Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi ya kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa zawadi ya siku ya leo. Pia, nichukue nafasi hii kukushukuru wewe kwa jinsi ambavyo unaliongoza Bunge letu Tukufu. Siku zote nimekuwa shahidi na Watanzania wamekuwa mashahidi juu ya uwezo wako na umakini wako katika kuliongoza Bunge letu Tukufu. Siku zote ukikaa hapo linapokuja jambo gumu, taaluma yako, uzoefu wako na umakini wako linakuwa ni jawabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana tu peke yake umeendelea kuonesha hivyo tulipokuwa tunapitisha Muswada wa Finance Bill. Katika Kifungu kile ulilazimika kuwaimamisha baadhi ya Wabunge waliokuwa kwenye Kamati ile kulikuwa na jambo dogo lakini kulikuwa na athari kubwa, lakini wewe mwenyewe uliliona kwa jicho lako na ukatufanya wote tulione. Nakupongeza sana kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakika watu wa Mbeya wanaendelea kuona na kwa kweli ninahakika kelele zile hazitamnyima Tembo kunywa maji na mambo yatakaa vizuri tu, nichukue nafasi hii sasa kurudi kwenye hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Spika, ni kweli usiofichika kwamba hatua ya leo ya kuleta pendekezo na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Comrade Mohamed Mchengerwa na Wasaidizi wake wote, baada ya maamuzi ya Mheshimiwa Rais, kwanza, nichukue nafasi hii kukupongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa uamuzi huu wa busara. Mimi nitamke bayana kwamba maazimio yote mawili ninayaunga mkono kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kulinda, kuhifadhi na kuendeleza rasilimali za nchi ni jukumu la kila raia kwa mujibu wa Katiba, lakini suala la kumaliza migogoro kati ya Hifadhi za Taifa, maeneo yaliyohifadhiwa au maeneo yanayopzunguka hifadhi zetu za Taifa kwa kweli Wizara yako inayo dhamana hiyo na nafasi kubwa ya kusaidia katika kumaliza migogoro hiyo. Leo umeonesha kwa vitendo kwamba yale uliyosema wakati wa ziara zako ulipokuwa unatembelea Hifadhi za Taifa kwamba utahakikisha kero hizi zinashughulikiwa, leo umeshughulikia mpaka umeweza kumpelekea Mheshimiwa Rais na kwa mamlaka aliyonayo Mheshimiwa Rais kwa mujibu wa sheria ameridhia kupunguzwa kwa hifadhi hizi mbili na moja kubadilishwa matumizi kutoka Hifadhi ya Taifa Kwenda TFS, hatua hii ni ya kimapinduzi na hatua hii ni faraja sana kwa wapiga kura wetu na Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, nichukue nafasi hii sasa kumpongeza mwenye mamlaka mwenyewe aliyeridhia hifadhi hizi mbili, moja iweze kumegwa na nyingine iweze kubadilishwa kutoka katika hadhi ya Hifadhi za Taifa na kwenda kuwa chini ya TFS naye si mwingine ni Dkt. Samia Suluhu Hassan, ninampongeza sana jinsi alivyowajali wapiga kura wake na Watanzania na ni jambo lake la kawaida, mimi nataka niseme wazi kwamba GN Na. 28 ya mwaka 2008, Kamati imethibitisha na wewe mwenyewe umethibitsha kwamba kwa kweli ushirikishwaji haukutosha, ndiyo maana wananchi walikuwa wanalalamika sana katika maeneo hayo ambayo GN Na. 28 iliweza kuondoa baadhi ya maeneo ya wakulima, wafugaji na kuyaingiza maeneo hayo katika Hifadhi ya Taifa bila ushirikishwaji wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni rai yangu tu kwamba sasa mmefanya maamuzi ya hekima, maamuzi haya yamefanyika baada ya ziara yako Mheshimiwa Waziri lakini pia baada ya ziara ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira. Ninataka nichukue nafasi hii kuipongeza Kamati, kukupongeza wewe na msaidizi wako Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Mtendaji Mkuu wa TANAPA na Mtendaji Mkuu wa TFS.

Mheshimiwa Spika, niseme bayana kwamba, kama tukifanya hivi katika maeneo mengine kwa kuzingatia mahitaji halisi ya wananchi wetu katika kuinua na kushughulikia masuala yao ya kiuchumi tutakuwa tunafanya maamuzi ya kushughulikia ustawi wa watu wetu. Ni dhahiri basi kwamba haya yaliyofanyika Ruaha, yaliyofanyika Kigosi yakiendelea pia kufanyika Kanda ya Kaskazini mwa nchi yetu itasaidia sana kupunguza migogoro iliyoko huko.

