Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, niongeze mchango kwenye hoja zilizoko mbele yetu leo. Kwa pekee kabisa niungane na wenzangu kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya ya kujali Maisha ya wananchi wa nchi hii. mazimio haya ni Ushahidi wa moja kwa moja wa Mheshimiwa Rais namna anavyowajali na kuwapenda na kuwasikiliza Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wameifanya kwenye kuchakata na kuandaa mazimio haya ambapo kufikia hatua hii kuja kujadiliwa ndani ya Bunge lako. Mwisho kwenye pongezi nikupongeze wewe mwenyewe na nikushukuru kwa namna ulivyotoa uongozi mzuri uongozi imara kwenye jambo hili mpaka tumefika hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama niongeze mchango kidogo na nianze kwa kuwaambia Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako Tukufu Kamati yako ya Bunge ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii inayofanya kazi kwa niaba ya Bunge lako kulisimamia na kuishauri Serikali kwa upande wa Wizara ya Ardhi na Wizara ya Maliasili na Utalii. Kwenye jambo hili imefanya kazi hii kwa umakini mkubwa sana. Imefanya kazi hii kwa kuangalia na ku-balance maslahi makubwa ya Taifa na kuangalia Maisha ya wananchi wa nchi ya Tanzania. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono mazimio haya na kuwasaidia watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nitoe mchango kwenye maeneo hayo mawili. Eneo la kwanza kwenye eneo hili la Ruaha kama tulivyosema tunaipongeza Serikali kwa kazi hii nzuri lakini kwenye mchakato wa jambo la Ruaha nimejifunza mambo makubwa mawili ambayo naomba Serikali niishauri. Moja, nimejifunza kwamba Elimu kwa watu wetu juu ya tunayoyafanya kwa ajili ya Maisha yetu lakini kwa ajili ya nchi yetu ni jambo muhiu sana. Niiombe sana Serikali si kwenye jambo hili, siyo kwa mamlaka ya maliasili peke yake lakini Elimu kwa wananchi wetu ni jambo muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nimejifunza, Serikali inafanya kazi kubwa inafanya kazi nzuri. Niwaombe Serikali iendelee kukubali kuwa na moyo huu mzuri wa kutafakari na kufikiria Maisha ya watu wetu wanaotoka kwenye jambo hili la Ruaha. Kwenye kazi iliyofanywa na Timu ya Mawaziri Nane mapendekezo yaliyotolewa kwenye kushughulikia jambo la Ruaha moja ya jambo nililojifunza yako baadhi ya maeneo machache ambayo taarifa zilizotumika kufikia maamuzi yale hazikuwa zimekaa sahihi kule uwandani kule chini kwenye ardhi. Naishukuru Serikali kwa busara yake baada ya kuona kuna haja ya kuongeza vitu vya ziada Serikali imefanya hivyo na leo tumefika hapa kuja kwenye haya maazimio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana Serikali nitoe mfano tu wa kule Tanga kwenye eneo la Kaka yangu Mkinga, kwa Mheshimiwa kaka yangu Kitandula, Wilaya ya Korogwe kuna eneo kule kwenye Mto Umba, eneo la Bonde la Umba kuna eneo kwenye Kata ya Mwakijembe, kuna eneo kwenye Kata ya Kalawani kwenye Wilaya ya Korogwe taarifa zilizotumika tunaamini wataalam wakienda uwandani watakuja na picha kamili ya kusaidia kutatua mgogoro huu na kuwanufaisha wananchi kama vile wananchi wa Ruaha wanakwenda kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyohivyo na kwenye Kata ya Magambo kwa Lukonge kwenye Jimbo la Korogwe Vijijini kwenye Kijiji kile cha Magamba kwa Lukonge eneo la Chang’andi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri wa Maliasili tutume tena timu yale maeneo ambayo bado wataalam wetu hawajarudi kwa mara ya pili, wakafanye uhakiki wa hali iliyopo kule chini pia tujitahidi kuongeza kasi ili maeneo yale yote ambayo yalipitiwa na Timu ya Mawaziri nane kazi ambayo mmewaachia wakuu wa mikoa ifanyike ikamilike ili tufunge mambo haya mogogoro hii iwe imekwisha na itakuwa ni utatuzi wa kudumu