watoto, tupunguze wanawake wengi wakajifungulie katika sehemu za huduma sahihi, lakini wamekuwa hawaendi kwa sababu tu kwamba kule mnakomlazimisha aende hawezi kwenda kutokana na changamoto kubwa za kiusafiri na wakati mwingine inabidi apande pikipiki, yuko barabara labda ina mashimo, anatembea huko mama wa watu anakaribia kujifungua, hatujui kwa sababu tu kwamba nini wengine akina baba mnatuonea huruma tunajua, lakini hamjaonja uchungu wa kujifungua, mngekuwa mmeonja mngejua kwamba hata kutembea kilometa moja wakati uchungu umeshakushika ni kazi kubwa sana. (Makofi)

Sisi mama zenu tumejitolea sana, yaani tumejitoa kwa hali ya juu kwa kutaka tu kwamba tuwe na watoto na ndiyo tuongeze Taifa na ndiyo maana tunaona kwamba hata sasa hivi Mheshimiwa Rais anapofanya maamuzi yake mengine ni ya uthubutu wa hali ya juu, ni kwa sababu akinamama tumezoea kuthubutu ndiyo maana tunafikia hayo malengo na mafanikio tunayoyafanya. (Makofi)

Kwa hiyo, niwaombe sana, fanya hata kama itabidi kwa miaka miwili tupate hiyo tozo, tuboreshe hivyo vifaa ili kuwe na tiba kamilifu katika maeneo hasa kwa vituo hivi ambavyo tayari tumeishavijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wakati huo huo suala la watumishi wa afya jamani hili lisiwe ni suala la kuzungumza sana, tusaidieni, tusaidieni watu wanaotakiwa kutibu wawepo kwenye maeneo ili watu wapate huduma inayostahili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)