Mheshimiwa Spika, nieleze bayana kwamba Mheshimiwa Waziri nina imani nae kubwa sana, ninaimani kwa sababu anatoa muda wa kusikiliza Wabunge, na mimi amenisikiliza katika suala la migogoro tuliyonayo katika eneo lile, ninaamini busara uliyoitumia baada ya kwenda kule Ruaha, ninakuomba na nikualike rasmi uje Kanda ya Kaskazini kwa maana ya Mkoa wa Manyara na Mkoa wa Arusha, ndipo mtakapoweza kujua kwamba changamoto kubwa waliyonayo wafugaji katika Wilaya za wafugaji na hata migogoro ambayo inatokana na mchakato unaoendelea wa timu inayofanya tathmini ya maeneo yenye rasilimali za wanyamapori katika mapori ya maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, hali hii imeleta taharuki kubwa sana kwa sababu tumetoa kama wafugaji maeneo ya hifadhi mnazozijua, haibishaniwi kwamba tumetoa mchango mkubwa Serengeti, Tarangire, Lake Manyara, Ngorongoro na tumetoa mchango mkubwa Mkungunero lakini bado mpaka leo katika ardhi ambayo iko kwenye nyanda kame, ardhi ambayo haitoshelezi malisho ya mifugo iliyoko leo, bado kuna mawazo na watu wanaopita katika kuangalia maeneo ambayo tumeyatenga kwa ajili ya malisho ya mifugo, ambapo tunapotenga maeneo ya mifugo ndiyo hayo hayo ambayo wanyama wetu ambao ni rasilimali za nchi wanapopata malisho kwa muda kabla hawajarudi katika Hifadhi za Taifa, mapori tengefu na mapori ya akiba.

Mheshimiwa Spika, kinachoshangaza sasa zoezi linaloendelea ambalo linajumuisha Wizara kadhaa linachukua sura sasa ya kutaka kuanzisha hifadhi nyingine katika eneo la Olokisale Game Controlled Area, eneo lote la Simanjiro Game Controlled Area, eneo lote la Southern Ruvu Masai Game-Controlled Area, eneo la Lake Natron Game Controlled Area, eneo la Longido Game Controlled Area.

Mheshimiwa Spika, nikueleze athari inayojitokeza ni hii, ni dhahiri kwamba maeneo niliyoyataja yanaifanya Simanjiro kwa ujumla kuwa ni eneo ambalo awali kulingana na Sheria ya Fauna Conservation ordnance ya Mwaka 1951 ilikuwa ni Wilaya nzima za Masai zilikuwa chini ya game-controlled area. Sasa kama maeneo yale tumeshayatoa kwenye hifadhi hizo na tumebaki na maeneo madogo ya malisho ambayo hayatutoshelezi leo, Mheshimiwa Waziri, nachukua nafasi hii kukualika naomba uje tutembee na wewe kijiji kwa kijiji, eneo kwa eneo ujue umaskini ulioingia huko umasaini katika Wilaya za wafugaji hao kutokana na maeneo kutowatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Kanda yetu ya Kaskazini mwa Wilaya ya Simanjiro na Ukanda wa Mashariki, mvua iliyopita mwaka huu haijanesha katika ukanda huo, maana yake mifugo yote ya Simanjiro iko katika Kata mbili za Loiborsiret na zingine zimevuka mpaka kuingia Kata ya Makame na Ndedo katika Wilaya Kiteto.

Mheshimiwa Spika, kinachoendelea leo ni kutaka tena kuchukua maeneo yale na kuyageuza kuwa Hifadhi au Game reserve au Game Controlled Area. Ninataka niiombe Serikali yangu sikivu ya CCM kwamba jambo hili naomba mliache. Liacheni maana maamuzi yenu haya ya juu yasiyo shirikishi, yana athari kubwa katika ngazi za msingi, ngazi zetu za Majimbo, Kata, Vijiji na Mitaa. Tunaomba sana tushirikishane.

Mheshimiwa Spika, ushirikishwaji unaotakiwa kwa mujibu wa sheria, kushirikisha Mamlaka za Serikali za Mitaa katika ardhi za vijiji ni mikutano mikuu ya vijiji, Halmashauri za Vijiji na Halmashauri za Wilaya ziweze kutoa maoni yao juu ya namna bora ya kutoka pale. Ninaimani sana na Mheshimiwa Mchengerwa, ninaomba ufike uione hali halisi, usiletewe na wataalam usije ukauziwa mbuzi kwenye gunia.