kwa migogoro hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la pili eneo la Hifadhi ya Kigosi, nirudishe tu historia kidogo kwa Neema ya Mungu nilipata nafasi ya kuwa sehemu ya Bunge la 11 mwaka 2019 nikiwa Mjumbe wa Kamati, ndiye niliweka mezani Taarifa ya Kamati kuhusu maoni kuhusu kupandisha hadhi eneo la Hifadhi ya Ugalla na Hifadhi ya Kigosi kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, kama kuna kazi ngumu tuliwahi kufanya kwenye Bunge hili ilikuwa ni kazi ya kupandisha Kigosi na kupandisha Ugalla. Wabunge wa maeneo haya walikuja wakilia walikuja wakilalamika wanaomba maeneo haya yasipandishwe hadhi ili wananchi wao wapate maeneo ya kufanya shughuli zao kwa sababu ya mazingira na sababu mbalimbali jambo hili halikuwezejana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee tumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hiki kilichokuwa kinafanyika sasa. Kimekuwa ni kilio cha muda mrefu sana cha watu hawa kimekuwa ni kilio kikubwa cha Wabunge na wananchi wa maeneo haya. Ninaamini jambo hili linalokwenda kufanyika linakwenda kuwafanya wananchi wa maeneo yanayokaribiana na eneo la Kigosi yanayonufaika na eneo la Kigosi kurudisha moyo wa kuendelea kuipenda na kuithamini Serikali. Ninaomba jambo hili likasimamiwe vizuri lifanyike vizuri ili mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho ninaushauri kwenye maeneo madogo matatu; moja tuna hifadhi nyingi sana za Taifa lakini hifadhi zetu nyingi hazifanyi vizuri na kwenye uhifadhi, Hifadhi ya Taifa ndiyo hatua ya juu kabisa ya uhifadhi ambayo kwenye hatua hiyo shughuli za kibinadamu haziruhusiwi kabisa. Ni wakati sasa kama nchi tufanye tathmini sahihi kuhusu hifadhi zetu za Taifa zipi zinafanya vizuri, zipi ambazo tunaweza tukazibadilisha baadaye kupata mapori ya akiba ili mambo yaweze kwenda vizuri. Lakini kama yako maeneo ya kupandisha na kwenyewe pia yaendelee kupandishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili kama nilivyosema tuongeze kasi kwenye kukamilisha utatuzi wa migogoro yale maeneo ambayo Kamati ya Mawaziri nane imefika.

Mheshimiwa Spika, jambo la nne niishauri Wizara, mambo yanayokwenda kufanyika na mazimio haya yanatusaidia kupunguza migogoro kati ya wananchi na hifadhi wananchi na Serikali. Lakini hii peke yake haitoshi Mheshimiwa Waziri ni wakati sasa na Mheshimiwa Rais alishasema na ametoa maelekezo kalitafakarini upya namna ya kuliboresha na kuliimarisha Jeshi Usu ili kulipa elimu zaidi kulipa weledi zaidi na kulifanya liwe rafiki na wananchi tupunguze migogoro kwenye haya maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ni wakati wa kwenda kuliunganisha Jeshi hili, leo tunakwenda kuirudisha Kigosi ambayo ni kubwa sana, moja ya sababu tutaipandisha wakati huo na mambo ya kiusalama pia yalikuwepo. Tutampa TFS kufanya kazi lakini tusipoliimarisha jeshi hili tunahitaji utunzaji na uangalizi zaidi wa weledi na taaluma wanaopewa watu wa misitu ili mambo yaweze kwenda vizuri. Tukaliimarishe Jeshi Usu ili mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nishauri, narudia tena kwa mara nyingine na nitaendelea kurudia hili. Kama nchi tukajidhatiti kwenye eneo la mipango ya matumizi bora ya ardhi. Siyo kweli kwamba tuna uhaba mkubwa kiasi hicho wa maeneo ya kufanya shughuli maeneo ya kulima, maeneo ya kuchunga na maeneo mengine. Moja ya changamoto tuliyonayo hatujatengeneza mipango vizuri ya matumizi ya maeneo yetu. Kuna ranch nyingi lakini ng’ombe wanaletwa maeneo ya kwenda kufuata malisho lakini ranch tunazo nyingi. Niombe sana Serikali jambo hili tukalipe uzito kwa wakati tuliokuwa nao ili mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hojanakubaliana na mazimio yote mawili nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)