Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi na mimi nichangie. Awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu ya kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya katika Taifa hili, ni ukweli usiopingika Mheshimiwa Rais amepokea miradi mikubwa na ameiendeleza vizuri na tunaona anaibua miradi mingine mikubwa, kwa kweli tuna kila sababu ya kumpongeza, tuna kila sababu ya kuendelea kumuombea ili Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya njema, aendelee kufanya kazi vizuri, lakini haya mazuri yote tunayoyaona tunaamini ni pamoja na wasaidizi wake hasahasa akiwemo Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kazi kubwa unayoifanya ya kusimamia Wizara inayokusanya fedha. (Makofi)

Ninakupongeza sana ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu, unafanya kazi kubwa nzuri, songa mbele tuko pamoja na wewe na ninaamini Mungu atakusaidia kwa kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee mikoa hii ambayo ni mikoa masikini. Ukiangalia kwenye bajeti zilizopita bado sijaona mkakati na mipango maalum ya Serikali kuweka nguvu kwenye hii mikoa maskini na miongoni mwa mikoa maskini, nisikitike mkoa wangu wa Kagera ni miongoni mwa mikoa maskini.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo ambalo linasikitisha ukija kuangalia hii mikoa ambayo ni maskini ndio mikoa ambayo zile fursa za kiuchumi haziko sawasawa. Ukija kuangalia mimi napakana na nchi ya Uganda, ukiangalia kwa majirani zetu pale, ukiangalia barabara wamekuja wameleta mpaka mpakani tena wakavuka wakaingia kwetu kidogo kutuonjesha, kwetu ukiingia hali ni mbaya.

Mheshimiwa Spika, nimeongelea barabara ya Mgakorongo kwenda mpaka Murongo, nimeongelea barabara ya Murushaka kwenda mpaka Murongo, barabara hizi zimeshatangazwa tender lakini shughuli ni kusaini barabara hizi ili ziweze kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri Mkoa wa Kagera tuna fursa nyingi sana, lakini shida iliyopo miundobinu ya barabara siyo rafiki. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, mimi ninaamini kazi unayoifanya ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, nimejaribu kufuatilia sana baada ya kuona Waziri ananiambia baada ya wiki mbili tutakwenda kusaini, baada ya wiki moja tutasaini. Sasa nikafuatilia, taarifa za ndani nilizozipata wanasema shida ni fedha. Sasa ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, wewe ndiye mwenye fedha, nikuombe sana barabara hii ambayo ni ya Murushaka kwenda mpaka Murongo, barabara ya Mgakorongo, barabara hizi zisainiwe ili tuweze kuinua uchumi wa Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kyerwa sisi tunalima kahawa nyingi sana, lakini nguvu tunayotumia kuisafirisha kahawa hii kwenye barabara hizi mbovu unakuta tunatumia gharama kubwa wakati tungeweza kutumia gharama kidogo.

Mheshimiwa Spika, lakini mikoa hii ambayo ni maskini ndiyo mikoa ambayo hata umeme wa uhakika hakuna. Umeme kwa siku unaweza ukakatika zaidi ya mara kumi, kweli hapo tunategemea hawa wananchi wanaweza wakaendelea? Tunaweza tukainua uchumi wao?

Mheshimiwa Spika, mimi kwangu nina vitongoji 617, kati ya vitongoji hivyo vitongoji 400 havina umeme; mnategemea hawa wananchi watainuka kweli? Lakini mikoa hii ambayo ni maskini fuatilia muangalie miradi ya maji, ni midogo sana. Hata hiyo iliyopo bado fedha inayoletwa kwangu mimi nina mradi wa Nkwenda mpaka Chanya, nina mradi wa Isingilo, nina mradi wa Mabila, miradi hii inavyokwenda inakwenda kwa kusasua kwa sababu fedha haiji kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, mikoa hii ambayo ni maskini uweke mpango maalum namna gani ya kuboresha miundombinu, namna gani ya kuipelekea miradi ya maji, namna gani ambayo mnaweza mkaipelekea umeme wa uhakika ili tuone kama hii mikoa inaweza ikainuka.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilisemee ni kahawa; kahawa ni zao la kimkakati, lakini zao hili, mimi nipongeze kwa sehemu Serikali imejitahidi ndani ya miaka hii miwili ya mama yetu Samia, kahawa tulikuwa tunauza bila utaratibu, lakini angalau tuemeweza kuipeleka kwenye mnada bei angalau inaweza kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini bado niiombe sana Serikali ifanye utafiti kwa nini nchi jirani ya Uganda kahawa bei iko juu kuliko Tanzania? Tunafanya kazi kubwa ya kupambana na watu wanaofanya magendo. Hebu tufuatilie; hawa Uganda wanauza wapi? Mimi ninaamini soko la kahawa dunia nzima ni moja, sasa hawa Uganda wanauza wapi?

