Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wanasayansi wa zamani, Hippocrates na Thomas Edison waliwahi kusema madaktari wa karne ya 21 watatumia lishe bora katika tiba badala ya kutumia madawa ya kemikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunatambua umuhimu wa lishe bora katika afya ya jamii. Niwakumbushe tu mwaka 2020 wakati wa ugonjwa wa Corona ulivyopamba moto katika nchi yetu, Watanzania mbalimbali wakiwemo baadhi ya Waheshimiwa wenzetu Wabunge walitengeneza dawa asili kwa ajili ya kupambana na ugonjwa wa Corona na kusema kweli dawa hizo zilitusaidia kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja linanisikitisha sana ninapoona Serikali yetu inatumia kiasi kikubwa sana cha fedha za kigeni kwa ajili ya kuagiza bidhaa hasa za chakula ambazo tunaweza tukazizalisha hapa nchini kwa ubora wa hali ya juu sana. Tunaagiza maziwa ya unga wakati Tanzania tuna ng’ombe wapatao milioni 23; tunaagiza juisi za matunda wakati Tanzania ina matunda ya kila aina yanaoyoharibika kwa kukosa soko; tunaagiza mayai na kuku, wakati Tanzania tuna kuku wa kila aina; tunaagiza dawa ambazo tungeweza kuzitengeneza hapa hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti na ndugu zangu, jambo linalonisikitisha zaidi, watoto wa Watanzania ambao ni warithi wetu, tunawalisha vyakula ambavyo vina kiwango kikubwa sana cha sukari na protini yenye kiwango duni sana. Matokeo yake ni nini? Tunadumaza akili na miili ya watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawezaje kama Taifa kuingia katika karne ya 21 tukiwa na watoto ambao uwezo wao wa kufikiri ni umedumaa sana? Sasa niliwahi kusoma mahali, nikawa natafuta siri ya Waisraeli kuwa na watoto wenye kipawa cha hali ya juu sana na nikabaini kumbe hakuna siri, jambo lililo wazi ni lishe bora ndugu zangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mawazo yangu nafikiri sasa wakati umefika sisi kama Taifa tufanye uamuzi wa kimapinduzi, tuiangalie mitaala yetu ya shule za udakitari na sayansi ile ya tiba, badala ya kusisitiza kwenye matumizi ya madawa yasiyokuwa na ulazima, tusisitize kwenye sayansi ya lishe na tiba ya asili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nayasema haya? Inasikitisha sana unapokwenda hospitali kwa ugonjwa tu wa kawaida, mfano una upungufu wa madini fulani fulani, au upungufu wa vitamini, basi madaktari wanakukusanyia multivitamin chungu nzima. Unaweza kwenda hospitali tu una kikohozi au una mafua, badala ya kupewa orodha ya vyakula ambavyo vinaweza kukusaidia na kurudisha haraka afya yako, basi madaktari wanakukusanyia madawa chungu zima. Ndiyo maana napendekeza tuiangalie mitaala yetu, badala ya kung’ang’ania tu kufundisha masomo kama pharmacology ambayo yanasisitiza na kuendeleza soko la madawa ya kemikali kutoka nje, sasa tuweke mkazo kwenye sayansia ya lishe na tiba ya asili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wakati Marehemu Baba wa Taifa aliwahi kufanya mipango kwamba sayansi ya lishe na tiba asili ziingizwe katika mifumo rasmi ya Serikali; matabibu wa hospitali, shule za utabibu kama nilivyosema, ziwe zinasisitiza juu ya masuala haya. Kwa bahati mbaya sana jambo hilo jema hatukulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu ana msemo wake maarufu sana na naomba niurudie hapa, anasema hivi: “Waafrika ni watu wa ajabu sana. Wanapoona Wazungu wanafanya jambo hata kama ni la kijinga, watalifurahia, lakini Mwafrika anapofanya jambo hata liwe la maana la kiasi gani, wanalipuuza.” Sasa ndugu zangu mimi nasema masuala ya umuhimu wa lishe na sayansi ya lishe na tiba asili siyo jambo jipya, lakini kwa sababu tu pengine amelisema Thomas Edison na Hippocrates, tunaweza kuliona ni jambo la ajabu. Jambo hili babu zetu, wazee wetu walilitambua zaidi ya miaka 1,000. Sasa nasema wakati umefika jambo hili tulifanyie kazi na tulipe uzito unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.