Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi jioni ya leo ili na mimi niweze kuzungumza kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mbogwe Mkoani Geita ili niweze kuwasilisha mawazo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi jioni hii ili niweze kuwasilisha mawazo ya wana Mbogwe. Kwa vile muda sio rafiki sana naomba niende haraka haraka, lakini ikikupendeza uniongeze kwa sababu ni mara ya pili tu toka Bunge lianze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na uwezo wa kuweza kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu kuweza kuwasilisha mawazo ya wananchi. Namshukuru Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi anazozifanya kwenye Taifa letu la Tanzania. Najua nguzo kubwa sasa hivi ni mkataba, wananchi wangu wangependa nilielezee suala la mkataba ambalo linagonga kichwa, kila mtu anajiuliza ni nini hatima yake, lakini muda hautoshi. Niwaombe wananchi wangu wa Mbogwe ninakuja mwezi wa saba, tutakuja tufafanuliane na tuelimishane vizuri kuhusiana na hilo suala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niwatoe wasiwasi, hakuna kitu cha kuharibika mbele ya Mama yetu ambaye ni Amiri Jeshi wetu Mkuu. Kwa hiyo Watanzania muwe na imani kabisa, kwamba nchi iko salama, na bandari haijauzwa. Hayo maneno mnayoambiwa mitaani yapuuzeni, hakuna kitu kama hicho, wala kufikiria suala kama hilo. Na mimi mwakilishi wenu mliniamini na endeleeni kuniamini hivyo hivyo, na mimi ninasimama kwa ajili yenu kuhakikisha kwamba hakuna jambo la kuharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwako, Waziri wa Fedha. Kwanza nikupongeze sana kaka yangu, wewe ni Waziri wa Fedha, ni sekta ambayo ni ngumu kuliko Wizara zote, maana wewe ndiwe umeshikilia fedha. Nikuombee tu kwa Mwenyezi Mungu. Mawe unayopigwa endelea kuvumilia. Hata Yesu alipigwa, wengine walisema alikuwa mwizi wa mbao lakini ki ukweli alikuwa anaponya watu. Kwa hiyo na wewe simama kuhakikisha kwamba Taifa letu tunakwenda vizuri na tuweze kukidhi mahitaji ya watu wetu waliotuchagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kushauri mambo mawili makubwa. Nimeona kwenye mpango huu Mheshimiwa Waziri amedhamiria kwenda kumwongezea mchimbaji asilimia mbili, naomba hiyo hebu aiache, maana itatuletea kero ambayo haitaisha tena; kwa sababu mpaka sasa hivi wanalipa rate ya asilimia saba lakini vile vile wachimbaji hawa wanakabiliwa na service levy, kwa hiyo ukiweka asilimia mbili tena itakuwa asilimia 9.3. Hii nikumwongezea mzigo mchimbaji na kumuumiza kumtoa barabarani na kusababisha utoroshwaji tena wa madini uendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka mwaka 2017, lengo la kuweka asilimia saba lilikuwa kwamba ninyi Serikali mtajuana huko; nne itaenda madini tatu itaenda TRA. Kwa hiyo hata sasa hivi niwaombe Serikali, kwa kuwa ni wamoja kaeni kwa ajili ya kutupunguzia adha au balaa wale tunaoishi kwenye maeneo ya madini. Muwe mnagawana tu humo kwenye asilimia saba, mtakuwa mnajua wenyewe hii inaenda TRA, hii inaenda madini ili watu waendelee kuzalisha dhahabu na kuchimba na wao waweze kutoka kwenye wimbi la umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili napenda nikushauri Mheshimiwa Waziri, kwenye suala la mafuta kuongezea tena shilingi mia moja, na lenyewe mimi nisingependa iongezeke hiyo shilingi mia moja, itoe. Tunavyo vyanzo vingi vya mapato kwenye Taifa hili ikiwemo Sheria tuliyopitisha ya miamala, najua ni trilioni nyingi tu tutaingiza kama usimamizi ni mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile bandarini pale mpaka sasa hivi kuna wafanyabiashara tuna ushahidi kabisa hawatoi hata risiti. Weka usimamizi mzuri kwenye maduka hayo makubwa ya Kariakoo ili watu waweze kuchangia Pato la Taifa. Nina imani hauta-fail popote pale nakuomba sana kaka yangu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine kwa kuwa hii ni bajeti kuu nizungumzie upande wa maliasili. Ninalo pori pale Mkweni wananchi wangu wanakaa kwa kubanana. Kwenye ahadi zetu kwenye Ilani, tulifanya mikutano mingi tukawaaminisha watu kwamba tutatenga maeneo kwa ajili ya kuchungia ng’ombe. Nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii atenge muda na siku aje anitembelee Wilayani Mbogwe aje alione hilo pori la Kigosi ambalo halina faida kabisa, maana hata wanyama walikwisha, sifa za kuwa pori ilikwishaisha, matokeo yake limekuwa pori la kusulubisha watu, kukamata watu wauza mikaa pamoja na watu wengine. Kwa hiyo niombe tutakapolimaliza Bunge hili Mheshimiwa Mchengerwa aje anitembelee kwenye Wilaya yangu ili kusudi tuangalia hayo maeneo tuweze kuwafungulia wananchi tuweze kuchungia maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niguse Wizara ya ujenzi. Tunazo barabara ambazo walitutengenezea kweli mwaka jana lakini mvua zimenyesha hizo barabara zimeharibika. Nakumbuka mwaka 2021 nilimuomba kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwamba kwenye bajeti zake hizi aniruhusu kwenye halmashauri yangu ninunue caterpillar. Nimeandika andiko maalum naomba ani-support kaka yangu kwenye Wizara yake ya Fedha, twende tukanunue grader ili barabara zinapokatika mvua zinaponyesha tuwe na uwezo wa kutengeneza barabara wenyewe kuliko kusubiria masuala ya bajeti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: … bao kuna matatizo makubwa kusubiria hizi bajeti, mvua zinaponyesha barabara zinakatika wananchi wanashindwa kupita, matokeo yake wanamuona Mbunge hafai, Rais hafai, chama hakifai lakini kumbe dhamira ni nzuri…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nicodemas Maganga, ahsante sana.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: …nitengee hii bajeti na andiko langu unipitishie Wizarani ili kusudi niweze kununua caterpillar. Baada ya kusema hayo machache na mengi nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)