Mheshimiwa Spika, tufanye utafiti wa uhakika ili tuweze kuwapa wakulima hawa bei nzuri tuondoe hii biashara inayoendelea ya magendo na kuanza kukimbizana na watu, kuwapiga na kufanya mambo mengine, kwa sababu hatuwezi kuzuia, kama huna bei nzuri jirani yako ana bei nzuri, watu watakimbia. Mimi Mbunge siungi mkono biashara ya magendo, lakini unazuiaje? Kwa hiyo, niombe sana Serikali iliangalie.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la kahawa kuna hii biashara ya butura inayoendelea. Biashara hii lazima tuje na mpango wa kuwawezesha hawa wakulima angalau waweze kupata fedha ambayo itawasaidia pale wanapoanza kuhudumia hii kahawa mpaka wanapofika kipindi cha kuvuna, awe na fedha ya kumsaidia kuhudumia kahawa mpaka anaipeleka kwenye soko.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri umeongelea suala la makusanyo na kwenye hotuba yako ukaeleza mwamko mdogo wa watu kulipa kodi.

Ndugu zangu, mimi nilikuwa namwomba sana Mungu, ni kwa nini Watanzania hatutaki kulipa kodi na hatutaki hata kudai risiti tu. Unatoa fedha yako mfukoni unakwenda kununua kitu lakini unaona haikuhusu. Ni kwa sababu hatuna upendo na Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, na nianze na sisi humu ndani, leo tumekuja hapa kila mmoja anaeleza anataka barabara, anataka maji, lakini wewe umewajibika vipi kuhamasisha wananchi wako, kuhamasisha wafanyabiashara ulionao, lakini wewe mwenyewe binafsi unapokwenda kununua vitu ni mara ngapi umedai risiti? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara wengi mko humu ndani, ni mara ngapi mmeiibia Serikali? Halafu tunakuja hapa tunataka barabara. Kila mmoja awajibike kwenye nafasi yake. Tulitangulize Taifa mbele, tuwe na upendo kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi hii tunayoidai siyo kwa faida ya Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, wala siyo kwa faida ya Mama Samia tu, ni kwa faida ya Watanzania wote. Wote tuiwa na moyo wa upendo kwa Taifa, tukalitanguliza Taifa, unapokwenda kununua kitu ukadai risiti, mimi hata kama ni shilingi 5,000 lazima unipe risiti, vinginevyo utarudisha hela yangu. Hebu tuwe na moyo wa kulitanguliza Taifa, tudai risiti tukalipe kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nina uhakika Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, hela mnayoikusanya na hili jambo ninalowaambia nimemwomba Mungu na nina uhakika Mungu alichosema na mimi ni sawa, Watanzania hatuna upendo na Taifa letu. Nina uhakika Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kama kila Mtanzania akisimama kwenye nafasi yake, akalipa kodi sawasawa, akadai risiti anapokwenda kununua, hela tunayoweza kukusanya peke yake inaweza ikakamilisha miradi yote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwaombe sana ndugu zangu kila mmoja awajibike. Wafanyabiashara wanapodai Serikali iwahudumie na wao wawe tayari kuhakikisha wanalipa kodi kwa uaminifu. Sisi Wabunge tunapokwenda tunasema tunataka barabara, tunataka miradi ya maji, tunataka umeme, na sisi tuwajibike tuwe waaminifu kulipa kodi, tuwe waaminifu kuhakikisha tunadai risiti tunaponunua bidhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingineā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Bilakwate, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)