Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Selemani Jumanne Zedi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukene

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia. Awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji wake mzuri na moja kwa moja nitaanza na mitandao ya simu katika maeneo ya vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Serikali kubaini kwamba, makampuni ya simu za mikononi yamekuwa reluctant kujenga minara katika maeneo ya vijijini kwa sababu maeneo hayo hayana mvuto wa kibiashara Serikali kwa nia njema kabisa iliamua kuanzisha Mfuko Maalum wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) ili uweze kutumia fedha za mfuko huo kujenga minara katika maeneo ya vijijini. Lakini mpaka sasa nimeona kuna jitihada fulani zimefanyika, lakini bado maeneo mengi ya vijijini hayana huduma hii muhimu ya simu za mikononi. Mimi mwenyewe kwenye jimbo langu katika huu mfumo wa UCSAF ni kata za Isagehe na Semembela na Kamahalanga ndizo ambazo ujenzi wa minara ya simu umeanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ombi langu kwa Serikali ni kwamba, kwa kuwa bado makampuni haya ya simu ya Airtel, Vodacom na Tigo tukiyaachia yenyewe yajenge minara kwenye maeneo ya vijijini hayataweza kufanya hivyo kwa sababu, hakuna mvuto wa kibishara. Kwa hiyo, naishauri Serikali kwenye maeneo mengi ya Vijijini bado mfuko huu wa UCSAF utalazimika kujena minara hata kwa kutoa ruzuku kwa asilimia mia moja. Tukiyaachia haya makampuni ya simu hayataweza kujenga kwa sababu maeneo hayo mengi hayana mvuto wa kibiashara na makampuni haya motive yake kubwa ni faida tu hayataweza kwenda huko. Kwa hiyo, tunahitaji mfuko wa UCSAF ujenge minara maeneo ya vijijini, maeneo mengine uwe tayari kujenga hata kwa asilimia mia moja kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu tatizo la upelekaji wa fedha katika Halmashauri zetu za Wilaya hasa Mfuko wa Barabara na fedha za ruzuku (LGCDD), ili kuhudumia barabara ambazo zinahudumiwa na Halmashauri za Wilaya. Kuna tatizo kubwa sana la kwamba fedha tunazopanga kwenda kuhudumia barabara zetu za Halmashauri mwisho wa mwaka unapofika ni asilimia ndogo mno ya fedha inakuwa imekwenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano wa Halmashauri yangu ya Wilaya ya Nzega, mwaka 2014/2015 kwenye Mfuko wa Barabara tulitenga takribani milioni 700 kwa sababu Halmashauri ya Wilaya ya Nzega inamtandao wa barabara wa karibu kilometa mia sita na kitu. Kwa hiyo, tulitenga na tulipanga shilingi milioni 700 ziende kuhudumia barabara za Halmashauri ya Wilaya ya Nzega, lakini mpaka mwisho wa mwaka unafika ni shilingi milioni 300 tu zilikuwa zimekwenda na hivyo kufanya barabara nyingi kukosa huduma. Lakini hali ilikuwa mbaya sana kwenye mfuko wa LGCDD ambako tulipanga zipelekwe shilingi milioni 700, lakini mpaka mwaka unaisha ni shilingi milioni 49 tu zilikuwa zimekwenda kwa hiyo…
MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa.
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naunga mkono hoja na tulikubaliana na Mheshimiwa Mwakasaka atamalizia dakika tano nyingine, asante sana.