Mheshimiwa Spika, juzi liliendelea zoezi moja lililokuwa Kimotoro Kata ya Kimotoro katika Wilaya ya Simanjiro na kijiji kilichopo Wilaya ya Kiteto katika eneo linalopakana na Mkungunero Game Reserve, kinachoshangaza Mawaziri Nane wakiongozwa na Mheshimiwa William Vangimembe Lukuvi, walifika katika maeneo hayo na kueleza maeneo ambayo Serikali imeridhia kuyarudisha kwa wananchi. Kilichokuja kutekelezwa katika uhalisia wake siyo kile ambacho kilitangazwa na Mheshimiwa Lukuvi.

Mheshimiwa Spika, kinachoogopesha kuliko yote kwa sababu mpaka wa Simanjiro na Kondoa ndiyo mpaka wa Mkoa wa Manyara na Mkoa wa Dodoma, kilichokuja kujitokeza katika tafsiri iliyokuwa inafanywa pale, kimsingi hata mtu aliyeishia darasa la saba anajua kabisa kwamba kilichofanyika hapa siyo sahihi, ninaomba Waziri mkae na Makongoro Nyerere awasaidie. Makongoro Nyerere alikuwa sahihi katika suala la mpaka wa Dodoma na Manyara kwa maana ya mpaka wa Wilaya ya Kondoa na mpaka wa Wilaya ya Simanjiro.

Mheshimiwa Spika, ile GN iko bayana hauhitaji kwenda kwenye darasa kubwa sana ili kujua, unaambiwa tu wazi kwamba, unatoka katika Mlima uliotajwa kwenye GN hiyo ya kuanzisha Wilaya ya Masai ambayo ndiyo GN ya kuanzisha Wilaya ya Kondoa, inaweka bayana kabisa na ninaomba ninukuu na ninatangaza tu point moja ambayo ndiyo inaleta mgogoro na ndiyo GN ilipo, inasema wazi kwamba, “… South - South East to a point four Miles, West South West of Mikuyuni Mikunga ….”

Mheshimiwa Spika, Mikuyuni Mikunga ndiyo beacon tunayogombania na wenzetu ambayo inahamisha leo nusu ya Kitongoji cha Kijiji cha Kimotoro kwenda Wilaya ya Kondoa. Badala ya kwenda hiyo Magharibi mile Nne ambayo Mlima uko hapa nilipo, kisima kipo hapo alipokaa Waziri wa Nchi, unatarajia Four Miles West South West ya alipokaa Mheshimiwa Jafo ndiyo inafanya kuwa kile kisima kinachotamkwa. West south west Four miles, kama hapo ulipo maana yake unakwenda kulia lakini wao wanakwenda kule alikokaa Mheshimiwa Waziri wa Madini.

Mheshimiwa Spika, sasa unajiuliza hapa nilipo ndiyo mlima ulipo unaambiwa nenda west south west four miles kutoka kwenye kisima hicho ambako ndiko aliko Mheshimiwa Jafo, badala ya kunyooka kwenda kutafuta point upande wa Magharibi, unakwenda kutafuta point upande wa Mashariki na kuweka jiwe, kwa maana hiyo, unahamisha mpaka wa Mkoa badala ya kwenda magharibi ambayo inaingia TANAPA ndani ya eneo la Tarangire unalazimisha kwenda mashariki ambapo unaathiri Kijiji kizima cha Kimotoro kuihamishia Wilaya ya Kondoa.

Mheshimiwa Spika, sasa GN hii ni yam waka 1961 GN Na. 65…

SPIKA: Mheshimiwa, dakika moja malizia mchango wako muda umekwisha.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, naomba tu uniongeze dakika moja ikikupendeza.

SPIKA: Mheshimiwa, ndiyo hiyo niliyokuongeza.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, ninashukuru Mkuu.

Mheshimiwa Spika, maana yangu ni nini? Kiacheni kitongoji cha Arkasupai kilichopo pale Kimotoro katika Wilaya ya Simanjiro kwa sababu GN yenyewe inawataka wabaki pale. Ninaomba Mawaziri mje wenyewe mshuhudie tafsiri potofu iliyotolewa hapo. Hatuna taabu hata ikitamkwa kwamba mpaka ndiyo huu lakini Rais anahitaji eneo hili kwa ajili ya hifadhi. Sisi ni wahifadhi lakini zaidi Mheshimiwa Waziri nikualike tuangalie njia za mapito ya wanyama uone jinsi sisi tulivyo wahifadhi wazuri. Angalia eneo la Natron linaathiri mno Longido, angalia lile eneo lingine la GN zile GSA za Simanjiro tusaidie ili tutoke pale.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nikiwa ninaimani kabisa kwamba Mheshimiwa Mchengerwa atatupatia muda wake wa ziada basi ninaomba niunge mkono hoja katika mapendekezo haya yote mawili na ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutubeba katika barabara yetu kubwa ya kihistoria. (Makofi)